HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

August 21, 2018

RC TABORA TOENI VITAMBULISHO KWA WAZEE WOTE BILA UBAGUZI

NA TIGANYA VINCENT, TABORA

SERIKALI ya Mkoa wa Tabora imetoa muda wa mwezi mmoja kwa Maofisa Ustawi wa Jamii wa  Wilaya zote kuhakikisha wamekamilisha zoezi la kuwatambua na kuwapatia vitambulisho vya matibabu kwa  wazee wote ambao wana umri wa  miaka 60 kuendelea.
Agizo hilo limetolewa jana na Mkuu wa Mkoa wa Tabora  Aggrey Mwanri wakati wa uzinduzi wa Baraza la Wazee Mkoani humo na baada ya takwimu za waliopatiwa vitambulisho hadi sasa kuwa kidogo wakati wazee wengi wakiwa bado hajapatiwa.
Alisema kati ya wazee  74,454 waliotambuliwa  ni 26,000 ndio wameshapata vitambulisho hivyo na kuongeza wengine bado hawajatambuliwa.
Mkuu huyo wa Mkoa alikasilishwa na Halmashauri ya Manispaa ya Tabora kwa kutoa vitambulisho 100 kati ya Wazee 9,000 waliotambuliwa.
Mwanri alisema katika zoezi hilo la kuwatambua na kuwapatia vitambalisho hakuna kumuacha mzee hata mmoja aliye na sifa kwa mujibu wa Sera ya Taifa ya Wazee ya Mwaka 2003.
Alisema baada ya mwezi mmoja kupita Afisa  Ustawi wa Jamii ambaye atakutwa katika Halmashauri yake kuna wazee wenye sifa hawana vitambulisho ajue hana kazi.
Aidha Mkuu wa Mkoa wa Tabora huyo aliwaagiza Waganga Wakuu wa Wilaya (DMO) kuhakikisha kunakuwepo na dawa muhimu na madirisha ya kuwahudumia wazee ili wasitumie muda mwingi kusubiri matibabu.
Alisema kitendo cha kuwachelewesha kinaweza kuwasababisha matatizo kuwa makubwa na kuwepo na uwezekano wa kupoteza maisha.
Mwanri aliwashauri kutenga muda wa kuwahudumia wazee katika maeneo yao na kuhakikisha wanafika Hospitali wanakuwa wa kwanza kupata huduma.
Naye Katibu Tawala Mkoa wa Tabora Msalika Makungu alisema Serikali inawategemea sana wazee hao katika kutoa ushauri ili watendaji wafanye maamuzi sahihi kwa ajili ya maendeleo ya Mkoa na Taifa kwa ujumla.
Alisema wazee ni kundi muhimu kwa watendaji wa ngazi mbalimbali katika kuchotoa uzoefu kutoka kwao ili kuhakikisha Mkoa unasonga mbele.
Awali Afisa Ustawi Mkoa wa Tabora Baraka Makona alisema kwa mujibu wa Sera ya Taifa ya Wazee , Mabaraza ya Wazee yatakiwa kuwa hadi ngazi za Mitaa na Vijiji.
Mwenyekiti wa Baraza la Wazee Mkoa wa Tabora Shidumu Mathew aliishukuru Serikali kwa kuwajali na kuwaomba kusaidia kutatua kero mbalimbali zinazowakabili kama vile kupata matibabu katika mazingira rafiki.
Baraza la Wazee wa Mkoa wa Tabora linajumuisha Mwenyekiti Shidumu Mathew, Makamu Mwenyekiti Maulidi Bakari, Katibu Humbi Shija, Mweka Hazina Sadala Juma, Mjumbe Jumanne Rashid, Naomi Kaswaka na Mumbe Tatu Ramadhan.

No comments:

Post a Comment

Pages