HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

November 19, 2014

WAENDESHA BODABODA WALALAMA

WASAFIRISHAJI abiria kwa kutumia bajaji na bodaboda jijini Dar es Salaam, wamelaani kitendo cha serikali cha kuwakamata wanapoingia katika ya jiji kwa madai kuwa ni kinyume cha sheria.

Wakizungumza jijini Dar es Salaam wasafirishaji hao, walisema kinachofanywa na serikali ni uonevu kwa sababu watu hao wanajitafutia riziki kwa ajili ya familia zao.

Mmoja wa Wasafirishaji hao, Mohamed Juma ambaye ni mmoja kati ya watu wenye ulemavu, alisema wanaalani kitendo hicho kwa sababu serikali yenyewe ndio imeamua kuingiza vyombo hivyo ili kupunguza tatizo la ajira kwa vijana, ambalo ni sawa na bomu linalosubiri kulipuka wakati wowote.

Alisema, wanashangaa kuona serikali ikiwashupalia wakafanye biashara hiyo pembezoni mwa jiji wakati wakijua fika kwamba hata huko nako yapo makundi ya vijana wanaofanya biashara hiyo.

“Unajua hii biashara ya usafirishaji inafanywa na makundi ya vijana katika maeneo mbalimbali ya jiji hivyo siyo rahisi kwa kutuondoa sisi tulioko katikati ya jiji na kutupeleka kwingine ambako nako tayari wapo, hii inaweza ikazusha ugomvi wa kimaslahi,”alisema Juma.

Juma, alisema watajaribu kutafuta muafaka na serikali kuhusu suala hilo na endapo itashindikana huenda huko mbeleni wakafikiria kurudisha vyombo hivyo serikalini kwa pamoja.

Charles James, muendesha bodaboda alisema, kama biashara hiyo ni haramu kufanyika katikati ya jiji basi ni vema serikali ikasimamisha uingizaji wa vyombo hivyo ambavyo vinadaiwa kuingizwa kwa wingi bandarini kuliko mzigo wowote.

“Sio kweli kama wamesimamisha operesheni hiyo kama wanavyodai baadhi watu eti kwa ajili ya uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika hivi karibuni,”alisema James.

James, alisema hata kama ikitokea hivyo hadhani kama kuna ulazima wa kushangilia, kwa sababu bado tatizo lipo la kuvunjwa haki zao ambazo ni kuuziwa vyombo hivyo kisha kuwekewa mipaka ya matumizi.

Alisema wakati watu wenye ulemavu wakijiaandaa kuvikusanya vyombo hivyo na kwenda kuvirundika kwenye ofisi ya Mkuu wa Mkoa Said Meck Sadik, wao waendesha bodaboda wanajipanga jinsi ya kujiunga nao katika kadhia, hata hivyo hawakufafanua  lini watafanya hivyo. 

No comments:

Post a Comment

Pages