HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

April 16, 2015

Dk. Slaa anguruma Marekani

Dk Slaa , mkewe Josephine na Meya wa Indianapolis
Dk Slaa akitoa muhadhara.
Dk Slaa, mkewe Josephine na wataalamu wa Katiba, Profesa  J.M Curtis na Dickson Ramsey.

NA ANDREW MSECHU

KATIBU Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa amesema Tanzania imedumaa kutokana na Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho kimetawala kwa miaka zaidi ya 50 kushindwa kurutubisha rasilimali kwa manufaa ya wananchi na kwamba njia pekee ya kulikomboa taifa  ni kukiondoa madarakani kupitia sanduku la kura.

Dk. Slaa alisema CCM ni sawa ni saratani inayolitafuna taifa, kutokana na serikali yake kukosa maadili na kukumbatia makundi ya wahalifu waziwazi bila hata kuona aibu, huku wananchi wake wakiendelea kuteseka na kwamba Watanzania wameendelea kuwa wabeba mizigo badala ya kuwa washindani katika uchumi wa dunia.

Akiwahutubia mamia ya wanazuoni katika Chuo Kikuu cha Purdue, nchini Marekani, Dk. Slaa alisema njia pekee ya kulinusuru taifa na saratani hiyo, ni kuleta mabadiliko ya kweli kupitia sanduku la kura na kwamba tiba ni kumpata rais atakayetokana na vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).

“Bila shaka, haya ni mambo muhimu ambayo yanahitaji tuyazungumze sisi kama Watanzania  kwa kushirikiana na wadau wetu na marafiki kama nyie. 

Tunahitaji msaada wenu katika kukabiliana kuiondoa saratani hii CCM ili tuijenge jamii yetu kiuchumi,”alisema Dk. Slaa.
Alisema Tanzania ni maskini na kwamba watu wake ni maskini pia lakini jambo la kushangaza ni kwamba Rais Jakaya Kikwete aliwahi kusema hadharani kwamba hajui chanzo cha umaskini wa wananchi wake, kauli ambayo Dk. Slaa alisema ililenga kuficha ukweli wa ubadhirifu mbele ya mataifa ya nje.

“Mlishuhudia taarifa za kusikitisha sana na za aibu kutoka kwa mkuu wa nchi. Labda rais alikuwa akiona aibu kuuambia ukweli ulimwengu, kwamba kwa miaka 54 nchi inaugua saratani inayoitwa Chama Cha Mapinduzi,”alisema Dk. Slaa na kuongeza:

“Hii ni saratani ya kisiasa tangu kuanzishwa kwa taifa, chama ambacho kimekuwa kinara wa rushwa na ubadhirifu, ambacho kimekuwa hakina muda wa  kuangalia namna ya kuinua uchumi, zaidi kinaangalia namna ya kuomba misaada badala ya kuangalia namna ya kuboresha uzalishaji na uimarishaji wa rasilimali za taifa.”
Dk. Slaa alisema ni wazi saratani hiyo imeshalitafuna taifa kiasi cha kutosha na hata kusahau ilipoanzia na kwamba imelifanya kuwa miongoni mwa nchi maskini duniani kwa makusudi, hivyo njia pekee ya kuondokana na tatizo hilo ni kuhakikisha inaondolewa kwa kura.

Alisema chama hicho tawala kimekuwa kikwazo cha ukuaji wa uchumi kwa kuua ubunifu wa ndani na badala yake kimetengeneza mfumo wa  kuingiza bidhaa hatari zisizokuwa na viwango kutoka mashariki ya mbali. 

Aliongeza kuwa serikali imejaa viongozi wanaopandikiza mbegu ya ukabila kwa wananchi ili kutumia mwanya wa kugawanyika kwao kuwatawala, bila kujali athari za baadaye za mgawanyiko huo.

“Ni Tanzania pekee ambapo kutokana na utawala dhalimu wa CCM, maskini aliyeiba mbuzi kwa ajili ya kuinusuru familia yake na njaa anaweza kufungwa jela, lakini muuza dawa za kulevya, wahalifu wa kiuchumi na majangili (wauaji wa tembo) wanalindwa kwa gharama zote na CCM. Wale wanaoiba mabilioni ya fedha za umma wanatembelea magari na kupata ulinzi wa serikali,” alisema.

Katika hotuba yake hiyo, Dk. Slaa alisema ni Tanzania pekee ambayo wale wanaopigania masilahi na kuangalia namna ya kulinda rasilimali za nchi wanaitwa ‘magaidi’ na kwamba CCM kimekuwa kikitumia polisi na vyombo vya usalama si kulinda rais na mali zao, bali kukandamiza haki za wananchi.

“…ukiwa mwanachama wa upande wa upinzani, wewe ndiye shabaha ya kwanza ya askari polisi na adui namba moja wa dola,”alisema. 

Dk. Slaa alisema katika miaka yote ya utawala wake, serikali ya CCM imekuwa kikwazo cha Tanzania kuingia katika mapinduzi ya viwanda na kwamba imeua ndoto za mapinduzi ya kilimo.

Alisisitiza kwamba CCM ni chanzo cha kuharibika kwa huduma hata za afya, elimu na kufa kwa uchumi, mambo ambayo alisema yamekuwa kichocheo kikubwa cha kuwageuza wananchi na taifa lao kuwa wategemezi wa misaada na ombaomba, badala ya kuwa washiriki katika uchumi wa kimataifa.

