HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

April 22, 2024

JamiiForums yazindua Awamu ya Nne Shidano la Stories of Change, Wananchi wahamasishwa kushiriki kuibua Mawazo

Na Hussein Ndubikile, Dar es Salaam


Asasi ya Kiraia ya JamiiForums imezindua Awamu ya Nne ya Shindano la Stories of Change ambalo litaanza rasmi Mei Mosi mwaka huu, na kuisha baada ya miezi miwili.


Akizungumza na wanahabari jijini humo Mkurugenzi Mtendaji wa JamiiForums  Maxence Melo amesema kauli mbiu ya shindano la mwaka huu itakuwa "Tanzania Tuitakayo" ikilenga kuhamasisha wananchi kuibua mawazo mbadala ya nini kifanyike kuipata Tanzania iliyo bora zaidi kwa kupendekeza mawazo bunifu yanayoweza kutekelezeka ndani ya miaka mitano (5), 10, 15 hadi 25 ijayo.

"Katika Mpango Mkakati wake wa miaka mitano (2020-2024), JamiiForums ilibuni shindano la 'Stories of Change' lililoanza mwaka 2021. Na katika awamu tatu zilizopita, takribani machapisho 6,000 yaliwasilishwa na wananchi. Miongoni mwa maudhui yaliyowasilishwa, yamechangia kuboresha mifumo ya utoaji huduma katika Sekta ya Umma na Binafsi," amesema Melo.

Amebainisha kuwa shindano la mwaka huu asasi hiyo itashirikiana na mshirika wake wa muda mrefu, Twaweza pamoja na wadau wengine kutoka Serikalini, asasi za kiraia, mashirika yasiyo ya kiserikali na makampuni binafasi katika nyanja mbalimbali kama habari, elimu, vijana, wanawake, watoto, makundi maalumu, teknolojia, afya na kadhalika.

Amesisitiza kuwa lengo ni kuimarisha ushiriki wa wananchi na utekelezaji wa maoni ambapo amebainisha kuwa wadau hao ndio watakaoshiriki mchakato wa kupata na kuwatuza washindi wa kisekta.

Amevitaja vigezo na masharti ya kushiriki shindano hilo, ni kwamba mshiriki anatakiwa kutayarisha andiko linakoelezea Tanzania Tuitakayo lenye maono ya kibunifu ambayo yanaweza kutekelezeka ndani ya miaka mitano, 10, 15 hadi 25 ijayo katika nyanja mbalimbali mfamo elimu, afya, teknolojia, uchumi, mazingira, miundombinu na kadhalika.

Kwamba andiko liwe kwa lugha ya Kiswahili au Kiingereza  lenye maneno kuanzia 700 hadi 100, kadhalika matumizi ya picha, vieo na vielelezo vingine yanaruhusiwa ili kuongeza uzito wa wasilisho ambapo ikiwa picha au video zilizotumika si za mshiriki atatakiwa kutaja chanzo.

Ameongeza kuwa, machapisho yanatakiwa kuwa halisi na hayajawahi kuchapishwa sehemu nyingine yoyote, kwamba ubwakuzi hautaruhusiwa na kueleza kuwa maandiko yawasilishwe ndani ya miezi miwili kuanzia Mei 1, 2024 kwenye jukwaa la "Stories of Change 2024".

"Ili kushiriki, lazima mtu awe mwanachama aliyejisajili JamiiForums.com ili kuchapisha andiko lake kwenye jukwaa la shindano la "Stories of Change". Ikiwa sio mwanachama, anapaswa kujiandikisha kwa kufuata kiuongo hiki https://jamii.app/Signup," ameeleza Melo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Uchechemuzi wa Twaweza Annastazia Rugaba. ametoa rai kwa wananchi wote wenye miaka 18 na kuendelea kushiriki katika shindano hilo ili kutimiza haki yao ya msingi ya kuchangia mawazo katika kujenga Tanzania Tuitakayo.

Amesema washindi watatangazwa kwenye Jukwaa la JamiiForums "Stories of Change" na kurasa rasmi za JamiiForums katika mitandao ya kijamii na X, Facebook, Instagram, WhatsAPP na Telegram.

No comments:

Post a Comment

Pages