HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 27, 2018

Wahandisi watakiwa kuchangamkia fursa


NA MWANDISHI WETU

WAZIRI wa Viwanda,  Biashara na Uwekezaji Charles Mwijage, amewataka wahandisi nchini kuchangamkia fursa za uwekezaji katika viwanda nchini ili kuiwezesha Serikali kufikia lengo la uchumi wa kati na jumuishi ifikapo 2025.

Mwijage alisema hayo jana wakati akifungua kongamano la siku moja la wahandisi kuhusu mchango wa wahandisi katika sekta ya viwanda jijini Dodoma.

Alisema mchango wa wahandisi ni muhimu sana katika kipindi hiki ili kuwezesha taifa kufikia uchumi wa kati wenye uwiano kati ya pato la nchi na uchumi wa mwananchi.
“Tumejipanga kuanzisha viwanda vinavyotumia malighafi zinazozalishwa hapa nchini ili kuongeza thamani ya mazao ya kilimo na hivyo kugusa uchumi wa wananchi wengi” alisema Mwijage.

Alisema uwekezaji katika viwanda vya sukari, mafuta na vifaa vya ujenzi ambavyo vyote malighafi zake zinapatikana nchini, utawezesha idadi kubwa ya wananchi wa Tanzania kupata ajira na hivyo kufikia lengo la Taifa  la uchumi wa kipato cha kati.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili wa Wahandisi nchini (ERB), Mhandisi Profesa Ninatubu Lema ameiomba Serikali kuthubutu kuwaamini wahandisi wazalendo kusimamia 
na kutekeleza miradi mikubwa ya ujenzi hapa nchini.

Prof. Lema alisema wahandisi wako tayari hata kupewa sehemu kidogo ya ujenzi wa Reli ya Kisasa ya (Standard Gauge), ili nao waweke alama ya uzalendo katika mradi huo mkubwa unaotekelezwa nchini.
“Tunapoadhimisha miaka 50 ya ERB tuko wahandisi tuliosajiliwa zaidi ya elfu 21 tunaweza kufanya kitu kama alama kwa taifa na vizazi vijavyo”,  alisema Lema.

Amewataka wahandisi kutathmini namna gani wanaweza kuendeleza kilimo na viwanda nchini ili kuweza kubadili uchumi wa wananchi na taifa kwa ujumla katika miaka ijayo.

Kaimu Msajili wa ERB, Mhandisi Patrick Barozi, alisema kongamano la wahandisi kuhusu uchumi wa viwanda ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya Bodi ya wahandisi yanayofanyika katika sekta mbalimbali za kihandisi yatakayofikia kilele chake mwezi Septemba mwaka huu.

Alisema lengo la kongamano hilo ni kuwakutanisha wahandisi pamoja kutafakari na kuhamasishana kuhusu namna bora ya kuendeleleza taaluma ya uhandisi kukuza uchumi wa nchi na wa mtu mmoja mmoja.

No comments:

Post a Comment

Pages