HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

May 05, 2015

Nyalandu awacharukia wahamiaji haramu

NA LOVENESS BERNARD, BIHARAMULO

WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, amewataka wahamiaji haramu waliovamia kwenye mapori ya akiba, kuondoka mara moja kabla hatua kali za kisheria hazijachukuliwa dhidi yao.

Pia amewaagiza askari wa wanyamapori nchini kukamata na kutaifisha mifugo yote ya wahamiaji haramu inayokamatwa kwenye mapori hayo ya akiba na fedha hizo zitumike kwenye ujenzi wa maabara na ununuzi wa madawati katika shule zilizopo jirani na mapori hayo.

Akizungumza na wafugaji pamoja na askari wa wanyamapori katika Wilaya ya Biharamulo mkoani Kagera, Waziri Nyalandu alisema, kumekuwa na wimbi kubwa la wahamiaji haramu kutoka nchi jirani za Rwanda, Kenya, Burundi na Uganda ambao wameingia na mifugo yao kwenye mapori ya akiba katika wilaya hiyo.

Alisema rasilimali zilizopo katika nchi hii ni mali ya Watanzania hivyo mgeni yeyote anayetaka kuingia na kufanya shughuli zake hapa nchini, ni lazima afuate sheria, taratibu na kanuni za nchi.
Amepiga marufuku kwa askari wa wanyamapori nchini kuwapiga risasi ng’ombe kwani kwa kufanya hivyo ni kuvunja sheria.

Alisema ni marufuku kwa askari wote kuwatesa raia wanapowakamata wakati  wakifanya shughuli za ujangili, ufugaji au uhalifu wa aina yoyote ndani ya hifadhi kwani nchi hii inaendeshwa kwa misingi ya sheria za haki za binadamu na utawala bora.

Amesisitiza kuwa, yeye kama waziri mwenye dhamana hatamvumilia askari yeyote atakayethubutu kuvunja sheria kwa makusudi ilhali akijua utaratibu anaopaswa kuchukua pindi anapomkamata mtuhumiwa.

Ameahidi kukutana na wafugaji wote nchini wanaotokea kwenye maeneo yenye migogoro na uhifadhi wakiwapo wabunge wao kwa lengo la kutafuta suluhu ya migogoro kati ya wahifadhi na wafugaji.

No comments:

Post a Comment

Pages