HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

March 06, 2013

ABSALOM KIBANDA AZUNGUMZA TUKIO LA KUJERUHIWA KWAKE, PIA TASWA YATOA TAMKO

Kwa mujibu wa maelezo ya mgonjwa aliyekaririwa akizungumza kwa shida, ameeleza kuwa, majira ya usiku wakati akiingia nyumbani kwake alivamiwa na watu watatu --mmoja akiwa ameshika bastola na wawili wakiwa wameshika nondo-- ambapo alipofika nje ya nyumba yake, watu hao walilivamia gari lake, wakauvunja mlango wa gari lake, wakamtoa nje, wakaanza kumpiga vibaya sana, wakamtoa meno mawili, wakamng'oa kucha katika moja ya vidole vyake na kumtoboa jicho lake kwa nondo. 
Absalom Kibanda akiwa hospitalini
Mhariri Mkuu wa Kampuni ya New Habari wachapishaji wa magazeti ya Mtanzania, Dimba, Bingwa na Dimba, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) ndugu, Absalom Kibanda amevamiwa na watu wasiojulikana akiwa ndani ya gari lake wakati akiingia nyumbani kwake huko Mbezi-Beach, jijini Dar es Salaam.


Akielezea tukio hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya New Habari, Hussein Bashe amesema Kibanda alivamiwa majira ya saa sita usiku wa jana, akitokea kwenye majukumu yake ya kila siku. Inadaiwa kuwa alitolewa kwenye gari, akapigwa kichwani, akajeruhiwa jichoni na kisha kutelekezwa mbali kidogo ya nyumbani kwake.


Wasamaria wema waliomwona walimpeleka katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, ambako alipokelewa vizuri na madaktari na kumpatia tiba ya awali na baadaye kumhamishia kwenye Taasisi ya Tiba ya Mifupa (MOI) ambako mpaka sasa anaendelea na matibabu.


Watu waliotenda ukatili huo hawakuchukua kitu chochote kwenye gari.


Taarifa za awali pamoja na picha vimetolewa na Chogolo kupitia kundi pepe la MabadilikoTanzania (bofya hapa kuendelea kusoma updates/taarifa mpya/reactions zinazotolewa kuhusiana na tukio hili).

(Picha iliyopigwa na Chogoloh saa tisa usiku hospitalini Muhimbili)
Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo (TASWA), Juma Pinto, amesema kuwa watu waliohusika na tukio la kuvamiwa na kupigwa kwa Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri, Absalom Kibanda wakamatwe ili sheria ichukue mkondo wake.

Tusingependa kama waandishi kuamini yanayosemwa lakini kutokana na uadilifu mkubwa wa vyombo vyetu vya ulinzi na Usalama kuwapata watu ambao wamehusika na tukio hilo.


Sisi tunaamini tukio hili la mwenzetu kuvamiwa na watu hao halikuwa kwa bahati mbaya ni Jambo ambalo linaonekana Kama limepangwa na Kama ni hivyo lengo na madhumuni yake ni nini kwa waandishi wa Tanzania? Uhuru na Usalama wa waandishi upo wapi?


Katakana na tukio hili la mpiganaji na Kiongozi wetu kuvamiwa ,ipo haja ya sisi waandishi kuungana pamoja katika kutafuta Usalama wetu. Kuna matukio mengi ya waandishi yametokea na tumekuwa tukipiga kelele lakini matokeo yake hakuna hatua ambazo serikali inayafanyia kazi.


Kutokana na majeraha makubwa aliyopata mwenzetu, tunaiomba serikali na hasa Mheshimiwa Rais, Dr. Jakaya Kikwete kutoa Msaada wa mwenzetu kwenda kutibiwa nje,tunaamini serikali ni sikivu na Rais wetu ni mwenye kusikia kilio cha watu wake.


Kibanda na wenzake ndani ya Jukwaa la wahariri wamekuwa mstari wa mbele katika kurudisha hadhi ya tasnia ya habari na kujenga umoja miongoni mwa waandishi wa habari na kuifanya tasnia ya habari kuheshimika tofauti na ilivyokuwa nyuma.


Tunaungana na kampuni ya habari, wafanayakazi wenzake, familia yake na waandishi wote kwa jumla na kumuomba Mungu amponye ili tuweze kuungana nae katika kusaidia kupasha habari Watanzania lakini ili aweze kuwaongoza waandishi wenzake.


No comments:

Post a Comment

Pages