HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

March 13, 2018

CUF yakutana na IRI

NA SULEIMAN MSUYA

CHAMA cha Wananchi (CUF), kimekutana na Mkurugenzi Mwakilishi wa Taasisi ya Kimataifa ya International Republican (IRI) Peter Okong'o na kuzungumza juu ya hali ya kisiasa nchini Tanzania na umuhimu wa wadau wote kushirikiana kuhakikisha demokrasia ya Tanzania inalindwa. 

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ya chama hicho, Julius Mtatiro katika taarifa yake aliyotoa kwa vyombo vya habari jana baada ya kukamilika kwa mazungumzo hayo.

“Nimemweleza ndugu Okong'o kuwa, wao IRI wanaweza kuendelea na kazi ya kushauri vyama vya siasa, serikali, taasisi za kidemokrasia, lakini kwa kweli sisi viongozi wa vyama na watanzania ndiyo wenye jukumu la kupigania haki na mabadiliko ya kweli,” alisema. 

Mwenyekiti huyo alisema baada ya maelezo ya kutosha kutoka CUF, Okong'o amewahakikishia kuwa taasisi yao itaendelea na juhudi zake za kufanya kazi na serikali wadau wote ili kujenga uwezekano wa kujenga utangamano na mabadiliko yanayotakiwa na wananchi. 

“Nimemhakikishia kuwa CUF na viongozi wake wako imara na watatoa mchango wao kwa nchi yao bila kukata tamaa, maana mabadiliko hayataletwa kwenye sahani bila kupiganiwa na wadau,” alisema. 

Mtatiro alisema Okong'o yumo katika ziara maalim ya kuwatembelea wakuu wa vyama hapa nchini Tanzania, taasisi za kiraia, taasisi za usimamizi wa uchaguzi (NEC na ZEC) na Serikali.

Alisema IRI ni taasisi isiyo ya Kiserikali na kisiasa lakini imejikita katika kushauri kuhusu uhuru na demokrasia duniani ikiwemo na kusaidia vyama vya siasa ili viweze kufikisha ujumbe kwa wananchi kuhusu mipango mbalimbali ambayo Serikali imeweka kuhusu wao.

No comments:

Post a Comment

Pages