HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

February 24, 2017

KUKANUSHA TAARIFA ZA UZUSHI KUHUSU AFYA YA MZEE MWINYI

Dar es Salaam, Ijumaa, Februari 24, 2017:  

Kumekuwa na habari zinazoenea na kujirudia sana katika mitandao ya kijamii kuhusu hali ya afya ya Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili, Alhaji Alli Hassan Mwinyi. Taarifa hizo ambazo hazieleweki lengo lake, zimekuwa zikidai kuwa Mzee Mwinyi amefariki dunia.

Tutautaarifu umma kuwa habari hizo si za kweli, ni za kupuuzwa. Mzee Mwinyi ni mzima wa afya, anaendelea na majukumu yake kama kawaida ambapo jana Alhamisi amehudhuria chakula cha jioni kuadhimisha siku ya Taifa la Kuwait na leo mchana alitarajiwa kwenda kumjulia hali Waziri Mkuu Mstaafu, Cleopa David Msuya.

Natumia fursa hii kuendelea kuwakumbusha watumiaji wa mitandao ya kijamii kuwa waliobuni teknolojia hii walikuwa na malengo adhimu ya kumpatia mwanadamu uwanja na uwanda mpana wa mawasiliano-tusiwachezee shere wabunifu hao kwa kuitumia kinyume cha malengo.

Aidha, jamii ifahamu kuwa ni kosa kwa mujibu wa kifungu cha 16 cha Sheria ya Makosa ya Mitandaoni, 2015, kwa mtu yeyote kutangaza, kuchapisha au kueneza habari za uongo au uzushi katika mitandao.

Kwa niaba ya Serikali nachukua fursa hii kuwapa pole familia ya Mzee Mwinyi na watanzania wengine kwa mshtuko walioupata kutokana na uzushi huu. Katika hili hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya watakaobainika kuhusika na uhalifu huu.

Imetolewa na:
signature2
 

Dkt. Hassan Abbasi

Mkurugenzi, Idara ya Habari-MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali


No comments:

Post a Comment

Pages