HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

May 05, 2019

Kikwete: Ukweli kifo cha Mengi anaujua mwanae, kakaake

Dk. Reginald Mengi akiwa na mkewe Jack enzi wa uhai wake.

Rais mstaafu wa Awamu ya Nne, Dk. Jakaya Kikwete, amesema kuwa ukweli kuhusu kifo cha Mwenyekiti Mtendaji wa Makampuni ya IPP, Dk. Reginald Mengi, anaujua mtoto wake Regina na mdogo wake Benjamin Mengi, ambao wako Dubai.

Kikwete ambaye alikuwa miongoni mwa Viongozi waliofika nyumbani kwa marehemu Dk. Mengi kutoa pole, alisema watu waache uongo na kuongea mambo yasiyokuwepo kuhusiana kifo cha bilionea huyo. 

Tangu kilipotokea kifo cha Dk. Mengi, kumekuwa na maneno na taarifa nyingi mtandaoni, zikieleza taarifa tofauti ambazo nyingi zinadaiwa kuwa ni za uongo na uchonganishi.

Kikwete ametoa kauli hiyo jana  wakati akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya kusaini kitabu cha maombolezo nyumbani kwa Dk. Mengi Kinondoni, jijini Dar es Salaam.

Alisema kama kweli watu walikuwa wanampenda Dk. Mengi, basi mambo ya uongo na ya kutunga wanapaswa kuyaacha na kusubiria watu waliopo Dubai wanaoshughulikia kurejesha mwili wa marehemu, kutoa taarifa sahihi juu ya kifo hicho ambacho kimetikisa nchi. 

"Tunajua Dk. Mengi amefariki dunia akiwa Dubai ila Benjamini ambaye ni mdogo wa marehemu yupo huko na binti yao Regina Mengi, yupo pia kwa hiyo hao ndio wenye ukweli hivyo wakirudi watatuambia nini hasa kilitokea na ilikuaje, ombi langu ni hilo na haya maneno yangu sasa msije mkayachanganya, " alisema.

Kikwete alisema kuendelea kwa maneno hayo ya uongo kutasababisha kuichanganya jamii hivyo watu wanapaswa kuacha kuyasema mambo hayo na kuwa wavumilivu mpaka wale waliopo Dubai watakaporudi nchini na kutoa taarifa sahihi.
 
 Hata hivyo alisema kuwa kifo cha Dk. Mengi kimestua wengi na ni pigo kubwa kwa Taifa  lakini hawezi kuacha kuukubali ukweli kwamba kila nafsi itaonja umauti. 

Alisema  Taifa limepoteza raia makini, mchapakazi na mzalendo hivyo  watamkumbuka Dk. Mengi kwani amechangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya nchi hii kwa kuwasaidia watu mbalimbali wakiwemo maskini na walemavu. 

"Najua tulitamani sana kama Taifa kuwa naye lakini ndo hivyo Mwenyezi Mungu amempenda zaidi na ameshapitisha uamuzi wake hata hivyo  tuelewe kuwa kwa sababu yoyote na kwa mazingira  yoyote ile kila mtu ataondoka hapa duniani, nawatakia moyo wa subra ndugu jamaa na marafiki," alisema Mzee Kikwete. 

Alisema kabla ya umauti kumkuta, alizungumza na kusalimiana naye kwa sababu alikuwa kama kaka yake na kuongeza kuwa walikubaliana naye kwamba akirudi safari nchini Benin, watakutana na kuzungumza.

Alisema Dk. Mengi amefanya mengi na hivyo ni muhimu yale aliyoyafanya hapa duniani yadumushwe na yaendelee kufanyika na kuongeza kuwa watu waendelee kuwa watulivu katika kipindi hiki.

Aidha alisema watamkumbuka marehemu Mengi kwani alikuwa mtu mwenye huruma na moyo wa kusaidia watu mbalimbali na ametumia utajiri wake kuwasaidia Watanzania wengi.

IGP Sirro. 

Naye Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP) Simon Sirro alisema kuwa wameona kinachoendelea katika mitandao ya kijamii na tayari  wameshafungua dokezo na wameshaanza kufuatilia  taarifa zinazotolewa na watu mbalimbali katika mitandao hiyo kuhusu kifo cha Dk. Mengi.

"Tumeona na tunafuatilia taarifa mbalimbali zinazotolewa katika mitandao ya kijamii kuhusu kifo cha Mzee Mengi  hatuzipuuzii ila kwa sasa kazi ni kuhakikisha msiba unamalizika kwa amani na utulivu, "alisema Sirro.

Alisema  Jeshi la Polisi limejipanga kuimarisha ulinzi siku ya kutoa heshima za mwisho ambayo anaamini kutakuwa na waombelezaji wengi  ili watu wenye nia ovu wasipate nafasi ya kuharibu zoezi hilo.

Alisema kifo cha Dk. Mengi ni pigo kubwa kwa Jeshi hilo  kwani alikuwa mdau muhimu na alilipenda Jeshi tofauti na wafanyabiashara wengine.

"Mengi ni mtu aliyekuwa na fedha lakini alikuwa tofauti na matajiri wengine hakika Jeshi letu limepoteza mdau mkubwa sana kwa sababu alilipenda Jeshi na alikuwa mzalendo na tofauti na wafanyabiashara wengine ambao wanaliona Jeshi adui kutokana na mambo wanayoyafanya ikiwemo kuvunja Sheria," alisema Sirro. Chanzo Gazeti la Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment

Pages