HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

April 01, 2020

ENDELEENI KUTOA ELIMU YA UGONJWA WA CORONA KWA WANANCHI - DKT.NDUGULILE

Eneo lililotengwa kwa ajili ya kuwatenga washukiwa wa ugonjwa wa Corona lililopo karibu na chuo cha Udom, Jijini Dodoma.


Na Rayson Mwaisemba, WAMJW-DOM

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile amewaasa Wataalamu wa Sekta ya Afya kuendelea kutoa Elimu kwa Wananchi kuhusu maambukizi ya ugonjwa wa Corona.

Ameyasema hayo leo wakati wa ziara yake ya kukagua hali ya utayari wa kupambana dhidi ya maambukizi ya ugonjwa wa Corona endapo utaingia Jijini Dodoma katika maeneo yote yaliyopangwa.

“Elimu bado haitoshi, kila siku ni lazima tuhakikishe tunatoa elimu kwenye jamii ili watu waweze kuelewa, watu waelewe ugonjwa huu maana yake ni nini, na kwanini tunasisitiza watu wanawe mikono, kwanini tunasisitiza maji tiririka na sabuni” alisema.

Amesema kuwa, ni muhimu kwa Wataalamu wa Sekta ya Afya kutoa Elimu ya kutosha kwa Wananchi, huku akisisitiza kuwa si kweli kwamba matumizi ya vitakasa mikono (sanitaizer) ni bora zaidi kuliko maji tiririka na sabuni.

“Si kweli kwamba Vitakasa mikono (Sanitaizer) ni bora zaidi kuliko kutumia maji tiririka na sabuni, tunahitaji tuwatoe hofu wanancni juu ya matumizi ya njia hizi mbili katika kujikinga dhidi ya ugonjwa huu.” Alisema.

Aliendelea kusisitiza kuwa, Wataalamu wa Sekta ya Afya kuongeza ubunifu katika kutoa elimu ili kuepuka upotoshaji unaofanywa na baadhi ya watu katika jamii juu ya kutibu maambukizi ya virusi vya ugonjwa wa Corona.

Aidha, Dkt. Ndugulile amewaagiza Wataalamu wa Sekta ya Afya kutumia njia nyepesi zaidi katika kutoa elimu ya ugonjwa wa Corona ili maambukizi haya yaweze kueleweka zaidi kwa Wananchi.

Mbali na hayo, Dkt. Ndugulile amesema kuwa, Serikali inaendelea kuleta mahitaji ya vifaa vyote vinavyohitajika katika maeneo yaliyotengwa kwa wagonjwa wa maambukizi ya virusi vya Corona endapo watatokea Jijini Dodoma.

“Niwahakikishieni vifaa vyote tutavileta, lakini pia niendelee kuwaomba tuwe imara muda wote, msisubiri ili kuweza kupambana na ugonjwa huu inabidi kuwa mbele muda wote” alisema.

Nae Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Best Magoma ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kuendelea kuboresha maeneo ya utayari na kuweka msisitizo katika maeneo yote ya muhimu ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kudhibiti maambukizi ya ugonjwa wa Corona endapo utatokea.

“Tunashukuru Wizara ya Afya na Ofisi ya Rais TAMISEMI, kwa kutuunga mkono, wamekuwa karibu na sisi katika kutupa maelekezo na muelekeo wa nini chakufanya katika kuboresha Sekta ya Afya”alisema.

Dkt. Best Magoma, aliendelea kusema kuwa, katika ngazi ya Mkoa wataendelea kuboresha maeneo yote ambayo Wizara ya Afya kupitia Naibu Waziri Dkt. Faustine Ndugulile ameelekeza katika zaira hiyo.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, wazee na Watoto Dkt. Faustine ndugulile amefanya ziara katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma, Kituo cha Afya Mkonze na makazi ya chuo cha Dodoma, kukagua hali ya utayari wa kupambana dhidi ya maambukizi ya ugonjwa wa Corona endapo utaingia.

No comments:

Post a Comment

Pages