HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

November 29, 2014

SAKATA LA ESCROW BUNGENI MJINI DODOMA

 Mbunge wa Hai na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe akichangia mjadala wa sakata la Escrow mjini Dodoma. (Na Mpiga Picha Wetu)
 Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka akichangia mjadala wa sakata la Escrow mjini Dodoma. (Na Mpiga Picha Wetu)
Kangi Alphaxard Lugola, mbunge wa Mwibara mkoani Mara.
Wakazi wa jiji la Mbeya wakifuatilia michango ya wabunge kuhusu sakata la Escrow mjini  Dodoma. (Picha na Christopher Nyenyembe, Mbeya)
  
Muhongo, Werema ‘wavuliwa’ nguo
*Kamati ya Zitto yaanika uongo wao, mawaziri warukana
*Yadai Mwanasheria Tanesco amebambikwa kesi ya mauaji

Na Waandishi Wetu

KAMATI ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (PAC), imeanika uongo wa Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Fredrick Werema, ikionesha walivyotoa taarifa za uongo kuhalalisha uchotwaji wa fedha zaidi ya sh. bilioni 306 kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow zilizokuwa zimehifadhiwa katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Hatua hiyo ilitokana wa viongozi hao kutetea kwa nguvu zote kwamba fedha hizo zilikuwa za watu binafsi (makampuni mawili ya IPTL na Tanesco), na hivyo kupingana na ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na Taasisi ya Kuzui na Kupamabana na Rushwa (Takukuru) zilizothibitisha kwamba fedha hizo ni za Umma.

Katika kujibu hoja za wabunge, PAC kupitia kwa wasemaji wake Dk. Khamis Kigwangala, Luhanga Mpina, Deo Filikunjombe na mwenyekiti wake, Zitto Kabwe walisema kuwa viongozi hao waliingilia majukunu yasiyo yao na kutumia taarifa za uongo kutetea kampuni ya IPTL.

Walisema kuwa haijapata kutokea katika historia ya nchi kwa serikali kuwa na waziri kama Muhongo anayesema uongo kwa kiwango kikubwa kiasi hicho tena kwa kuurejea mara kwa mara ndani ya Bunge.

Walisema kuwa kutokana na uongo na upotoshaji wa viongozi hao, umeisababishia serikali hasara ya mabilioni kupitia kampuni hiyo, jambo linaloashiria kulikuwa na harufu ya rushwa katika suala hilo hasa ikizingatiwa uharaka uliyotumika kuhamisha fedha hiyo BoT licha ya tahadhari kubwa iliyowekwa na Gavana.

Zitto 

Katika kujenga hoja yake, Zitto alianza kwa kuwasifu wabunge wenzake wa kambi ya upinzani wa vyama vinavyounda kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), akisema waliweka tofauti zao kando na kuungana naye kutetea maslahi ya Taifa.

“Kwa muda sasa nimekuwa na mgogo na chama changu cha Chadema, lakini katika hili tumeweka tofauti kando, tumekaa pamoja na kujadili kama taifa. Kwa mara ya kwanza nimehudhuria kikao cha Ukawa...nimewamiss sana wenzangu,” alisema.

Zitto alianza kwa kuwaondoa shaka baadhi ya wabunge wa CCM waliombeza na kumbambika tuhuma za kuhongwa, akisema hawajui uadilifu na mchango wake kwa taifa.
Alisema kwamba fedha hiyo ya Escrow ilinyemerewa kuporwa tangu mwaka 2008 na 2009 wakati PAC ilipoleta hoja ya IPTL iondolewe chini ya mufilisi.

“Siwezi kuwajibu wote walioniparua maana hawajui nilichokifanya kwa nchi hii. Wakati fulani nikiwa bungeni alikuja Balozi wa Uingereza akiwa na ujumbe wake, akitaka kufanya ushawishi ili Benki ya Standard Chartered ilipwe fedha hizo, lakini niliwakatalia kwa sababu hawakuwa na kibali cha Waziri wa Sheria na Katiba wakati ule; mh. Chikawe unakumbuka...labda unikane,”alisema.

Zitto alifafanua kuwa inashangaza kuona waziri Muhonga amekuwa akihadaa Umma kwamba ghara za umeme zinapungua na hasara ya Tanesco inaendelea kupungua, huku akitoa takwimu za hasara iliyopatikana tangu waziri huyo aingie madarakani.

“Waziri Muhongo alipoingia alikuta Tanesco inapata hasara ya sh. bilioni 43 lakini mwaka mmoja tu 2012, Tanesco ilipata hasara ya sh. bilioni 117 na hadi kufikia Desemba mwaka 2013 hasara ni sh. bilioni 467,” alisema.

Zitto alisema kwa kuwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imekiri kuwepo kwa utakatishaji, ukwepaji kodi, nyaraka za kughushi zilizowasilishwa na Harbinder Singh Sethi, njia rahisi ni mtambo wa IPTL kutaifishwa na kumilikiwa na Serikali.

Kuhusu kauli ya Mwanasheria wa Tanesco, Godwin Ngwilimi ambaye waziri Muhongo alidai kuwa aliomba kuacha kazi mwenyewe baada ya kubaini kwamba alifanya makosa ya kwenda kuichunguza kampuni ya PAP nchini Malaysia bila idhini ya AG, Zitto alisema taarifa hizo sio za kweli.

Huku akionesha barua ya AG iliyomruhusu kufanya kazi hiyo, Zitto alisema kuwa mwanasheria huyo alishinikizwa na Bodi ya Tanesco kuandika barua kuacha kazi baada ya kuleta ushauri ambao haukutakiwa kwa sababu watuhumiwa tayari walikuwa wameishagawana fedha za Escrow.

“Kijana huyu alifanya kazi nzuri ya kizalendo kwa sababu alibaini kuwa Sethi ndiye PAP na Sethi ndiye IPTL, na sasa amefunguliwa kesi ya mauaji ili kushughulikiwa, serikali imlinde,” alisema Zitto na kuongeza kuwa;

Benki za nje kama Stanbic imekwishachukua hatua za kinidhamu kwa kuwafukuza kazi wakurugenzi wake waliohusika katika sakata hilo, kwamba hata serikali ya Tanzania kupitia BoT inatakiwa kuwaandikia barua Stanbic warejeshe fedhe hizo kwa sababu miamara hiyo ilifanyika kwa uzembe wao.

Zitto alihitimisha akiahidi kujipeleka kwenye Kamati ya Bunge ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge ili kuhojiwa kwa tuhuma za kuhusishwa kuhongwa fedha hizo za Escrow akisema ni uzushi unaopaswa kudhibitishwa.

“Mimi ni mwanasiasa na nina ngozi ngumu, wote mnajua miongoni mwa tuhuma zinamhusisha mama yangu mzazi ambaye ametangulia mbele ya haki, hivyo naomba mnishughulikie mimi, muacheni mama yagu apumzike,” alisema Zitto na kububujikwa na machozi. Chanzo cha Habari-Tanzania Daima, Novemba 29.

No comments:

Post a Comment

Pages