HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 22, 2016

Watumia dawa za kulevya Z’bar waonywa

Na Talib Ussi, Zanzibar

KAIMU Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Zanzibar, Dk. Mahmoud Ibrahim Mussa, amesema matumizi ya dawa hizo ni janga linaloathiri vijana na kupoteza mwelekeo ambao husababisha kufanya uamuzi usio sahihi na kuzitaka taasisi husika na wazee kushirikiana kuondoa tatizo hilo.

Mussa aliyasema hayo  katika shamrashamra za mafunzo ya watendaji wa Chuo cha Mafunzo Zanzibar,  ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha Siku ya Kudhibiti Madawa ya Kulevya Duniani.

“Mtumiaji  wa dawa za kulevya huathirika ubongo, hivyo hawezi kuacha kutumia dawa hizo ili kuongeza kiwango, hali inayosababisha kutoweza kufanya kazi yoyote yenye kuleta manufaa kwake wala kwa taifa,” alieleza Dk. Mussa.

Alisema kuwa matumizi ya dawa hizo yanakuwa ni chanzo kikuu cha maambukizi makubwa ya virusi vya ukimwi, hasa kwa watumiaji wa njia ya kujidunga sindano, hivyo kusababisha jamii kupoteza nguvu ya taifa.

Dk. Mahamoud alitanabaisha kuwa kinga ya msingi ya kuachana na matumizi ya dawa za kulevya imo ndani ya familia ambayo inatakiwa kumkubali muathirika ili aweze kuachana na kilevi hicho, kwa kumpa huduma nzuri bila ya kumnyanyapaa.

Aidha, ameshauri kutafuta njia ya kudhibiti utumiaji wa dawa za kulevya katika vyuo vya mafunzo kwa wafungwa, kwani imebainika kuwa baadhi yao hutumia dawa hizo wakati wakitumikia vifungo vyao.  
  
Nao washiriki wa mafunzo hayo wameiomba jamii kutoa ushirikiano mkubwa kwa vyombo vya kudhibiti dawa za kulevya ili kuweza kuwafichua na kuwadhibiti wale wote wanaoingiza, wanaosambaza, watumiaji, pamoja na kutoa elimu hiyo kupitia skuli mbalimbali ili kuhakikisha jambo hilo linadhibitiwa nchini.

No comments:

Post a Comment

Pages