HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

October 03, 2019

DPP AWAONYA MAWAKILI WANAOCHUKUA FEDHA ZA WATUHUMIWA WALIOKIRI MAKOSA KATIKA KESI ZA UHUJUMU UCHUMI

Mkurugenzi wa Mashtaka Nchini (DPP), Mganga Biswalo, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu
MKURUGENZI wa Mashtaka Nchini (DPP), Biswalo Mganga, amestushwa baada ya kubaini kuwapo kwa baadhi ya mawakili wanaokwenda gerezani na kuchukua fedha kwa washtakiwa wanaokabiliwa na kesi za uhujumu uchumi kwa kusema kuwa wanakwenda kuwalipia katika ofisi yake jambo ambalo amesema si kweli. 

Mganga amesema mawakili hao wanatafuta ugomvi na Ofisin yake na wasije wakamlaumu  kwani ni miongoni mwa watu wanaotumika kukwamisha mchakato wa msamaha uliyotolewa na Rais John Magufuli hivi karibuni kwa washtakiwa hao. 

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, DPP Mganga alisema tayari ameshaanza kufanya uchunguzi ili kuwabaini mawakili wanaofanya kazi hiyo ya utapeli. 

"Leo (jana) nimepata taarifa juu ya uwepo wa baadhi ya mawakili wanaochukua fedha kutoka kwa washtakiwa na kusema wanazileta kwa DPP, naomba niwakanye na niwaonye wanaofanya hivyo maana wanatafuta ugomvi,  tusije kulaumiana kwani nimeshaanza kufanya uchunguzi,  niwasihi wafanye shughuli zao za uwakili na kuheshimu ofisi ya DPP," alisema Mganga. 

Alisema utaratibu wa mshtakiwa kukiri upo pale pale na kusisitiza kuwa watu hao wanapaswa kufuata taratibu za kisheria za mahakama.

Aidha Mganga alisema taratibu za kulipa fedha  zipo mahakamani na sio wakili ama mtu yoyote kutoka na kwenda gerezani au kumfuata ndugu wa washtakiwa na kuwaambia awapatie fedha.

“Huo utaratibu haupo katika mchakato kama huu, naona  kuna wajanja wajanja wanajitokeza wanaotaka kufanya uhalifu katika zoezi hili wajiandae tutapambana nao wala hatutawavumilia,” alisema DPP Mganga

Hata hivyo,  Mganga alisema Serikali imeamua kufungua akaunti maalumu  Benki Kuu ya Tanzania (BoT)  kwa lengo la kuwawezesha washtakiwa wanaoandika barua za kukiri makosa hayo ya uhujumu uchumi na kuamriwa kurudisha fedha kulipia kwenye akaunti hiyo.

"Hii sio akaunti ya mahakama ni akaunti maalumu imefunguliwa BoT kwa amri ya serikali viongozi wakuu wa mahakama watajulishwa, hivyo hakuna fedha itakayolipwa katika akaunti ya mahakama, kwa DPP ama Mamlaka ya Mapato Nchini (TRA),” alisema Mganga.

Mganga alisema ambaye atalipa sehemu nyingine wasilaumiane kwani lazima fedha hizo ziende zinapotakiwa na kusisitiza kuwa si mawakili wa Serikali, watumishi wa ofisi ya DPP au mtu yeyote atakayefanya vitendo vya rushwa watakayemvumilia. 

“Ninasema hivi  sisi hatutamvumilia mla rushwa kama wakili wa kujitegemea ni mzuri sana mahakamani unakula rushwa hatutakuvumilia ama wakili wa serikali ni mzuri sana mahakamani unawasilisha hoja unakula rushwa hatutakuvumilia,” alisema Mganga

 Hata hivyo Mganga alisema watu wote wanaofanya uhalifu katika kipindi hiki cha washtakiwa walioambiwa kuomba msamaha kwa kuwaibia fedha zao kupitia ndugu au washtakiwa wenyewe waache.

Septemba 30, mwaka huu,  Rais Magufuli aliongeza muda mwingine wa siku saba kwa watuhumiwa wa kesi za uhujumu uchumi na kuwataka wote waliogoma kufuata masharti hayo, vinginevyo hatatoa muda zaidi baada ya siku hizo alizoongeza kumalizika. 

Rais Magufuli alitoa onyo hilo Ikulu jijini Dar es Salaam mara baada ya kupokea taarifa ya DPP Mganga kuhusu agizo alilotoa la kutaka watuhumiwa wa uhujumu uchumi kukiri makosa, kuomba radhi na kukubali kurudisha fedha ili waachiwe huru. 

Septemba 22 mwaka huu Ikulu jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya kuwaapisha viongozi mbalimbali aliowateua hivi karibuni wakiwemo mabalozi, makatibu wakuu na makatibu tawala wa mikoa, Rais Magufuli alimshauri DPP kuangalia uwezekano wa kuwaachia huru washtakiwa baada ya kukiri makosa na kukubali kurudisha fedha wanazodaiwa kukwapua. 

DPP  alisema ofisi yake imepokea barua 467 za watuhumiwa wa kesi za uhujumu uchumi waliokuwa tayari kukiri na kurudisha fedha walizowaibia watanzania. 

Alisema barua hizo ziliendelea kufika ofisini kwake hadi Jumamosi (Septemba 28,2019) na Jumapili (Septemba 29,2019) kwa sababu zingine zilichelewa kufika kutoka mikoani. 

Alisema kati ya washtakiwa hao kundi la kwanza lipo tayari kurudisha Sh. Bilioni 7.8 muda wowote kuanzia Septemba 30, mwaka huu, huku washtakiwa wengine ambao kesi zao zipo kwenye mfumo wa dola za Marekani nao wapo tayari kurudisha dola zaidi ya Milioni mbili ambazo ni sawa na Sh. Billioni 5.7 za kitanzania. 

Alisema kundi lingine la pili lipo tayari kulipa kwa awamu ambao wataweza kulipa Sh. Bilioni 94.2 na kuongeza kundi hilo lipo tayari kurudisha  fedha hizo kwa awamu kadri watakavyokubaliana nao kwa mujibu wa taratibu za kisheria. 

Aidha alisema kundi la tatu ni la watuhumiwa wengine wa kesi hizo ambao wapo tayari kulipa moja kwa moja bila kulipa kwa awamu ambapo fedha wanazoweza kulipa ni kiasi cha Sh. Bilioni 13.6.

Alisema jumla ya fedha zote za washitakiwa 467 wenye kesi hizo za uhujumu uchumi ambao wapo tayari kurudisha ni Sh. Bilioni 107.8 ambazo watazirudisha serikalini kwa utaratibu watakaokubaliana nao.

No comments:

Post a Comment

Pages