HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

September 12, 2019

TTCS yaja na igizo la ‘Misitu Yetu Maisha Yetu’

NA SULEIMAN MSUYA

KATIKA kuhakikisha kuwa rasilimali misitu nchini inakuwa endelevu Mradi wa Mkaa Endelevu Tanzania (TTCS), umetengeneza igizo la ‘Misitu Yetu Maisha Yetu’ ili kulinda rasilimali hiyo muhimu kwa maisha ya viumbe hai.
Akizungumzia igizo hilo, Ofisa Uhusiano wa Shirika la Kuhifadhi Misitu Asili Tanzania (TFCG), Bettie Luwuge alisema wameamua kuja na mfumo wa igizo ili elimu ya uhifadhi misitu iweze kusambaa zaidi.
Luwuge alisema igizo hilo ambalo limetengenezwa katika mazingira ya vijiji vinavyojihusisha na Usimamizi wa Misitu ya Shirikishi ya Vijiji (USM), limejikita katika utoaji wa elimu zaidi.
“Sisi TFCG ambao ndio wawezeshaji wa mradi wa TTCS tumeamua kuja na igizo lenye ujumbe wa USM tukiamini rasilimali misitu itakuwa salama kwani wananchi wengi watanufaika zaidi,” alisema.
Alisema igizo hilo limeshirikisha waigiza wakubwa na wadogo ambapo matumaini yao ni kuona ujumbe unafika kwa haraka kwa jamii.
Ofisa Uhusiano huyo alisema matarajio yao ni kuona wananchi wanashiriki katika USM ili kuweza kunusuru misitu ambayo ina mchango mkubwa katika maisha yao ya kila siku.
Kwa upande wake Ofisa Uraghibishaji wa Mtandao wa Jamii wa Usimamizi wa Misitu Tanzania  (Mjumita), Elida Fundi alisema igizo hilo ambalo limejikita katika kuongelea hali halisi ya uharibifu wa misitu nchini litakuwa linarushwa katika vituo vya televisheni na redio ili kufikia wananchi wengi zaidi.
“Tumeamua kutumia njia ya igizo ili kuanisha visababishi vikuu vya uharibifu wa misitu kwenye ardhi za vijiji na namna mpango shirikishi wa misitu unavyochangia kupunguza upotevu wa misitu,” alisema.
Fundi aliwataka wananchi kufutialia vipindi vya televisheni kuanzia kesho kwenye televisheni za ITV, EATV na nyinginezo ili kupata elimu hiyo muhimu ya USM.
Alisema iwapo jamii kubwa itapata uelewa wa USM ni dhahiri misitu itakuwa salama na malalamiko ya manadiliko ya tabia nchi ambayo yanalalamikiwa kila mara yatakuwa yamedhibitiwa.

No comments:

Post a Comment

Pages