HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

August 07, 2017

Simbu ang’ara Mashindano ya Dunia

Mwanariadha Alphonce Simbu akipiga magoti kumshuluru Mungu baada ya kuibuka na ushindi wa tatu katika mashindano ya Dunia jijini London.
Simbu wa pili nyuma akimalizia mbio.

 LONDON, ENDLAND

MWANARIADHA Alphonce Simbu, jana ameing’arsha vilivyo Tanzania katika Mbio za Marathon za Mashindano ya Dunia yanayoendelea jijini hapa, baada ya kushika nafasi ya tatu na kutwaa medali ya shaba ya mashindano hayo.

Simbu alikimbia kwa saa 2:09.51 na kuibuka na medali ya Shaba, ingawa ameshuka kiwango cha muda wake aliokimbia katika London Marathon alikotumia saa 2:09.10.
Katika kinyang’anyiro hicho jana, Mkenya Geoffrey Kirui alimaliza kinara na kutwaa medali ya dhahabu ya mbio hizo, akitumia saa 2:08.27, huku nyota wa kimataifa wa Ethiopia, Tamirat Tola akishika nafasi ya pili ya mbio hizo.

Tamirat alikimbia akitumia saa 2:09.49, tofauti ya sekunde mbili tu na Simbu, ambaye amekuwa akiibeba mno Tanzania katika mashindano mbalimbali, kama alivyofanya London Marathon na Mumbai Standard Chartered Marathon.

Jijini Mumbai, India, Simbu, anayedhaminiwa na Kampuni ya Multichoice Tanzania, aliibuka mshindi kwa kutumia muda wa dakika 2:09:28 Januari mwaka huu, kabla ya Aprili kukimbia katika London Marathon alikotumia saa 2:09.10.

Katika Olimpiki ya Majira ya Joto jijini Rio de Janeiro Brazil mwaka jana, Simbu (24) alishika nafasi ya tano akitumia saa 2:11:15, sekunde 11 nyuma ya aliyeibuka mshindi wa nne, Ghirmay Ghebreslassie wa Ethiopia.

Dalili za Simbu kuibuka na medali katika kinyang’anyiro cha juzi zilianza kuonekana mapema wakiwa wamekimbia umbali wa kilomita 21, ambayo ni nusu marathon. 

Kwa kufanikiwa kutwaa shaba katika mbio za jana, Simbu ataondoka na kitita cha dola za Kimarekani 20,000, huku bingwa Kirui akizawadiwa dola 60,000 na mshindi wa pili, ambaye ni Tamirat akiondoka na dola 30,000.

Simbu anakuwa Mtanzania wa pili kunyakua medali katika Mashindano ya Dunia, yaliyo chini ya Shirikisho la Riadha la Kimataifa (IAAF), tangu kuasisiwa kwa mashindano hayo miaka 80 iliyopita.

Mtanzania wa kwanza kunyakua medali ya katika Mashindano ya Dunia ni Christopher Isegwe, aliyefanya hivyo kwenye mashindano yaliyofanyika mwaka 2005 jijini Helsinki nchini Finland, ambako alitumia saa 2:10.21.

Historia kwa ufupi

Ni kijana aliyeko kwenye kiwango kizuri hivi sasa, akiwa na historia ya kushiriki michezo ya Olimpiki mara moja, Rio Brazil mwaka jana.

Alizaliwa mwaka 1992 Kijiji cha Nampando Singida Mashariki (Ikungi), akiwa ni mtoto wa saba kati ya 10 wa Mzee Felix Simbu.

Anasema alianza kushiriki mchezo wa riadha akiwa Shule ya Msingi Nampando huko Singida kutokana na ushawishi wa Mwalimu Juma Jambau aliyekuwa akifundisha Shule ya jirani ya Lighwa.


Alphonce, anasema mwaka 2003 akiwa darasa la tano alijaribu kukimbia mbio za Km 5 ambazo zilifanyika Singida chini ya udhamini wa kampuni ya Puma, ambako baada ya hapo aliacha na kuendelea mambo mengine.

