HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

December 13, 2020

KITABU CHENYE HISTORIA YA WAKIMBIZI KUANDIKWA NCHINI

 

Mkimbizi kutoka DRC Congo, Ebengo Waluta, akielezea namna alivyojikuta anakuwa mkimbizi mbele ya washiriki wa semina iliyoandaliwa na Diginity Kwanza.

 Ofisa Hifadhi na Sheria wa Idara ya Huduma kwa Wakimbizi, Asnath Barnabas akitoa mada kuhusu Sheria ya Wakimbizi ya mwaka 1998 kwa wa washiriki wa semina iliyoandaliwa na Diginity Kwanza.

 

NA SULEIMAN MSUYA

 

KATIKA kuhakikisha Watanzania wanaelewa historia ya nchi yao katika kupokea na kuhifadhi wakimbizi wadau mbalimbali wanashirikiana na Serikali wanaandika kitabu kitakacho elezea historia hiyo kwa miaka 60 iliyopita.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Diginity Kwanza Janemary Ruhundwa, wakati akizungumza na waandishi wa habari na wadau kutoka Asasi za Kiraia (CSOs) katika warsha ya siku mbili iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Ruhundwa amesema Diginity Kwanza inashiriki mchakato huo kama mratibu lengo likiwa ni kuhakikisha historia ya zaidi ya miaka 60 ya ushiriki wa Tanzania kupokea na kuhifadhi wakimbizi inawekwa kwenye maandishi na usahihi.

"Tumewaita nyie waandishi wa habari na CSOs ili muelewe kinachofanyika kwenye mchakato wa kuandika kitabu hiki ambacho kitaonesha miaka 60 ya ushiriki wetu kwenye kupokea na kuhifadhi wakimbizi.

Kitabu hiki kitandikwa na sisi Watanzania wenyewe hivyo tumeamua kukutana na Watanzania wote ambao watakuwa na taarifa kuhusu wakimbizi," amesema.

Amesema wao kama Diginity Kwanza wanaamini historia hiyo itasaidia jamii kuelewa mchango wa nchi kwenye eneo hilo.

"Pamoja na juhudi za Serikali kutekeleza miradi ya maendeleo pia eneo la wakimbizi Tanzania imefanya mambo makubwa sana ndio tunataka kuyaanisha kwenye kitabu sasa," amesema.

Ruhundwa amesema matarajio yao ni kitabu hicho cha miaka 60 ya kupokea na kuhifadhi wakimbizi kinakamilika mwishoni mwa mwaka 2021.

Mkurugenzi huyo amesema watahakikisha kitabu hicho kinaandikwa kwa lugha inayoeleweka kwa Watanzania wote.

"Naomba ndugu zangu waandishi mtumie kalamu zenu kuandika habari za wakimbizi kwa kina ili tuwe na kizazi chenye uelewa kwenye eneo hilo," amesema.

Ruhundwa amesema awali walifikiria kuandika kitabu cha kutumika vyuoni lakini baada ya mijadala wameona umuhimu wa kuwepo kitabu chenye kuhusisha Watanzania wote kwanza.

Amesema kumekuwepo na taarifa za utafiti kuhusu wakimbizi ambazo zinaandikwa na watu kutoka nje hivyo ni wakati muhimu kutumia wazawa kuandika historia hiyo muhimu kwa nchi.

Emmanuel Mgala wa Kituo cha Kusimamia, Mazingira na Utawala Bora amesema kitabu hicho kitafungua watu wengi kuhusu ukimbizi nchini hasa wale ambao wanaamini Tanzania haigharamiki kuhifadhi.

"Kitabu hiki ni fursa muhimu kwani watu watajua ukweli wa halisi ya nchi yao kwenye eneo la wakimbizi ambalo linachukuliwa kama jambo la kawaida," amesema.

Kwa upande wake Ruth Ndagu wa Kituo cha Msaada wa Sheria kwa Wanawake na Watoto (WLAC), amesema kitabu hicho kitakuwa na mchango mkubwa kwa Tanzania ambayo imekuwa ikipokea wakimbizi kwa miaka 60 na zaidi.

"Jamii itapata mwanga kuhusu dhana ya wakimbizi lakini pia tutaendelea kutunza amani yetu kwani ukimbizi sio jambo zuri," amesema.

Ndagu amesema kitabu hicho kitafungua ukurasa mpya kwa mashirika ya kimataifa kuongeza misaada katika eneo hilo.

Naye Saimon Samitei Meneja Mwandamizi wa Miradi Shirika la Relief to Developing Society (REDESO), amesema uandishi wa kitabu hicho kwa sasa ni wakati muafaka.

Amesema wadau wanapaswa kuunga mkono uandishi wa kitabu hicho ili kusaidia jamii ya Kitanzania kupata elimu.

Samitei amesema mchango wa Tanzania katika kuhifadhi wakimbizi ni mkubwa sana hivyo kitabu kinapaswa kuanisha kila kitu kwa kina.

Akizungumzia hisitoria ya miaka 60 ya kupokea na kuhifadhi wakimbizi nchini Ofisa Tawala Mkuu, Usimamizi wa Kambi na Makazi kutoka Idara ya Huduma kwa Wakimbizi, Stephen Msangi amesema imepitia changamoto na mafanikio hivyo kitabu hicho ni muhimu kuandikwa.

Msangi amesema kwa miaka 60 sasa Tanzania imepokea wakimbizi kutoka nchi ya Malawi, Msumbiji, DRC Congo, Burundi, Rwanda, Uganda na Kenya hivyo historia hiyo ikiandikwa iweze kuanisha uhalisia huo.

"Tumepokea wakimbizi wengi sana na wengine wameomba uraia wamekuwa Watanzania ila wengi werudi katika nchi zao haya yote yanapaswa kuwa kwenye kitabu," amesema.

Aidha, amesisitiza kitabu hicho kianishe changamoto ambazo nchi inakutana nazo katika kuwahifadhi wakimbizi ili Watanzania wajue.

Ofisa Hifadhi na Sheria wa Idara hiyo, Asnath Barnabas amesema kitabu hicho kitafungua ukurasa mpya kwenye eneo la wakimbizi nchini.


No comments:

Post a Comment

Pages