HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

July 06, 2020

USMJ, FBE zinavyochochea uhifadhi misitu vijijini

>Viongozi, wanavijiji wasema ni sawa na kumpa mchawi akulelee mtoto 
Ofisa Maliasili wa Wilaya ya Kilosa, John Mtimbanjayo akieleza kwa waandishi wa habari pichani hawapo namna vijiji vya wilaya hiyo vilivyonufaika na mfumo wa USMJ na FBE.

Darasa la Shule ya Msingi Ulaya Mbuyuni wilayani Kilosa mkoani Morogoro lililojengwa kwa fedha za USMJ na FBE. 
Tanki la maji lililopo Shule ya Msingi Ulaya Mbuyuni wilayani Kilosa mkoani Morogoro lililojengwa kwa fedha za USMJ na FBE. 
 

Na Suleiman Msuya


UPO msemo wa Kiswahili unasema ‘Mchawi mpe mtoto akulelee’. Msemo huo una maana nyingi na kubwa katika jamii hasa ukilenga iwapo kuna mtu ambaye una wasiwasi naye katika maisha unapaswa kumpa jukumu ili kumpima.

Hali hiyo inatokea kuanzia ngazi ya familia, jamii na nchi kwa ujumla ambapo unapotaka kubaini jambo fulani unaambiwa unaweza kutumia njia hiyo.

Pamoja na dhana hiyo lakini imekuwa ngumu kutekelezeka katika jamii kwani hasa pale inapobainika kuwa kuna mazingira ya kishirikina kuwa anayehusishwa na jambo hilo apewe aliyelogwa akae naye.

Hili limeweza kutokea katika kutekeleza dhana ya Usimamizi Shirikishi wa Misitu ya Jamii (USMJ) na Biashara ya Mazao ya Misitu (FBE) ambapo wadau mbalimbali kwa kushiriana na Serikali wamefanikiwa kuwapa wanavijiji mamlaka ya kulea mtoto misitu kwa wao kunufaika nao kijamii, kiuchumi na maendeleo.

Wilaya ya Kilosa, mkoani Morogoro ni moja ya wilaya ambayo asilimia 80 ya eneo lake liligubikwa na migogoro ya wakulima na wafugaji huku uharibifu wa misitu hasa ya vijiji na ile ya Serikali ukiota mizizi.

Hali hiyo iliibua masharika kama Shirika la Kuhifadhi Misitu Tanzania (TFCG), Mtandao wa Jamii wa Usimamizi wa Misitu Tanzania (MJUMITA), Shirika la Kuendeleza Nishati Tanzania (TaTEDO) chini ya ufadhili wa Shirika la Maendeleo Uswiss (SDC) na kuhakikisha wanavijiji wanaomiliki misitu ya vijiji wanakuwa wanakuwa wachawi kwa kuwakabidhi kuilinda, kuisimamia na kuitumia kwa njia endelevu.

Mchango wa mashirika hayo pamoja na Serikali umeweza kubadilisha maisha ya wananchi wa vijiji takribani 20 ambavyo vinatekeleza Mradi wa Kuleta Mageuzi katika Sekta ya Mkaa Tanzania (TTCS).

DAS KILOSA

Katibu Tawala wa Wilaya ya Kilosa (DAS), Yohana Kasitila anaelezea kwa kina namna wilaya na wananchi wa vijiji vilivyopo kwenye mradi wameweza kunufaika na dhana ya USMJ na FBE hasa ikizingatiwa na historia ya huko nyuma.

Kastila anasema awali misitu yote ilikuwa inaharibiwa na wananchi wenyewe ila ujio wa TFCG na MJUMITA kupitia TTCS kuna manufaa makubwa ya kimazingira, kiuchumi, huduma za kijamii na maisha ya mwananchi mmoja mmoja.

“Katika vijiji vile ambavyo mradi umepita kuna manufaa makubwa sana kwani miradi mingi ya kiujasiriamali imebuniwa na inaendelea kubadilisha maisha ya wananchi wenyewe.

Kila mwananchi katika kijiji chenye mradi amekuwa mhifadhi na mtoa taarifa pale ambapo anaona kuna uharibifu jambo ambalo awali halikuwepo,” anasema.

