HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

October 14, 2017

RC TABORA : WAKURUGENZI NENDENI MKATOE ELIMU YA UFUGAJI WA KISASA WA WAFUGAJI

Na Tiganya Vincent, RS –TABORA 

SERIKALI ya Mkoa wa Tabora imeziagiza Halmashauri zote zenye wafugaji wa ng’ombe  kuandaa mipango ya kuwahamasisha wafugaji juu ya ufugaji bora kwa kuwa na mifugo michache ambayo inahudumiwa vizuri na inakuwa na tija.

Kauli hiyo imetolewa jana na Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri wakati wa mkutano uliwahusisha Wakuu wa Wilaya , Wakurugenzi Watendaji  , Wakuu wa Idara na Seketarieti ya Mkoa wa Tabora.

Alisema kuwa wakati umefikiwa wa kuwasaidia wafugaji kuwa na ng’ombe wa kisasa ambao wanazalisha nyama na maziwa ya kutosha kinyume na walivyo ng’ombe wa sasa hivi ambao uzalisha wastani wa kilo 150 hadi 200 kama ni mkubwa.

Mwanri alisema kuwa ufugaji huo wa kizamani hauwezi kumsaidia mfugaji kusonga mbele bali utamfanya aendelee kuwa na mawazo ya kudhani kuwa na ng’ombe wengi wasio na uzito ni utajiri.
“Natarajia Wakurugenzi Watendaji hasa wa maeneo yenye mifugo mingi kama vile Nzega na Igunga mwende mkawaelimishe wafugaji juu ya ufugaji bora na wa kisasa unaweza kuwasaidia kuongeza uzito wa ng’ombe na wingi wa maziwa…wakati sisi ng’ombe wetu wanauzito wa kilo 150 wenzetu Botswana ng’ombe anafika hadi kilo 1,000” alisema Mkuu huyo Mkoa.

Alisema kuwa sanjari na hilo ni vema idadi ya ng’ombe katika maeneo yao ikajulikana ikiwa ni pamoja na kujua hao wanapata wapi malisho na wawekewe alama kwa ajili ya kutenga maeneo kwa ajili ya malisho ya wanyama hao.

Mwanri alisema kuwa kutokuwa na mipango mizuri ndio maana unakuta ng’ombe wamerundikana sehemu moja huku wakiwa hawana hata majani ya kula mwishowe wanakufa kwa sababu ya njaa na kukosa maji.

Alisema kuwa kuanzia sasa kila Halmashauri lazima impe na mikakati yake ya kusimamia sekta ya mifugo kwa ajili ya kuhakikisha kuwa wafugaji wananufaika na mifugo yao na kutoa mchango katika ujenzi wa uchumi wa viwanda ambao nchi imeazimia kuujenga.

No comments:

Post a Comment

Pages