HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

September 29, 2019

Tamasha la kumuenzi Baba wa Taifa laiva Butiama

Mratibu wa Tamasha la  Mwalimu Nyerere, Kulwa Karedia, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana kuhusu kumbukizi ya 20 ya Mwalimu Nyerere inayotarajiwa kufanyika kijijini Butiama mkoani Mara kuanzia Oktoba 8-14. Kushoto ni Mkurugenzi wa Kituo cha Kuhifadhi Utamaduni wa Wazanaki, Mashaka Mgeta. (Na Mpiga Picha Wetu).


NA MWANDISHI WETU

TAMASHA la Pili la Kumuenzi Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere linatarajiwa kufanyika Butiama, Musoma Vijijini mkoani Mara kuanzia Oktoba 8 hadi 14 mwaka huu likishirikisha matukio ya michezo na kongamano.

Akizungumza na Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuhifadhi Utamaduni wa Kizanaki, Mashaka Mugeta, tamasha la mwaka huu litakuwa na kauli mbiu isemayo; “Uadilifu na uchapakazi ni dira kufikia Tanzania ya Viwanda’.

Mugeta, alisema mwaka huu ukiwa wa 20 Tanzania bila Mwalimu, kwa kushirikiana na wadau wengine walioko Butiama wameamua kufanikisha tamasha la pili baada ya lile la mwaka kijijini Butiama.

“Tofauti na matamasha mengine, tamasha hili linafanyika nyumbani alikozaliwa, kukulia na kuzikwa Baba wa Taifa. Kama mnavyojua Mwalimu alikuwa na mambo mengi sana katika kulijenga Taifa hususan uadilifu, upendo, haki, umoja na mshikamano…Na sisi tunapomkumbuka tunapaswa kuvienzi kivitendo,” alisema Mugeta na kuongeza.

Tamasha la mwaka huu limegawanyika katika matukio mawili makubwa, michezo na kongamano, ambako wamewaalika wadau mbalimbali ikiwamo viongozi na mabalozi wa nchi rafiki zikiwamo Mwalimu alizopigania ukombozi wao.

Alibainisha kuwa, tamasha hilo halina itikadi na wanapata ushirikiano mzuri kutoka Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Butiama na Mbunge wa Musoma Vijijini, hivyo yeyote anayetaka kushiriki hakuna kipingamizi.

Pia, wameialika mikoa yote inayopakana na Mara, ambayo ni Kagera, Mwanza, Simiyu na Arusha.
Kwa upande wake Mratibu wa tamasha hilo, Kulwa Karedia, alisema mwaka huu wameboresha zaidi kwa kuongeza matukio.

Alisema mbali na kongamano litazungumzia masuala ya elimu, uhifadhi na mengineyo, katika michezo wameongeza Netiboli ambayo mwaka jana haikuwepo, Soka, Riadha Kilomita 10, Kilomita 5 na Kilomita 2.5 kwa watu wazima, Mbio za Baiskeli na Ngoma za Asili.

Karedia, aliwahakikishia washindi kuwa zawadi ziko za kutosha na zimeboreshwa.

Mgeni rasmi katika tamasha la mwaka huu ambalo limeandaliwa na Maranda Investment, Serengeti Media Centre na Kituo cha Kuhifadhi Utamaduni wa Kizanaki, anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais mstaafu, Jaji Joseph Warioba.

No comments:

Post a Comment

Pages