HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

October 03, 2019

WANARIADHA WA TANZANIA WATUA SALAMA DOHA

Wanariadha wa Tanzania, kutoka kulia Agustino Sulle, Stephano Huche na Alphonce Simbu, wakimsikiliza Kocha wao, Andrew Panga, mara baada ya kuwasili leo Doha, Qatar kwenye mashindano ya Dunia.


Na Mwandishi Wetu

NYOTA watatu wa Riadha Tanzania wakiongozwa na Alphonce Simbu wamewasili salama jijini Doha, Qatar tayari kwa kinyang’anyiro cha mashindano ya Dunia ‘IAAF World Championships’.
Msafara huo wa Tanzania ukiwa na Nahodha Simbu kutoka Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Agustino Sulle wa klabu ya Talent na Stephano Huche wa African Ambassador Athletics Club (AAAC), chini ya Kocha Andrew Panga, uliwasili majira ya saa nane usiku wa kuamkia leo Oktoba 3 na kupokelewa na Katibu Mkuu wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), Wilhelm Gidabuday.
Gidabuday, alisema vijana wako salama na baada ya kuwasili walipumzika na jana asubuhi walikwenda kupasha misuli na kujionea hali ya hewa. “Vijana wote wako na hali nzuri, hawana wasiwasi kwani tayari Failuna alishawafanyia utafiti na wanajua namna ya kukabiliana na hali ya joto iliyoko huku,” alisema Gidabuday.
Naye Nahodha Simbu alisema kwa ufupi; “Tunashukuru Mungu tumefika salama, tumeishaona hali ilivyo na tupo tayari kwa kazi iliyotuleta hapa. Watanzania watuombe,”.
Kwa upande wake, Kocha Panga ambaye pia ni Kocha wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), alisema wachezaji wako salama na wana ari ya kufanya vema, tayari wameishapata vitendea kazi vyote na wapo tayari kulipigania Taifa.
Tanzania, ilianza vibaya mashindano hayo usiku wa kuamkia Septemba 28 katika mbio za Marathon Wanawake, pale Failuna Matanga aliposhindwa kumaliza mbio hizo na kuishia Kilomita 21.
 Sasa kete za mwisho zimebaki kwa Wanariadha hao watatu, ambao watachuana katika Marathon Kilomita 42.195 hapo Oktoba 5, huku Simbu akiwa anatetea medali yake ya Shaba aliyoitwaa katika mashindano yaliyopita huko London, Uingereza.

No comments:

Post a Comment

Pages