HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

March 21, 2019

WADAU WATAKIWA KUJITOKEZA MBIO ZA NGORONGORO

Na Mwandishi Wetu

WANARIADHA na wapenzi wa michezo kwa ujumla wametakiwa kujitokeza kwa wingi kujisajili mbio za Ngorongoro ‘Ngorongoro Race 2019 - Half Marathon’ zinazotarajiwa kurindima Karatu mkoani Arusha, Aprili 20 mwaka huu.

Kwa mujibu wa Muandaaji, Meta Petro kutoka Meta Sports Promotions, maandalizi yanakwenda vema na mbio za mwaka huu zitakuwa na msisimko wa hali yake.

Alisema taratibu za usajili tayari zimeanza na walio mbali na Karatu na Arusha wanaweza kujisajili kwa njia ya mtandao wa simu, M-Pesa 0754 82 13 80 (Meta Petro Bare).

Meta, alisema pia usajili unafanyika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid Arusha, Ofisi za Gidabuday Sports Foundation jengo la Namvua Plaza jijini Arusha na Ofisi za Ngorongoro Race mjini Karatu.

Ngorongoro Race 2019 inashirikisha mbio za Kilomita 21 ‘Half Marathon’, Kilomita 5 ‘Fun Run’ na Kilomita 2.5 maalumu kwa watoto.

“Maandalizi yanakwenda vema na tunatarajia washiriki zaidi ya 2,000 mwaka huu, hivyo tunatoa rai kwa wakimbiaji kutoka sehemu mbalimbali ndani na nje ya nchi kuwahi kujisajili mapema kwani zoezi litafungwa rasmi Aprili 15 mwaka huu,” alisema Meta.

Alisema kuwa mbio za mwaka huu, zitashirikisha wanariadha wengi kutoka ndani na nje ya nchi kutokana na uamasishaji uliofanywa na waandaaji, ambao pia wameahidi kuongeza zawadi kwa washindi.

Alibainisha kuwa, mbali na zawadi kwa washindi, wakimbiaji 1,000 wa kwanza watakaofanikiwa kumaliza mbio, kila mmoja atapewa medali yake ya ushiriki.

Muandaaji huyo, alisema medali hizo zinatarajiwa kutua nchini wakati wowote kuanzia sasa kwa ajili ya mbio hizo, ambazo zitaanzia Lango Kuu ya kuingilia na kutokea katika Hifadhi ya Ngorongoro na kumalizikia kwenye viwanja vya Mazingira Bora mjini Karatu.

“Namba kwa wanaotaka kushiriki mbio za kilomita 21 zitatolewa kwa Sh. 20,000 wakati zile za kujifurahisha za kilomita 5, zenyewe zitatolewa kwa Sh. 10,000 na watoto watapewa namba baada ya kutoa Sh. 5,000,” alisema na na kuongeza.

Wameamua mwaka huu kutoa namba kwa watoto kwa gharama ya Sh. 5,000, ili kuwafanya watoto hao kuwa makini na mbio hizo na sio kushirikisha lundo la watoto, ambao hawajajiandaa kwa lolote.

Alibainisha kuwa, tayari shule zaidi ya tano za jijini Arusha zimethibitisha kupeleka zaidi ya watoto 100 katika mbio hizo za mwaka huu, ambazo watoto watakimbia kilometa 2.5.
Akizungumzia maandalizi kwa ujumla, Petro alisema kuwa yanaenda vizuri na wanatarajia kila kitu kitakuwa tayari siku chache kabla ya Aprili 20, ambayo ni siku yenyewe ya mbio hiyo.

Mbali na kuhamasisha ushiriki wa jamii katika michezo na kuimarisha ushirikiano, Ngorongoro Race inahamasisha utamaduni wa kutembelea vivutio vya nchi na kupiga vita ujangili.

No comments:

Post a Comment

Pages