HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

July 01, 2013

SIMBA WAFANYA ZIARA MIKOANI



Na Elizabeth John
KLABU ya Simba ya jijini Dar es Salaam, imesema mara baada ya kuondoka kwa Rais wa Marekani, Barrack Obama nchini, itafanya ziara katika mikoa ya Katavi, Tabora na Rukwa kwa kucheza mechi za kirafiki kwa ajili ya kujiandaa na Ligi Kuu Bara.

Mbali na kwenda katika mikoa hiyo, pia ipo katika mchakato wa kupiga kambi katika moja ya nchi jirani kwa ajili ya maandalizi zaidi ya ligi hiyo.


Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa klabu hiyo, Ismail Aden Rage alisema wamepata mwaliko kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Rajab Rutengwe akiomba timu hiyo iende mkoani kwake.


“Tumepokea mwaliko kutoka kwa rafiki yangu Shehe Rajab ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Katavi  akituomba tukamtembelee na kikosi changu chote, na sisi tupo tayari hatuna tatizo katika hilo,”.

“Kikubwa tunachosubili kama unavyojua hivi sasa nchi ina ugeni mkubwa wa Rais Obama, hivyo kila mtu yupo katika pilikapilika hizo lakini baada ya kuondoka tutasema tarehe rasmi ya kuondoka,”.


Alisema wakiwa huko wanatarajia Waziri Mkuu, Mizengo Pinda atakuwa mgeni rasmi katika mechi watakazocheza ambapo pia waziri huyo ameiomba timu yake ifike mpaka Jimboni kwake Mpanda Magharibi, Rukwa.


Alisema wakiwa katika mikoa hiyo pia watakwenda Tabora kucheza mechi ya kirafiki na baada ya kumaliza ziara hizo watarejea jijini Dar es Salaam.


Aliongeza kuwa wapo katika mipango ya kuhakikisha timu yake inaweka kambi moja ya nchi jirani ambapo ana uhakika baada ya kufanya hivyo, kikosi chake kitakuwa tayari kwa ligi kuu ya msimu ujao.


Wakati Simba ikijinadi hivyo, watani wao Yanga, wanatarajia kuondoka Ijumaa kwenda Kanda ya Ziwa kwa ajili ya kulitembeza kombe lao la ligi kuu pamoja na kucheza mechi ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya KCC ya Uganda.


Mbali na hayo, pia itaingiza wanachama wapya pamoja na kuuza vifaa mbalimbali walivyonavyo.

No comments:

Post a Comment

Pages