HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

August 10, 2019

Mbomole kumlinda Kolokolo Domorefu

 Meneja Mradi wa Nature Tanzania, Victor Mkongewa, akizungumzia mradi huo mbele ya viongozi wa Kijiji cha Mbomole. (Picha na Suleiman Msuya).
 Mkurugenzi Msaidizi wa Shirikia la Kuhifadhi Misitu Asili Tanzania (TFCG), Emmanuel Lyimo (kushoto), akimkabidhi bango lenye ujumbe wa uhifadhi wa misitu kwa Mjumbe wa Serikali ya Kijiji cha Mbomole wilayani Muheza, Rashid Omari, mkoani Tanga.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Mbomole, wilayani Muheza, mkoani Tanga, Athuman Singano, akitoa maelezo kuhusu faida za mradi huo kijijini kwake. 

NA SULEIMA MSUYA, ALIYEKUWA MUHEZA


VIONGOZI na wananchi wa Kijiji cha Mbomole, Kata ya Mbomole wilayani Muheza mkoani Tanga wameahidi kumlinda ndege aina ya Kolokolo Domorefu anayepatikana katika Hifadhi ya Mazingira Asili ya Amani pekee.
Kauli hiyo viongozi na wanakijiji kuahidi kumlinda ndege huyo ambaye anatajwa kuwa katika kundi la viumbe hai adimu duninia inakuja baada ya kupatiwa elimu na Shirika la Nature Tanzania kuhusu umuhimu wa ndege huyo kiuchumi na mazingira.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Mbomole, Athuman Singano, alisema mwaka jana Nature Tanzania iliwaletewa Mradi wa Uhifadhi Endelevu wa Usimamizi Misitu kwa Uhifadhi wa Ndege Kolokolo Domorefu katika Milima ya Usambara Mashariki ambapo umekuwa na matokeo chanya.
Singano alisema wanakijiji wameupokea kwa mikono miwili ambapo wanashiriki kutunza msitu huo wa aina yake nchini Tanzania huku wakiwekeza katika kilimo msitu kisichoharibu mazingira.
“Kolokolo Domorefu ameweza kutukomboa sisi kama wananchi lakini kijiji kimeweza kupata zaidi ya shilingi 910,000 kwa ajili ya kumalizia ofisi ya kijiji lakini pia tumenufaika kwa mafunzo kutoka Nature Tanzania wakishirikiana na Shirika la Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG),”alisema.
Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Mbomole, Emmanuel Mageta alisema mradi huo wa Nature Tanzania umesababisha wananchi wote wawe sehemu ya ulinzi wa misitu na mazingira.
“Wapo wananchi wamewezeshwa kiuchumi katika miradi ya ng’ombe, nguruwe na miche ya mbegu za mazao ya viungo hivyo matarajio yetu ni siku chache zijazo Mbomole itainuka kiuchumi,” alisema.
Mnufaika wa mradi huo Jomo Simon alisema baada ya kuwezeshwa ameanza kuona matarajio yake ya baadae kimaisha na kuwaomba wananchi wengine kushiriki katika mradi huo.
Simon alisema anajishughulisha na kilimo cha viungo vya iliki, pilipili manga, karafuu ambapo mwishoni mwa mwaka huu ataanza kuvuna,
Kwa upande wake kijana wa miaka 15 Halifa Jumaa alisema mradi huo umemjengea uelewa wa kulinda viumbe hai akiwemo ndege Kolokolo Domorefu na kuwataka vijana wenzake kumlinda ili aweze kuchochea uchumi wa kijiji chao.
Meneja Mradi wa Nature Tanzania, Victor  Mkongewa alisema mradi huo wa kumlinda Kokoloko Domorefu unafadhiliwa na Mfuko wa Kuhifadhi Viumbe Adimu Duniani (CPEF), umejikita kuhakikisha ndege huyo anaendelea kuwepo nchini.
Alisema Kolokolo Domorefu ni ndege adimu ambaye anavutia watalii lakini pia ni ishara tosha kuwa mazingira yapo salama.
“Kolokolo Domorefu hawazidi 249 duniani kote hivyo katika kuhakikisha anaendelea kuwepo tumeamua kuiwashirikisha wananchi wa Mbomole na Shebomeza ambavyo vipo kandokando ya Hifadhi ya Amani na mwitikio ni mzuri,” alisema.

No comments:

Post a Comment

Pages