DAS Kastila anasema kinachofanyika Kilosa kinapaswa kusambazwa kila kona ya nchi hasa kwenye misitu ya vijiji na kuachana na dhana ya kuhamisha mamlaka kwa Serikali Kuu ambapo usimamizi unaweza kuyumba.

Anasema sera za nchi zinazungumzia ugatuzi wa madaraka hivyo kinachofanyika katika vijiji ni tafsiri sahihi ya sera hiyo kwani Serikali Kuu haina rasilimali watu, vitendea kazi vya kutosha vya kuisimamia.

Kastila anasema kinachohitajika ni elimu zaidi itolewe kwa wananchi kujua umuhimu wa kushiriki katika ulinzi na usimamizi wa rasimali misitu na sio kujilimbikizia majukumu ambayo kuyasimamia sio rahisi.

Anasema pia mradi umewezesha kuwepo kwa Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi kwenye vijiji hali ambayo inaongeza thamani kwenye ardhi za vijiji na wananchi kukopesheka jambo ambalo Serikali Kuu imeshindwa kuwafikia kwa haraka.

Aidha, akizungumzia bei elekezi ambayo imependekezwa kwenye Tangazo la Serikali GN 417 ambayo inataka ushuru wa mkaa kwa gunia iwe shilingi 125,000 anasema kinachohitajika ni usimamizi kwa kila eneo ambalo linazalisha ili kuwe na usawa.

“Hilo sio tatizo iwapo kutakuwa na udhibiti wa biashara holela ya mkaa kwani faida itapatikana kwa kila pande, ila kinyume na hapo watakaoumia ni wale waliopo mbali na baraba,” anasema.

DED KILOSA

Mkurugenzi wa Wilaya ya Kilosa (DED), Asajile Mwambambale anasema USMJ na FBE ni njia muafaka ya utunzaji misitu na kuifanya iwe endelevu kwa vizazi vijavyo.

Anasema wanavijiji ambao wana rasilimali misitu wamekuwa walinzi na mabalozi wa uhifadhi jambo ambalo linapaswa kupewa nguvu ili liwe endelevu.

“Wapo wanaona kuwa wanavijiji wananufaika na fedha sio kweli manufaa makubwa yapo msituni kwa kuwa kila mwananchi analinda msitu akiamini tofauti na kukata mkaa kuna manufaa ya hewa safi, mvua na mazingira kwa ujumla,” anasema.

Mwambambale anasema USMJ na FBE imechangia mapato ya Halmashauri ya Kilosa kuongezeka ambapo hupata asilimia 10 ya makusanyo ya mazao yanayotokana na misitu jambo ambalo halikuwepo awali.

Anasema mradi wa TTCS umekuwa shamba darasa kwa vijiji vingine hivyo wao wanajipanga kusambaza kwa vijiji vingine ambavyo vina misitu ya vijiji na kwamba haoni sababu ya kubadilisha mamlaka ya usimamizi kama GN 417 inavyotaka.

Mkurugenzi anasema kinachohitajika ni changamoto ambazo zipo zinapatiwaufumbuzi na sio kukimbilia kubadilisha mamlaka ya usimamizi kwani inaweza kuwa sababu ya uharibufu kuongezeka zaidi.

Anasema kuhusu bei elekezi kinachohitajika ni usimamizi ambao utahakikisha kila anayejihusisha na biashara ya mazao ya misitu anafuata taratibu zote.

DED huyo anasema Serikali Kuu inapaswa kuhamasisha wawekezaji katika sekta ya uhifadhi na namna ya kuitumia rasilimali misitu kwa njia endelevu kama yanavyofanya mashirika ya TFCG na MJUMITA kupitia TTCS.

“Nisisitize ili misitu iwe salama ni lazima vijiji  viweze kunufaika moja kwa moja ila ikiwa ni kusubiri muda mrefu ni dhahiri watashindwa kuilinda,” anasema.

DNRO KILOSA

“Mimi kwa muda ambao nimekuwa hapa Kilosa ninadiriki kusema ‘USMJ ni sawa na kumpa mchawi akulelelew mtoto hawezi kumloga’ ni maneno ya John Mtimbanjayo Ofisa Maliasili (DNFO).

Anasema miaka saba ya utekelezaji mradi wa TTCS umeweza kuchochea maendeleo makubwa katika vijiji huku uhifadhi ukiwa umechukua nafasi kubwa.

