HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

February 10, 2019

Tamasha la Pasaka Dar ndani ya Viwanja vya Kijitonyama

Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Tamasha la Pasaka, Alex Msama , akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, kuhusu maandalizi ya tamasha hilo.
Baadhi ya waandishi wa habari.

 

Na Mwandishi Wetu

WAKATI  wadau na wapenzi wa muziki wa injili jijini Dar es Salaam wakisubiri kwa hamu kuona ni sura zipi za waimbaji watakuwemo katika Tamasha la Pasaka la mwaka huu, Kamati ya Maandalizi imetangaza Uwanja utakaotumiwa siku hiyo.

Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Tamasha hilo, Alex Msama alisema kwamba kwa jiji la Dar es Salaam, uhondo wa tukio hilo la kimataifa utafanyika katika Uwanja wa Kijitonyama TCCL Posta, wilayani Kinondoni.

Msama alisema kuwa, hadi sasa maandalizi yamezidi kushika kasi kwani tayari wameshakamilisha mazungumzo na mmoja wa waimbaji mahiri wa kimataifa ambaye kwa umaarufu wake, ndiye atabeba uzito wa tukio hilo la mwaka huu.

“Tunashukuru Mungu, maandalizi yanakwenda vizuri sana kwani hadi sasa tumeshakamilisha mazungumzo na mwimbaji mmoja wa kimataifa ambaye ndiye atabeba uzito wenyewe wa tamasha la mwaka huu,” alisema Msama.

Alisema jina la mwimbaji huyo litawekwa bayana baadaye, lakini akidokeza kuwa ni mwimbaji mahiri ambaye kila mdau wa nyimbo za injili, atamkubali kutokana na uwezo na kipaji chake.

Kuhusu Uwanja wa Kijitonyama, Msama alisema kuwa Kamati yake imefanya utafiti wa kina kabla ya kufikia uamuzi huo, ikiwemo ukubwa wa eneo, usalama pamoja na wepesi wausafiri wa kwenda na kurudi.

“Tumetafakari sana ni uwanja gani unafaa kwa ajili ya kufanyia tukio hili la kimataifa. Tukaona ni Viwanja vya Kijitonyama kwa sababu ni rahisi kufika na usalama wake kwa watu na mali zao ni mkubwa mno,” alisema Msama.
Msama alisema baada ya tukio hilo kutumbuiza wapenzi na mashabiki wa muziki wa injili wa Dar es Salaam,  litahamia katika mingine 10, likianzia jijini Dodoma, Singida, Simiyu na Mwanza.

Alisema mikoa mingine zaidi itakayofikiwa na Tamasha hilo, itajulikana baadaye kwa kadiri maandalizi yanavyoendelea kwani lengo ni kuhakikisha uhondo huo unafika mikoa mingi zaidi ili ujumbe wa Neno la Mungu uweze kuwafikia wengi.

Alisema mbali ya tamasha hilo kutumika kwa ajili ya kufikisha ujumbe wa neno la Mungu kwa njia ya kuburudisha, pia sehemu ya mapato hutumika kufariji wenye mahitaji maalumu kama walemavu, wajane na yatima katika jamii.

Msama alisema kwa mwaka huu, Tamasha hilo ambalo linahimiza umuhimu wa hali ya amani na upendo katika taifa, linaangaza juhudi za serikali katika miradi ya maendeleo iliyofanyika na inayoendelea kufanyika kwa kasi kote nchini.  

Alisema Tamasha hilo limejitosa kuhimiza amani na upendo katika taifa kwa kutambua, vitu hivyo viwili ndio msingi wa watu na taifa kupiga hatua katika nyanja zote za kiuchumi, kijamii na kisiasa. 

Msama kwa mutambua hiyo, ndio maana anawasihi wadau na wapenzi wa muziki wa injili, kukaa mkao wa kupokea uhondo wa Tamasha hilo ambalo litabeba uzito mkubwa wa waimbaji mahiri wa kutoka ndani na nje ya nchi.

No comments:

Post a Comment

Pages