HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

January 09, 2017

TANZANIA KUENDELEZA USHIRIKIANO NA CHINA

Waziri  Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Watu wa China,   Wang Yi   (kulia kwake) kwenye makazi yake, Oysterbay jijini Dar es salaam Januari 9, 2017.  Kushoto kwake ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa,  Augustine Mahiga na wanne kulia ni Balozi wa China nchini, Lu Youqing. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).


Dar es Salaam, Tanzania

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali ya Tanzania itaendeleza ushirikiano na Serikali ya China katika nyanja mbalimbali kupitia uwekezaji kwenye sekta ya viwanda, nishati na miundombinu.

Ametoa kauli hiyo leo (Jumatatu, Januari 9, 2017) alipokutana na  Waziri wa Mambo ya Nje wa China, Mheshimiwa Wang Yi, kwa niaba ya Mheshimiwa Rais Dk. John Magufuli kwenye makazi ya Waziri Mkuu, Oysterbay jijini Dar es Salaam.

Waziri Mkuu amesema ushirikiano wa Tanzania na China ni wa kihistoria, hivyo ameihakikishia Serikali ya China kwamba utaendelezwa kwa manufaa ya wananchi wa Mataifa yote mawili.

Aidha, Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji kutoka nchini China kuja kuwekeza  katika sekta mbalimbali nchini zikiwemo za miundombinu, viwanda, kilimo na nishati.

 “Tanzania iko tayari kupokea kampuni zaidi za China kuja kuwekeza katika maeneo mbalimbali nchini.Tupo tayari kupokea viwanda kati ya 200 hadi 700 katika kipindi cha miaka mitatu ijayo,” amesema.

Kwa upande wake Mheshimiwa Wang Yi amepongeza utendaji kazi wa Mheshimiwa Rais Dk. Magufuli pamoja na viongozi wengine hususan katika mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi na tayari matunda yameanza kuoneka.

“Serikali ya China kwa sasa iko katitka mkakati wa kuhamishia viwanda vyake vingi Barani Afrika. Iliamua kuichagua Tanzania kuwa moja katika ya nchi watakayohamishia viwanda hivyo kutokana na kuridhishwa na dhamira inayoonyeshwa na Serikali katika kuleta maendeleo,” amesema.

 IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
2 MTAA WA MAGOGONI,
S.  L. P. 3021,

JUMATATU, JANUARI 9, 2017

No comments:

Post a Comment

Pages