“Zaidi ya shilingi bilioni 1 zimeweza kukusanywa na kutekeleza miradi ya maji, elimu, afya, utaewala na mingine mingi hali ambayo inawapa nguvu wanavijiji kulinda misitu yao hivyo iwapo kinachohitajika kwenye GN 417 kitapewa nafasi kuna uwezekano wa hali kuwa mbaya kimapato na uhifadhi,” anasema.

Mtimbanjayo anasema vijiji vya Ulaya Mbuyuni, Ulaya Kibaoni, Msumba, Uhombwe, Kisanga, Kigunga, Nyali, Kitundueta, Mhenda, Mvumi, Zombo, Chabima,, Gongwe, Rudewa Gongani na vingine vimeweza kufanya mapinduzi ya kiuhifadhi.

DNFO Mtimbanjayo anasema kuhusu bei elekezi ya GN 417 kunahitaji tafakuri ya kina ili isije kuwa sababu ya kuchochea uvunaji ambao haufati taratibu  zilizopo.

“Bei elekezi hadi sasa imeshaleta athari kwa wavunaji wa mkaa kwani wapo ambao wanavuna kiholela hali ambayo inaweza kuzalisha wavunaji haramu katika misitu ya vijiji yenye USMJ na FBE,” anasema.

DIWANI VITI MAALUM

Diwani wa Viti Maalum Halmashauri ya Kilosa, Amina Laizer anasema USMJ na FBE ni mfumo ambao unapaswa kusambaa nchini kote kwa kuwa unatatua changamoto za jamii na kuchochea uhufadhi wa misitu.

Anasema vijiji ambavyo vinatekeleza mfumo huo vimekuwa na mabadiliko makubwa ya kiuchumi, kijamii na maendeleo jambo ambalo linasababisha halmashauri kuhangaika na vijiji vingine ambavyo havina miradi ya maendeleo.

“Mimi nimekuwepo kwenye Baraza la Madiwani kwa misimu miwili ninajua karibu vijiji vyote vya Kilosa kusema kweli vijiji vyenye kutekeleza USMJ na FBE vimekuwa kwenye utulivu mkubwa tofauti na ambavyo havina kwani vina uhakika wa kupata fedha na kutekeleza miradi yake,” anasema.

MTENDAJI WA KIJIJI ULAYA MBUYUNI

Mtendaji wa Kijiji cha Ulaya Mbuyuni wilayani Kilosa, Piolon Lyatuu anasema USMJ, umefanya mapinduzi makubwa katika kijiji hicho kwa kufanikiwa kutatua migogoro ya wakulima na wafugaji baada ya kuweka mpango wa matumizi bora ya ardhi.

Pia anasema manufaa mengine ni ujenzi wa madarasa mawili na ofisi ya mwalimu kwa shilingi milioni 37, wamechimba kisima cha maji chenye urefu wa mita 60 kwa shilingi milioni 20, ofisi ya kijiji imejengwa kwa shilingi milioni 50, afya wameweza kukatia CHF kwa kaya zaidi ya 200.

“Tumeboresha uwanja wa michezo kwa kutumia shilingi milioni moja ambazo zinatoka katika msitu na pia tunaendelea kuboresha soko ili liwe la kisasa,” anasema.

Anasema kutokana na manufaa hayo hawaoni sababu ya Serikali Kuu kujihusisha na USMJ moja kwa moja kwani inaweza kukwamisha hayo ambayo yamepatikana kufanikiwa.

Lyatuu anasema USMJ ambayo imesambazwa na TTCS imeweza kuwajengea uwezo wavunaji kujua ni aina gani ya miti ya kuvuna ambayo inaweza kuwa endelevu.

MWENYEKITI WA KIJIJI ULAYA MBUYUNI

Akizungumzia faida za USMJ na FBE, Mwenyekiti wa Kijiji Selemani Hashimu anasema anaongoza kwa amani kwa kuwa wanakijiji hawasumbuliwi na michango kwani msitu wao unatatua changamoto zote.

Anasema kupitia msitu wapo kwenye mchakato wa kujenga zahanati ya kijiji kwa shilingi milioni 84 hli ambayo itaweza kusogeza huduma za jamii karibu na wananchi.

“USMJ na FBE imewezesha kijiji kuingiza zaidi ya shilingi milioni 100 hali ambayo awali haikuwepo, kinachotutesa kwa sasa ni kuwepo wavamizi kama saba ambao wanapewa kiburi na aliyekuwa diwani,” anasema.

