HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

March 31, 2019

‘Sanaa Mkalama, Iramba ni sura ya jamii zetu’

Wakazi wa Iramba na Mkalama wakisakata muziki katika tamasha hilo.
 Rais wa Shirikisho la Sanaa za Ufundi na Ubunifu (TAFCA), Adrian Nyangamale akishuhudia zana za jadi za wakazi wa Iramba na Mkalama.

NA MWANDISHI WETU
SHIRIKISHO la Sanaa za Ufundi na Ubunifu (TAFCA) limeeleza kwamba zana za jadi asili ya Wilaya za Mkalama na Iramba ni sura ya jamii zetu kimatendo kwani zinabeba taswira ya maendeleo kimaudhui.
Akizungumza leo katika Tamasha la wenyeji wa wilaya za Mkalama na Iramba mkoani Singida (IDA) lililofanyika kwenye hoteli ya African Heritage Beach Resort iliyoko Kigamboni jijini Dar es Salaam, Rais wa Tafca, Adrian Nyangamale alisema tamasha hilo linawagusa moja kwa moja na kueleza kwamba wataendelea kuwa sambamba na waandaaji wa tamasha hilo ili kuendeleza sanaa hizo.
Nyangamale alisema mojawapo ya mikakati itakayofanikisha Tafca kuwa karibu na IDA ni kupitia mradi wa Utambuzi wa Wasanii Tanzania (TACIP) unaoendelea hapa nchini ambako hadi sasa mikoa ya Mtwara, Dodoma, Pwani na Morogoro imeshapitiwa na mradi huo.
Alisema malengo ya mradi huo ni kufika kila kona na Tanzania na kuwatambua wasanii wa sanaa za ufundi na kuwataka Singida kujiandaa na mradi huo ili mkoa huo upate nafasi ya kujitambulisha kwa serikali ambayo imeandaa mpango huo.
Aidha Nyangamale alisema tamasha hilo ambalo ni la pili kufanyika anatamani lifanyike mkoani Singida kwenye asili ya wakazi wa Mkalama na Iramba ili kuonesha uhalisia wa tukio lenyewe ambalo litaleta mvuto zaidi kwa jamii.
Mkurugenzi wa Ukuzaji Sanaa wa Baraza la Taifa la Sanaa (BASATA), Nsao Shalua alisema tamasha hilo ni kwa ajili ya kuwarithisha vijana wa Singida, tamasha ambalo ni muhimu kwa maendeleo ya sanaa.
Shalua ambaye pia ni Mjumbe wa Tamasha la IDA alisema wazazi wanatakiwa kuwafundisha na kuwarithisha watoto wao tamaduni za makabila yao na kutumia kauli ya baba wa Taifa, Mwalim Julius Kambarage Nyerere aliyewahi kueleza kwamba Taifa lisilo na Utamaduni ni sawa na Taifa mfu.
Mwenyekiti wa tamasha hilo, Dk Alfred Mlima aliweka bayana malengo ya tamasha hilo ni kufahamiana zaidi kwa wakazi wa wilaya hizo na kueleza kwamba tamasha hilo linatumika kama sehemu ya furaha kwao.
“Watu wa jamii moja wakikutana kuna elimu inapatikana kupitia mkutano huo, mtu hawezi kuendelea kama hajui asili yake,” alisema Dk Mlima.
Dk Mlima alisema asilimia kubwa ya Watanzania wanasahau asili yao, hata wao wanasahau hata tiba za mitishamba  ambayo ilikuwa ikiwasaidia na kuhamia kwenye tiba za magharibi.
Naye Mwanamakati wa tamasha hilo, Profesa Amos Majule wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) alisema jamii zetu hazitambui umuhimu wa maliasili zetu kama miti ya Miyombo ambazo zinatakiwa kuenziwa na kutunzwa ili tuendelee kuwa nazo kwani umuhimu wake katika jamii ni muhimu zaidi.
Profesa Majule alisema kupitia tamasha hilo, jamii inatakiwa kuienzi miti ya asili, mali kale na matukio mengine ya kihistoria ili vizazi vijavyo vipate kumbukumbu.
Mwenyekiti wa IDA, Joseph Nsoza alisema lengo la umoja huo ni kukumbuka walipotoka kwani maisha yamebadilika hasa ikizingatiwa vijana wengine wamekimbilia mijini na kusahau walipotoka.
Nsoza alisema wameketi na kugundua kwamba kuna mambo mengi ambayo ni ya asili yanayokosekana kwa vijana wa sasa.
Katika tamasha hilo kulikuwa na matukio mbalimbali kama maonesho ya zana za jadi za mkoa huo, mnyimbo mbalimbali za asili ya makabila ya Wanyiramba na Waikizu, kukimbiza kuku, mchezo wa soka na muziki wa dansi.
Awali kabla ya tamasha hilo, umoja huo ulizindua Ushirika wa Kuweka na Kukopa (SACCOS) na viongozi hao kutoa wito kwa wenyeji wa wilaya hiyo kujitokeza kwa wingi katika umoja huo.

No comments:

Post a Comment

Pages