HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

April 25, 2016

Timu nne zatinga nusu fainali katika Mei Mosi

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

TIMU nne za soka zimeingia hatua ya nusu fainali kwenye mashindano ya Mei Mosi yanayoendelea kwenye atika uwanja wa Jamhuri mkoani hapa.

Timu hizo ni Tamisemi na Tanesco zilizotoka kundi A, wakati za kundi B ni Uchukuzi SC na Geita Gold Mine (GGM).

Nusu fainali hiyo itafanyika keshokutwa kwa kumshindanisha mshindi wa kwanza wa kundi A na mshindi wa pili wa kundi B kwa mechi ya saa 8:00 mchana na mechi ya saa 10:00 mshindi wa kundi B ataumana na mshindi wa pili wa kundi A.

Timu zilizoishia kwenye hatua ya makundi ni TPDC, CWT na UDOM za kundi A na za kundi B ni Ukaguzi, CDA na Mambo ya Ndani.

Kwa upande wa netiboli inayochezwa kwa mtindo wa ligi,  timu ya Tamisemi inaongoza kwa kuwa na pointi sita sawa na Uchukuzi SC, lakini wanamagoli mengi ya kufunga ambayo ni 76 wakati wenzao wanayo 54, wakifuatiwa na CDA yenye pointi tatu, huku Tanesco na TPDC wakiwa hawana kitu.

Katika michezo ya awali ya kuvuta kamba timu ya wanawake ya Uchukuzi SC ilipata ushindi wa chee dhidi ya UDOM, ambao hawakutokea uwanjani, pia Tanesco wanaume walipewa pointi baada ya CWT kushindwa kuonekana ulingoni, nayo TPDC wanawake waliwavuta Tamisemi kwa mivuto 2-0.

Katika mchezo wa bao wanawake Mayasa Kambi wa UDOM alitwaa ubingwa akifuatiwa na Thea Samjela wa Uchukuzi SC na mshindi wa tatu ni Catherine Likunguwa wa CDA; wakati kwa wanaume Omari Said wa Uchukuzi SC alitwaa ubingwa baada ya kumfunga Lameck Mboje wa Tamisemi katika mchezo wa fainali.

Nayo TPDC ilitoshana nguvu na Tanesco katika soka kwa kufungana bao 1-1. Tanesco ndio walikuwa wa kwanza kufunga bao katika dakika 25 na TPDC walisawazisha katika dakika za nyongeza.

Michuano hiyo itaendelea Jumanne (Aprili 26,2016) katika soka kwa Uchukuzi SC kuwakaribisha CDA Dodoma asubuhi na jioni Ukaguzi watacheza na Mambo ya Ndani.
 Kikosi cha Tamisemi kilichoingia nusu fainali katika michezo ya Mei Mosi.
 Kiungo wa Ukaguzi, Mansour Juma (17) akikokota mpira mbele ya Seleman Kaitaba wa Uchukuzi SC katika mchezo wa soka katika mashindano ya Mei Mosi yanayoendelea kwenye uwanja wa Jamhuri Dodoma. Uchukuzi SC walishinda 3-1. 
 Kipa wa GGM Emmanuel Charles  (mwenye jezi nyeusi) akijiandaa kudaka mpira wa kona uliochongwa na Omar Said ‘Chidi’ wa Uchukuzi (hayupo pichani). Timu hizo zilitoka sare ya bao 1-1.
   Kikosi cha Uchukuzi SC kilichotinga nusu fainali kwenye michezo ya nusu fainali.

No comments:

Post a Comment

Pages