HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

January 16, 2019

BURIANI MBWEZELENI

Picha tofauti zikimuonyesha aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Shirikisho Soka Tanzania (TFF), Hamidu Mbwezeleni enzi za uhai wake.


NA MAKUBURI ALLY
RAIS wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) Wallace Karia amepokea kwa mshituko mkubwa kifo cha aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya shirikisho hilo, Hamidu Mbwezeleni kilichotokea jana.
Kwa mujibu wa Ofisa habari wa TFF, Clifford Ndimbo, Rais Wallace Karia ametuma salamu za rambirambi kwa familia ya Mbwezeleni, ndugu jamaa na marafiki wa soka hapa nchini.
Alisema kipindi cha uhai wake, Mbwezeleni alikuwa mwanamichezo mzuri ambaye alishiriki katika shughuli mbalimbali za soka.
“Kwa niaba ya TFF natoa pole kwa ndugu, jamaa, marafiki na wanafamilia wa soka kwa msiba huu mkubwa,” alisema Karia.
Alisema Mbwezeleni alikuwa ni mwenye weledi katika shughuli mbalimbali alizokuwa akifanya  ambazo alizifanya kwa uhodari.
Katika kipindi chote alichokuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya TFF alifanya kwa moyo wake wote wa kuutumikia mpira wa Tanzania.
Rais Karia amewaomba wafiwa kuwa na subira katika kipindi chote cha msiba na TFF iko karibu nao.
Mbwezeleni atakumbukwa kwa kuwafungia maisha kutojihusisha na shughuli za Soka Makamu wa Rais wa TFF, Michael Wambura kutokana na kupokea fedha zisizo halali kiasi cha Shilingi milioni 84, kugushi nyaraka za malipo, na kula njama kulipwa fedha, adhabu ilianza Machi 15, 2018.
Agosti 27, 2018 Mjumbe wa kanda ya Shinyanga, Mbasha Matutu alifungiwa maisha na kamati ya Mbwezeleni,  Matutu alifungiwa kwa makosa matatu ya kushindwa kutekeleza majukumu yake, ubadhirifu, kughushi na kuiba kinyume na kanuni za Maadili na Ligi Kuu.
Ambako kabla, Mjumbe wa Kanda ya Mtwara na Lindi, Dunstun Mkundi pia alifungiwa maisha kutojihusisha na soka kwa makosa ya kughushi.
Novemba 5, 2018, aliyekuwa Mwenyekiti Kamati ya Uchaguzi ya TFF, Wakili Revocatus Kuuli naye alifungiwa maisha kutojihusisha na soka na Kamati ya Maadili kwa makosa ya kusambaza taarifa alizotumiwa na Katibu Mkuu, Wilfred Kidao.
Kama hiyo haitoshi, Kamati ya maadili iliwafungia maisha, viongozi wa Chama cha Soka Arusha (ARFA), Mwenyekiti Peter Temu, Katibu msaidizi Nassoro Mwarizo.
Wengine ni mweka hazina wa ARFA, Omar Nyambuka na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji wa Chama hicho Hamis Issah alifungiwa miaka mitano.
Pia Kamati ya Mbwezeleni ilimfungia mwaka mmoja Meneja wa timu hiyo, Robert Richard kwa makosa ya maadili.

No comments:

Post a Comment

Pages