HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

September 12, 2019

RITA YAKISAPOTI CHAMA CHA WASIOONA DAR

KAIMU Ofisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili Ufilisi na Udhamini (RITA), Emmy Hudson, amesema taasisi hiyo inathamini makundi yote ya jamii katika kutoa huduma ikiwemo cheti cha kuzaliwa, vizazi na vifo, wosia, udhamini na kuyataka makundi hayo kujitokeza kupata huduma
hizo.

Aliyataja makundi hayo ni pamoja watu wenye ulemavu wa viungo, ikiwemo wasioona, walemavu wa miguu,wenye watoto wadogo,wamama wajawazito na wazee na hivyo kutengewa dawati lao kwa ajili ya kuwahudumia.

Akizungumza jijini Dar es Salaam mara baada ya kutoa hundi ya Shilingi Milioni moja kwa Chama cha wasioona cha Mkoa wa Dar es Salaam, Mtendaji huyo alisema kuwa kwa sasa ofisi yao imeweka dawati maalum la kuhudumia watu hao na kuwataka wasijifiche na kukosa huduma hizo muhimu. 

Fedha hizo ni kwa ajili ya kuwasaidia udhamini wa chama hicho kwenda kwenye maonesho ya siku ya fimbo nyeupe ambapo kimataifa inafanyika Oktoba 10 mpaka 15 na kitaifa inaadhimishwa Kigoma Oktoba 22 mpaka 24.

“Watu wa makundi maalum nao wanahitaji kupata huduma zetu na tumekuwa tunatoa elimu mbalimbali kwa jamii kwamba hata watu hao wanahitaji cheti cha kuzaliwa,kuandika wosia na hata kuanzisha taasisi zao kwa kufuata sheria mbalimbali za udhamini katika ofisi yetu,’’alisema Emmy.

Alisema ofisi ya RITA pia itafika Kigoma kwa ajili ya kutoa elimu hiyo kwa wenye makundi maalum ili waweze kupata huduma kama ambavyo wamekuwa wakipata wananchi wengine.; Kwa upande wa Mwenyekiti wa chama hiko mkoa wa Dar es Salaam, Paul Mathias aliishukuru RITA kwa kusikia kilio cha kuomba udhamini huku akizitaka taasisi nyingine kufanya hivyo ili kufanikisha safari yao ya kwenda Kigoma.

Hata hivyo alizitaka jamii kutoacha kuficha watoto wenye ulemavu ndani na badala yake kuwatoa kwa ajili ya kupata huduma mbalimbali za kijamii.

Mwenyekiti huyo alimuomba Mtendaji Emmy kuhakikisha wanapata huduma kwa kutumia vifaa vyao maalum ikiwemo Nukta nundu ambazo wamekuwa wakitumia hata katika masomo yao.

Naye Mtendaji Emmy aliwaeleza suala hilo litafuatiliwa serikali kuona wanapata huduma zao mbalimbali kwa vifaa maalum ambavyo ni nukta Nundu katika kujisajili kwa huduma mbalimbali. 

Naye Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya maonesho hayo Iddi Kiwimbi alisema mpaka sasa kuna uhitaji wa ufadhili mbalimbali ikiwemo tisheti 200,fimbo nyeupe 300, ambazo zitasaidia hata kwa ambao hawatafanikiwa kuhudhuria maadhimisho hayo. 

Naye Lucy Bupamba mjumbe wa kamati ya maandalizi naye aliwashukuru RITA huku akiwataka wengine kujitokeza lakini aliiomba jamii hasa wanawake kuacha kufichan watoto wao wenye ulemavu majumbani na badala yake wanatakiwa kuwapeleka kupata elimu,ambayo itawasaidia katika maisha ya kila siku.

No comments:

Post a Comment

Pages