Mwaka 2005 alishiriki Babati Half Marathon, ambako kulikuwa na mbio za Km 5 kwa ajili ya wanafunzi na kushika nafasi ya tano, ambazo zilikuwa chini ya ufadhili wa mradi wa mazingira uliokuwa chini ya taasisi ya Lamp ya Sweden, ambao ulikuwa ukitoa nafasi ya watoto 20 kushiriki mbio hizo toka kila wilaya inakoendesha mradi huo.

“Mbio hizi nakumbuka tena nilikimbia peku peku, nilifanikiwa kushika nafasi ya tano, mbio hizi zilinisaidia kipaji changu kuonekana na kupata ufadhili kujiunga na shule ya vipaji ya Winning Spirit ya jijini Arusha.

Alijiunga na shule hiyo 2006 baada ya kuhitimu darasa la saba, ambako aliendelea na mazoezi na mwaka 2008 alishiriki mashindano ya Nyika (Cross Country), ya vijana Taifa, yaliyofanyika viwanja vya Gofu mjini Moshi, Kilimanjaro.

Anasema baada ya mashindano hayo alichaguliwa timu ya Taifa na kushiriki mashindano ya Afrika Mashariki yaliyofanyika pia Mjini Moshi.

2009 alihitimu kidato cha nne na kupata daraja la nne pointi 27, hivyo hakuweza kuendelea na kidato cha tano na sita na kuamua kujiendeleza kimazoezi zaidi, kwani alikuwa hana fedha za kujiendeleza kielimu.

“2010 nilijikita zaidi katika mazoezi na mwaka 2011 nikawa bingwa wa Taifa mita 5000 na 10000 nikiwakilisha Mkoa wa Mjini Magharibi Zanzibar , baada ya Arusha kunikataa licha ya kushika nafasi ya tatu katika mbio ya majaribio,” anasema.
Anasema mwaka 2011 aliumwa sana , lakini alishiriki hivyo hivyo michezo ya All African Games katika mbio za mita 10,000 ambako alichemka vibaya.

Mwaka 2012 mwishoni alikwenda Brazil na kushiriki mbio ya Brasilia Km 10 na kushika nafasi ya kumi.
Mwaka 2003 alishiriki mbio za Dar Rotary Km 21 na Rock City Km 21 ambazo zote alishinda akishika nafasi ya kwanza.

2014 alishiriki Gyongoy Half Marathon Korea Kusini na kushika nafasi ya pili kabla ya kwenda kambini Ethiopia akiwa na timu ya Taifa ya Tanzania kujiandaa na michezo ya Common Wealth, lakini bahati mbaya alirejea na maumivu.

2015 afya iliimarika na kuanza mazoezi kasha kushiriki Kilimanjaro Half Marathon na kushika nafasi ya nne na baadaye World Cross Country huko Gyuyang China akishika nafasi ya 49 Km 12.

Baada ya hapo alianza maandalizi ya kufuzu World Championship na Julai 5, 2015 alikimbia Marathon yake ya kwanza, Gold Coast Airport Australia na kushika nafasi ya 6 akitumia saa 2:12.01 na kufuzu.


Agosti 22, 2015 alishiriki World Championship Beijing China , Marathon na kutumia saa 2:16.57 nafasi ya 12.

Desemba mwaka jana alijiunga na kambi West Kilimanjaro na Machi 6, alishiriki Lake Biwa Marathon huko Japan kuweka muda wa saa 2:09.19 nafasi ya tatu, muda wake bora aliofuzu kwa Rio 2016.

 Katika mashindano ya Rio Brazil mwaka jana, alishika nafasi ya tano na hapo nyota yake ilizidi kung’ara aliposhika nafasi ya kwanza Mumbai Marathon kisha nafasi ya saba London Marathon na jana kunyakua Medali ya Shaba. Huyu ndiye Alphonce Felix Simba anayepeperusha vema bendera ya Tanzania kimataifa.

No comments:

Post a Comment

Pages