Waziri wa Ujenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa pili kulia) akitoa maelekezo
kwa Meneja wa Kiwanja cha ndege cha Kikwetu Mkoani Lindi Bw. Boniface Njanda (Wa
kwanza Kulia) wakati alipotembelea uwanja huo.
Meneja wa Wakala wa
Barabara nchini (TANROADS) mkoa wa Lindi Eng. Isaac Mwanawima akitoa taarifa ya
utendaji wa Wakala huo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa
Makame Mbarawa (wa kwanza kushoto) wakati alipotembelea wakala huo.
LINDI TANZANIA,Waziri wa Ujenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa ameutaka uongozi wa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na
Majini (SUMATRA) kutoa adhabu kali kwa wamiliki wa vyombo vya usafirishaji na
madereva wazembe wanaosababisha ajali za barabarani.
Ameyazungumza hayo wakati
wa ukaguzi wa utendaji kazi kwa wafanyakazi wa taasisi zilizopo chini ya
Wizara hiyo pamoja na miundondombinu ya Barabara, Bandari, Mawasiliano na
kiwanja cha ndege cha Kikwetu mkoani Lindi.
Profesa Mbarawa amesema
kuwa ongezeko la ajali zinazosababisha vifo kutokana na uzembe wa madereva, kutofuata
sheria na alama zinazowekwa barabarani
zizidhibitiwe ili kuokoa maisha ya watanzania na nguvu kazi ya Taifa.
“Nataka kuona wamiliki
wa vyombo vya usafiri na madereva wazembe wanaposabisha ajali na kuua watu
wanafutiwa leseni zao vile vile nawataka mfikirie kwanini watanzania wengi
wanaendelea kufa kwa ajali za barabarani ili muweze kutafuta ufumbuzi wa namna
ya kudhibiti ajali hizo”, amesisitiza Prof. Mbarawa.
Katika
hatua nyingine Waziri Mbarawa amemuagiza Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya
Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Eng. George Sambali kukamilisha kazi ya
kupima eneo la kiwanja cha Kikwetu ili kupata hati miliki na kudhibiti uvamizi
wa kiwanja hicho.
“Kama
kiwanja hiki hakitapimwa watu watavamia eneo la kiwanja na Serikali italazimika
kuingia gharama za kulipa fidia hivyo kuchelewesha maendeleo ya uwanja huo”,
amesema Prof. Mbarawa.
Ameongeza
kuwa Serikali iko kwenye hatua za mwisho za kutafuta fedha kwa kushirikiana na
Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) ili kuimarisha miundombinu ya kiwanja hicho
na kuongeza chachu ya maendeleo Mkoani
humo.
Naye
Meneja wa Uwanja wa Ndege wa Kikwetu, mkoani Lindi Bw. Boniface Njanda amemuhakikishia
Waziri Prof. Mbarawa kuwa Mamlaka itafanya tathmini ya Kiwanja hicho kabla ya
kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami.
Waziri
Mbarawa yupo katika ziara ya kukagua utendaji kazi kwa wafanyakazi wa taasisi
zilizopo chini ya Wizara na kuangalia maendeleo ya utekelezaji wa miradi katika
kanda ya kusini.
Imetolewa na Kitengo
cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
No comments:
Post a Comment