Uhuru wa habari
Dk. Slaa ambaye yuko katika ziara ya kikazi ya siku tisa nchini Marekani, pia alizungumzia uhuru wa habari nchini akisema hali siyo nzuri kwani baadhi ya magazeti yamekuwa yakiandamwa na mengine kufungiwa kwa sababu ya kuanika uovu wa serikali na mengine kufungiwa kwa sababu ya kuchora vikaragosi tu.
Alisema baadhi ya waandishi wa habari wamekuwa wakikamatwa, kutishwa na hata kuuawa kikatili na vyombo vya usalama, pale wanapoandika habari zinazokinzana na maoni au mitazamo ya watawala.

Utajiri wa rasilimali
Akizungumzia utajiri wa rasilimali nchini, Dk. Slaa alisema Tanzania imejaliwa vyanzo vya asili na vyanzo mbadala vya nishati, kuanzia hifadhi kubwa ya gesi asilia (ujazo wa meta 47 trilioni za mraba), mito mikubwa, vyanzo muhimu kwa ajili ya umeme wa maji, jua na upepo kwa ajili ya nishati mbadala. 

Alisema kwa utajiri huo, nchi imegeuzwa kuwa sehemu ya watu kuvuna madini na kuondoka, kuzima ndoto za mamilioni ya vijana kupata ajira kiasi cha kusababisha suala hilo kuwa bomu linaloweza kulipuka na kusababisha matatizo makubwa katika nchi.

“Tanzania ina hifadhi kubwa yenye kila aina ya madini na vito kuliko inavyodhaniwa, Kuna uranium, makaa ya mawe, chuma, shaba, bauxite, almasi, akiki, nikeli, tanzanite, yakuti na mengine mengi ambayo hupatikana Tanzania, tena kwa wingi,” alisema.

Alisema kwamba hata hivyo, pamoja na utajiri huo mkubwa kitendawili ni kwamba Afrika na Tanzania bado zinaorodheshwa katika ‘nchi maskini’ duniani, wakati rasilimali hizo ni chanzo cha utajiri unaoweza kuinua taifa.

Alisema pamoja na madini, Tanzania pia ina utajiri mkubwa wa mifugo na kwamba inashika nafasi ya tatu duniani kwa wingi wa mifugo hasa ng’ombe, lakini cha kushangaza hata bidhaa za ngozi tu zinaagizwa kutoka nchi za nje.

Alisema baada ya kuingia madarakani, serikali ya upinzani kupitia Ukawa itahakikisha bidhaa zote za mazao ya mifugo zinazalishwa nchini, badala ya kuuza mazao hayo kwa bei nafuu na kwenda kurutubishwa nje kisha kurudishwa na kuuzwa kwa bei ya kutupa.
Alisistiza kwamba, hata utajiri wa dhahabu, Chadema inataka utumike vyema si kwa nia ya kuzuia kuuza nje, bali kuhakikisha inashughulikiwa na kusafishwa nchini ili kutoa ajira kwa Watanzania kisha kuuzwa nje kwa thamani halisi.

Muungano wa Ukawa
Dk. Slaa alitumia fursa ya Ukawa, akisema kwamba Chadema na vyama rafiki vya ndani; CUF, NCCR-Mageuzi na NLD vimeamua kuunda ushirikiano maalumu kwa ajili ya kuhakikisha wanakabiliana isapavyo na CCM.

Alisema kupitia ushirika wa Ukawa wamejipanga kurejesha heshima ya Tanzania iliyopotea na kwamba kipaumbele chao baada ya kuingia Ikulu kitakuwa ni kufuta aibu ya nchi kuwa ombaomba duniani.

Alisema badala yake wataelekeza nguvu katika kurutubisha utajiri wa nchi ili kulifanya taifa lisimame kiuchumi na kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kimataifa.

“Daima nimekuwa nikisisitiza kwamba Chadema tunatoa kipaumbele namba moja kwa elimu, na elimu pia ni kipaumbele namba mbili na elimu hiyohiyo ni kipaumbele namba tatu kwani ndiyo msingi wa maendeleo ya uchumi. Misaada ya kiuchumi si kipaumbele cha Chadema,” alisema.

Alisema hali hiyo inatokana na ukweli kwamba mafanikio ya kiuchumi ya Marekani na ya mataifa mengine ya magharibi yanatokana na uwekezaji wao katika elimu ambao umewezesha kupata rasilimaliwatu ya kukuza kilimo, viwanda na uhakika wa chakula.

Ziara ya Dk. Slaa nchini humo inatokana na mwaliko wa Gavana wa Jimbo la Indiana, Mike Pence pamoja na taasisi mbalimbali za nchini humo vikiwamo vyuo vikuu kutokana na kutambua mchango wake wa kisiasa na kijamii na chama chake katika maendeleo ya Bara la Afrika.

 Mbali na Chuo Kikuu cha Purdue, pia Dk. Slaa anatarajiwa kutoa mihadhara katika vyuo vikuu vya Indiana na Marion.
  CHANZO TANZANIA DAIMA

No comments:

Post a Comment

Pages