SERIKALI
inatarajia kukusanya sh. bilioni 200 kwa mwaka, ikiwa ni mapato ya kodi baada
ya kukamilika kwa ujenzi wa kiwanda cha kimataifa cha Kiluwa Steel Group kitakachokuwa
na uwezo wa kuzalisha tani 3,000 za nondo kwa siku.
Awamu
ya kwanza ya ujenzi wa kiwanda hicho kinachomilikiwa na mwekezaji mzawa kwa kushirikiana
na Wachina, inatarajiwa kukamilika Oktoba, mwaka huu ambapo fedha hizo zitapatikana
baada ya kukamilika awamu tatu za ujenzi wake.
Akizungumza
mbele ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa aliyetembelea kiwanda hicho jana (Jumanne,
Julai 12, 2016), Mkurugenzi Mtendaji wa kiwanda hicho, Bw. Mohammed Kiluwa alisema
ujenzi huo utasaidia kuimarisha uchumi.
“Kukamilika
kwa mradi huo, kutaongeza kasi ya ukuaji wa uchumi wa nchi, upatikanaji wa
ajira pamoja na kufanikisha azma ya serikali ya awamu ya tano ya kuifanya
Tanzania kuwa nchi ya maendeleo ya viwanda,” alisema.
Alisema
kiwanda hicho kitazalisha nondo kwa matumizi ya ujenzi pamoja na vifaa vingine
vinavyohusiana na bidhaa za chuma. “Lengo ni kuweza kuuza malighafi hizo kwenye
viwanda vingine vya chuma nchini na nchi jirani kwa kuzingatia ubora unaokidhi mahitaji
ya soko la kimataifa,” alisisitiza.
“Katika
awamu ya kwanza ya ujenzi, tunatarajia kutumia dola milioni 40; awamu ya pili
tutatumia dola milioni 50 na dola milioni 200 zitatumika kwenye awamu ya tatu
ili kukamilishia ujenzi wa kiwanda hiki,” alisema.
Kiluwa
alisema, awamu ya kwanza inatarajiwa kukamilika Oktoba mwaka huu, ambapo awamu
ya tatu itakamilika Februari mwakani. Kikikamilika, kinatarajiwa kuajiri vijana
zaidi ya 500 wa Kitanzania.
Kwa
upande wake, Waziri Mkuu alisema lengo la ziara hiyo ni kukagua maendeleo ya
ujenzi wa kiwanda hicho kikubwa cha kwanza kinachojengwa na mwekezaji mzawa.
“Uwekezaji
sio lazima ufanywe na watu wa nje, Watanzania wana nafasi ya kuwekeza katika
sekta mbalimbali, Kiluwa amefungua njia hivyo wengine wafuate nyayo zake. Uwezo
tunao na sababu ya kuwekeza tunayo, kwani tunataka tuzalishe bidhaa mbalimbali sisi
wenyewe,” alisema.
Aliongeza
kuwa uwepo wa kiwanda hicho katika eneo la Disunyara, Mlandizi mkoani Pwani,
utawezesha kuboresha hali ya uchumi kwa wakazi wa eneo hilo na Taifa kwa
ujumla.
Waziri
Mkuu alitolea mfano kwa wakazi wa Mtwara, ambao wamenufaika kutokana na ujenzi
wa kiwanda cha saruji cha Dangote ambapo awali walikuwa wakinunua saruji kwa
sh. 17,000, lakini hivi sasa wanainunua kwa sh. 7,000.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alilitaka Shirika la Umeme Tanzania
(TANESCO) lipeleke umeme mapema kwenye eneo hilo ili kuharakisha shughuli za uwekezaji.
No comments:
Post a Comment