HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 17, 2022

BENKI YA CRDB, WIZARA YA MAMBO YA NJE ZASAINI MAKUBALIANO KUTENGENEZA MFUMO WA DIASPORA DIGITAL HUB

Na Mwandishi Wetu

BENKI ya CRDB na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wamesaini hati ya makubaliano ya kutengeneza mfumo wa kidigitali wa kutunza taarifa za Diaspora, (Diaspora Digital Hub).

Makubaliano hayo yamesainiwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, AbdulMajid Nsekela, katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo Jijini Dar es Salaam, Balozi Sokoine amesema mfumo huo wa kidigitali utaisaidia Serikali kuwatambua, kuwasajili na kuwawezesha Diaspora wa Tanzania waliopo sehemu mbalimbali ulimwenguni kupata huduma mbalimbali na kushiriki kidigitali katika shughuli mbalimbali za maendeleo, biashara, uchumi na uwekezaji.

“Ushirikiano wa Wizara na Benki ya CRDB ni wa muda mrefu na wenye mafanikio mengi katika kuendelea kusukuma gurudumu la maendeleo ya Tanzania. Wizara ina imani kuwa kupitia udhamini wa shilingi milioni 100 kutoka CRDB za kutengeneza mfumo wa Diaspora Digital Hub utaboresha huduma mbalimbali zenye kukidhi mahitaji ya Diaspora kote ulimwenguni,” amesema Balozi Sokoine

Balozi Sokoine ameongeza kuwa, mfumo huo pamoja na mambo mengine, utafungua uwezekano wa fursa zaidi za ushirikiano kati ya Wizara na Benki ya CRDB katika kazi ya uendelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ya Balozi za Tanzania nje ya nchi.

Balozi Sokoine ameyataja baadhi ya mafanikio ya mfumo huo ambayo ni kutekeleza kwa vitendo azma ya Serikali ya Tanzania kuhamasisha taasisi na watumishi wake kutumia ipasavyo mifumo ya kidigitali katika kutoa huduma ili kuendana na mabadiliko ya dunia na kuongeza tija katika utoaji wa huduma.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB Plc, Bw. AbdulMajid Nsekela amesema CRDB inaamini kuwa kuanza kwa Mfumo wa Kidigitali wa kutunza taarifa za Diaspora (Diaspora Digital Hub) utakuwa na manufaa mengi kwa Serikali na Benki ya CRDB kwa ujumla ikiwa ni pamoja na kusaidia kufahamu idadi ya Diaspora walioko ulimwenguni na kutunza taarifa za watanzania walioko nje.

“Diaspora Digital Hub itasaidia pia kupata taarifa za fursa za uwekezaji nchini na kuwatambua wawekezaji wenye nia ya kuwekeza nchini, kuisaidia Serikali katika zoezi la sensa litakalo fanyika mwezi Agosti, 2022, kusaidia kupata taarifa sahihi za pamoja na kuisaidia Wizara kupanga bajeti yake” amesema Bw. Nsekela

Bw. Nsekela ameongeza kuwa mfumo huo wa kidigitali utaisaidia Benki ya CRDB kuboresha zaidi huduma zake na kuwafikia wateja wengi wakiwemo Diaspora waliopo ulimwenguni.

“CRDB inaahidi kuendelea kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki katika kuhakikisha mfumo wa kidigitali wa Diaspora Digital Hub unakamilika kwa wakati,” amesema Bw. Nsekela

Mkurugenzi wa Kitengo cha Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi James Bwana akizungumza katika hafla hiyo amesema Mfumo wa kidigitali wa Diaspora Digital Hub utakapokamilika utaiwezesha Serikali kuwa na kanzidata ya uhakika kuhusu Diaspora kote ulimwenguni.

“Mfumo huu pia utaiwezesha Wizara kutekeleza majukumu yake kwa njia ya kidigitali ambapo uratibu wa masuala mbalimbali yanayotolewa katika mfumo huo utafanyika papo kwa papo.

Balozi Bwana aliongeza kuwa kupitia mfumo huo Serikali itaweza kufahamu kwa ufasaha idadi ya Diaspora, ujuzi, elimu walizonazo na mengine mengi. Kadhalika, Diaspora wenyewe wataweza kupata kupitia mfumo huo huduma mbalimbali kwa ajili ya mahitaji yao.

Ushirikiano wa Wizara ya Mambo ya Nje na Benki ya CRDB ni wa muda mrefu tangu 2010 wakati Kitengo cha Diaspora kilipoanzishwa. Ushirikiano huo umewezesha Benki ya CRDB PLC kuwa ya kwanza kuanzisha utoaji wa huduma kwa Diaspora ambapo hadi sasa zaidi ya Diaspora 30,000 wananufaika na huduma ya Tanzanite Account.

 

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela kwa pamoja na Katibu Mkuu Wizara la Mambo ya Nje na Ushikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine, wakitiliana saini hati ya makubaliano baina ya  Benki ya CRDB na Wizara kwa ajili ya utengenezaji wa mfumo wa kidigitali kwa Wantazania waishio nje ya nchi (Diaspora), utakaowawezesha kupata huduma mbalimbali wanazohitaji kutoka nyumbani Tanzania wakiwa  hukohuko ughaibuni. Mfumo huo utajumuisha watoa huduma wa Serikali kama; NIDA, UHAMIAJI & TIC pamoja na watoa huduma wengine ambao huduma zao zinawalenga Diaspora. Hafla hiyo imefanyila leo kwenye ofisi za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, jijini Dar es Salaam. Wengine pichani ni wanasheria wa pande zote mbili wakishuhudia.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela kwa pamoja na Katibu Mkuu Wizara la Mambo ya Nje na Ushikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine, wakibadilishana hati za makubaliano baina ya  Benki ya CRDB na Wizara baada ya kuzisiani kwa ajili ya utengenezaji wa mfumo wa kidigitali kwa Wantazania waishio nje ya nchi (Diaspora), utakaowawezesha kupata huduma mbalimbali wanazohitaji kutoka nyumbani Tanzania wakiwa  huko huko ughaibuni. Mfumo huo utajumuisha watoa huduma wa Serikali kama; NIDA, UHAMIAJI & TIC pamoja na watoa huduma wengine ambao huduma zao zinawalenga Diaspora. Hafla hiyo imefanyila leo kwenye ofisi za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, jijini Dar es Salaam. 


No comments:

Post a Comment

Pages