Hashimu anasema Serikali ikiamua kuchukua usimamizi wa misitu inaweza kuchangia uharibufu kuongezeka kwani ulinzi utapungua na vijiji vitashindwa kujiendesha kama ilivyo sasa ambapo wananchi wanapanga mambo yao,” anasema.

Anasema kinachohitajika ni Serikali kuja na mpango ambao utaweza kuendeleza haya yaliyopatikana ili misitu iweze kuwa endelevu.

KAMATI YA MALIASILI ULAYA MBUYUNI

Katibu wa Kamati ya Maliasili Kijiji cha Ulaya Mbuyuni, Victoria Ndekelo anasema pamoja na manufaa ya USMJ na FBE pia wameweza kujifunza mbinu nyingine za ujasiriamali kama mpango hisa, kilimo hifadhi hali ambayo inasaidia kujiingizai kipato.

Ndegelo anasema uhifadhi umeboreka zaidi, ila anaomba Serikali iangalie uwezekano wa kiusimamia kwa nguvu zote bei elekezi ambayo ipo kwenye GN mpya kwa kuwa vijiji vya ndani na vinavyofuata utaratibu vitaumia zaidi.

Aidha, anasema yeye binafsi amenufaika na USMJ na FBE ambapo ameweza kufuga kuku, amejenga nyumba na uhakika wa milo mitatu hali ambayo awali haikuwepo.

Mohammed Titima Mwenyekiti wa Kamati ya Maliasili kijijini hapo anasema USMJ kwakwe ni mkombozi wa maisha kwani amefanikiwa kuanzisha mradi wa ufugaji kuku zaidi ya 300, kilimo hifadhi na kushiriki mpango hisa kwa uhakika.

Anasema bei elekezi itakuwa na faida iwapo kila muuza mkaa kijijini ataifuata kinyume na hapo ni wazi kuwa uharibifu wa misitu utaongezeka zaidi na zaidi.

TFS WILAYA

Meneja Misitu wa Wakala wa Huduma za Misitu Wilaya ya Kilosa Samuel Nyabange anasema USMJ pekee haiwezi kufanikisha uhifadhi hivyo jambo la msingi ni elimu zaidi kutolewa kuhusu hasara na manufaa ya kutumia rasilimali misitu kinyume na utaratibu.

“Hakuna shaka kuwa USMJ ni njia sahihi ya kukabiliana na uharibifu wa misitu na mazingira lakini jambo la muhimu ni kujikita katika kutoa elimu zaidi kwani kokote ambapo kuna uharibifu lazima wanavijiji wanashiriki,” anasema.

KAMISHNA MHIFADHI TFS

Akijibu baadhi ya maswali ya waandishi Kamishna Mhifadhi TFS, Profesa Dos Santos Silayo anasema ushiriki wa wananchi kupitia  kamati za maliasili za vijiji  ni muhimu katika kulinda misitu ikiwa zitaelimishwa na kuratibiwa vizuri.

“Kamati hizi zinaweza kwa kiasi kikubwa kulinda misitu iliyoko karibu na vijiji vyao. Suala muhimu ni elimu na uwazi  kwa kuwashirikisha  ipasavyo katika maamuzi na hasa  kuhusu  faida zitokazo na misitu wanyopaswa kuilinda. Kwa misitu inayoruhusu uvunaji wananchi wanaweza kupata faida za moja kwa moja kutokana na mazao yanayovunwa,” anasema.

Anasema tatizo kubwa ni ushirikishwaji katika misitu isiyoruhusu uvunaji  misitu ambayo  ni kwa ajili ya uhifadhi wa mazingira. “Katika misitu hii ushirikishwaji umeimarishwa  kwa  kusaidia wananchi kuanzisha miradi mbadala ya kiuchumi  kama ufugaji wa nyuki juhudi ambazo zimeonyesha mafanikio katika  kuhifadhi misitu hiyo.

Kuhusu bei elekezi anasema kwa   kiwango kikubwa mkaa hutumika zaidi kwa wakazi wa mijini maeneo ambayo pia upatikanaji wa nishati mbadala ikiwepo gesi vinapatikana.

