HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

February 03, 2021

GePG yasaidia TANESCO kuokoa Bil 38

 


Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Richard Kwitega, akifungua semina ya wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari jijini Arusha kuhusu Mfumo wa Ukusanyaji Mapato Serikalini (GePG).

 

NA BETTY KANGONGA 


MFUMO wa kieletroniki wa Serikali wa ukusanyaji wa fedha za umma umesaidia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuokoa zaidi ya Sh. Bilioni 38 iliyokuwa ikilipa kwa mwaka kwa mawakala wa kuuza umeme nchini. 

Akifungua semina ya wahariri wa vyombo vya habari nchini iliyofanyika jijini Arusha, Katibu Tawala Mkoa wa Arusha Richard Kwitega alisema, Wizara ya Fedha na Mipango imebuni na kuunda Mfumo wa Kielektoniki unaotumika kukusanya Fedha zote za Umma unaojulikana kama “Government e-Payment Gateway” au kwa kifupi “GePG.

Alisema kuwa, mfumo huo umewezesha kupanda kwa mapato ya serikali baada ya kuboreshwa kwa mfumo huo.

Kwitega alisema, kutokana na kuanza kutumika kwa mfumo huo taasisi zimepunguza gharama walizokuwa wanalipia ada za miamala ya kielektroniki inayohusu makusanyo ya fedha za umma akitolea mfano TANESCO iliyokuwa ikilipa zaidi ya Sh. Bilioni 38 kwa Mwaka kwa mawakala wa kuuza umeme ambapo baada ya kufunga mfumo wa GePG kwa sasa shirika halilipi chochote.

Alitaja taasisi nyingine zilizopandisha makusanyo yake ni Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) ambayo yameongezeka kutoka Sh. Bilioni 95 kabla ya kuanza kwa mfumo hadi kufikia Sh.Bilioni 115 baada ya kuanza kutumia mfumo wa kielektroniki.

Wengine ni Wakala wa Vipimo (WMA) mapato yao yameongezeka kutoka kiasi cha Sh. Bilioni 1kwa mwezi kabla ya Mfumo wa GePG mpaka kufikia Sh. Bilioni 2.5 kwa mwezi baada ya kujiunga na GePG.

Alisema kuwa, Mfumo huu umebuniwa na kutengenezwa na wataalamu wa ndani wa Serikali ambapo upo kwa mujibu wa Sheria ya Fedha za Umma (PFA) ya mwaka 2001 kupitia marekebisho ya mwaka 2017 (Sura 348), na Waraka wa HAZINA Namba 3 wa mwaka 2017.

"Sheria ya Fedha za Umma inawataka Maofisa Masuuli wote kukusanya fedha za Umma kupitia Mfumo wa GePG. Mfumo huu ulianza kutumika rasmi Julai mosi, mwaka 2017 ambapo ulianza na taasisi saba (7) lakini kwa sasa Mfumo huu unatumiwa na taasisi za Umma zaidi ya 600. Mfumo huu ndiyo unatoa kumbu kumbu namba (“Control number”) ya kulipia huduma na tozo mbalimbali za Serikali," alisema.

Kwitega alisema, kuwa Mfumo huu wa GePG ulianzishwa ili kukabiliana na changamoto mbalimbali zilizokuweko serikalini katika zoezi zima la ukusanyaji wa fedha za Umma. 

Alitaja changamoto hizo ni pamoja na; Gharama kubwa za miamala inayohusu makusanyo ya fedha za umma; Utaratibu usio rafiki kwa mlipaji wa huduma za Umma unaoanzia namna anavyopatiwa ankara, anavyolipia ankara yake, anavyothibitisha malipo, anavyopatiwa stakabadhi hadi  anavyopatiwa huduma; 

Pia alitaja changamoto nyingine ni kulikuwa na machaguo (options) machache ya njia za kulipia (Mabenki, Mitandao ya simu za mkononi au Mawakala) kwa sababu kuongeza machaguo kulikuwa kunaongeza gharama za ukusanyaji kwa taasisi; 

"Ilipohitajika kufungamanisha Mfumo wa Ankara wa taasisi na Mifumo ya Ulipaji (kama vile mabenki, Mitandao ya simu za mkononi na Mawakala wakubwa (Aggregators) gharama ilikuwa kubwa kwa sababu kila Mfumo ulifungamanishwa peke yake; Ilikuwa ni vigumu sana kupata taarifa ya makusanyo yanayofanyika kwa wakati huo huo (“Real time collection reports”). Alisema.

Kwitega alisema, Wizara ya Fedha na Mipango inatambua kuwa Mafanikio ya mfumo huu wa GePG yanategemea sana ushiriki wa wananchi wote katika kuutumia. Hivyo, kila mwananchi anayelipia huduma yoyote ya Umma ni lazima ahakikishe kuwa amepewa “Control number” na taasisi inayotoa huduma hiyo, na akiwa analipa ahakikishe amelipa kwa kutumia “Control number” hiyo.

No comments:

Post a Comment

Pages