“Kwa maoni yangu mimi bei elekezi haina tatizo kwani mazao yote ya misitu yana bei elekezi hata  magogo ya mbao yamewekewa bei na serikali.  Kuhusu uvunaji holela ambao umekuwa ukilalamikiwa, uvunaji huu hufanyika kwa wingi kwenye maeneo ya ardhi huria ambapo hata bila ya kuwepo kwa bei elekezi uvunaji huu utafanyika.

Ufumbuzi wa tatizo hili sio bei elekezi bali ni usimamiaji wa sheriaa ili kuhakiksha uvunaji unafanyika katika maeneo yanayoruhusiwa na kwa kuzingatia sharia. Bei elekezi  ilipangwa kwa makusudi ya kupunguza matumizi ya mkaa kwa kuufanya mkaa usiwe rahisi kiasi cha kuwafanya watu wasione umuhimu wa kutumia gesi na nishati zingine mbadala,” anasema.

Prof. Silayo anasema kwa mawazo yake anadhani tunapaswa kuongeza bei ya mkaa unaotokana na miti ya asili zaidi ili kushawishi watu watumie nishati mbadala au kuzalisha mkaa kutoka katika miti ya kupandwa inayokua haraka ili kuepusha nchi yetu kugeuka jangwa.

Aidha, kuhusu Kanuni kudaiwa kwenda kinyume na Sheria ya Vijiji vya mwaka 2002 ambayo katika 1(b) inasema kwamba lengo la sheria hiyo ni pamoja na kuhamasisha katika kupanga, kusimamia, kutumia na kuhifadhi rasilimali za misitu kiendelevu kupitia haki ya maendeleo kwa mtu mmoja mmoja na jamii kama ilivyoelekezwa kwenye sheria ya kimila au sheria ya misitu ya mwaka 2002 katika kutumia na kusimamia rasilimali za misitu.  Kwa nini wananchi wasiendelee kujipangia bei zao na ushuru.

Profesa anasema wanapozungumzia suala la biashara ya  mkaa tusilichukulie kiurahisu tu kuwa mkaa ni bidhaa ya kuuzwa sokoni, ni vyema tukaangalia biashara ya mkaa kama biashara ambayo inapaswa kufanywa kwa umakini sana kutoana na madhara ya biashara hiyo kimazingira. 

“Badala ya kuhamasisha biashara ya mkaa tunapaswa kufanya udhibiti kwani kushamiri kwa biashara  holela ya mkaa  ni kuchocheo kikubwa cha uharibifu wa mazingira. Biashara hii ni lazima iwekewe utaratibu na serikali ikiwepo kuwekewa masharti na bei  elekezi ya bidhaa hiyo ili kutunza mazingira.

Kuruhusu kila Kijiji kijipangie bei kitakayo kutavutia watu wengi kukimbili vijiji ambavyo vimejipangia bei ndogo na  kuacha kazi rafiki wa mazingira na kuanza kufanya kazi ya kuchoma mkaa  jambo amblo linaweza kuathiri hali ya hewa  na kuchochea  mabadiliko ya tabia ya nchi,” anasisitiza.

Kamishna Silayo anasema kwa mujibu wa sheria ya misitu Mkurugenzi wa misitu amepewa malaka kusimamia msitu yote hapa nchini. Tangazo la Serikali Na 417 kama mwenyewe ulivyosema  linalenga kuboresha usimamizi na uendeleza wa misitu kwa kusisitiza umuhimu wa kuwa  wa mipango ya usimamizi misitu na kuzuia uvunaji holela wa misitu. 

Kwa mamlaka aliyopewa kwa mujibu wa sheria mkurugenzi  wa misitu anapaswa kuidhinisha mipango ya uvunaji ambao utakuwa umeandaliwa na wamiliki wa msitu sharia kanuni na miongozo kwa kuhakikisha kuwa mipango hiyo inafuata mwongozo kuapelekea kuwepo kwa uvunaji wa mazao ya misitu.
Anasema wananchi na wamiliki hawapaswi kuwa na woga kwani mkurugenzi anaizinisha  mipango ya usimamizi wa misitu kuhakikisha inakidhi matakwa ya kisheria unazingaztia muongozo kabla  ya kuruhusu uvunaji. Wajibu huu hauwapokonyi wananchi mamlaka ya matumizi ya msitu wao bali unawataka watimize wajibu wao wa kuhakikisha kuwa uvunaji unakuwa endelevu.

No comments:

Post a Comment

Pages