HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

October 10, 2019

LHRC YASISITIZA KUFUTWA KWA ADHABU YA KIFO

KITUO cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimetoa wito kwa serikali kufuta adhabu ya kifo nchini katika sheria zinazoainisha kosa hilo na kuweka adhabu mbadala. 
 
Wito huo umetolewa jijini Dar es Salaam na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo hicho, Naemy Sillayo wakati wa maadhimisho ya 17 siku ya kupinga adhabu ya kifo, ambapo pia walizindua makala fupi ya video inayohusu wazee walioachiwa baada ya kuhukumiwa kunyongwa. 

Alisema LHRC ni mwanachama wa mtandao wa kupinga adhabu ya kifo duniani ‘’World Coalition Against Death Penalty’’  na wanaendelea kuelimisha umma juu ya madhara yanayoweza kutokana na adhabu hiyo sambamba na kuhamasisha serikali kubadilisha adhabu hiyo kuwa adhabu ya kifungo cha Maisha. 

Alibainisha kuwa kwa mujibu wa Ripoti ya Haki za Binadamu Tanzania,  2018 jumla ya watu 480 wapo kwenye orodha ya watu waliohukumiwa adhabu ya kifo wakiwa gerezani kusubiri kunyongwa.

Aliongeza kuwa, Ibara ya 14 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 1977 inalinda haki ya kuishi kwa kila mtu. Hata hivyo, ibara hii inaathiriwa na Sura ya 16 ya Sheria za Makosa ya Jinai zinazoweka adhabu ya kifo kwa kosa la uhaini, mauaji na ugaidi.

"Pamoja na mtazamo chanya ya Rais John Magufuli ikiwemo kauli aliyoitoa  mwaka 2017  akiwa anamuapisha Jaji Mkuu wa Tanzania Profesa Ibrahim Juma akieleza nia yake ya dhati ya kutokutia saini adhabu hiyo kwa ajili ya utekelezaji pamoja na kuwasamehe wafungwa 61 waliohukuwiwa kunyongwa katika sherehe za uhuru mwaka 2017, bado LHRC inasisitiza uwepo wa utayari wa kufutwa kwa adhabu hiyo katika sheria na kuwa na adhabu ya kifungo cha maisha kama adhabu mbadala. 

"Lengo la wito huu si kuwatetea wahalifu bali ni kupunguza madhara ya adhabu hii ya kikatili kwa jamii na kuendelea kulinda haki ya kuishi. Tunaiomba ibadilishe iweke adhabu nyingine isiyohusisha kuua au kifungo cha maisha," alisema. 

Alitaja baadhi ya sababu za kupinga adhabu hiyo, kuwa ni  ya kikatili na inakiuka haki ya msingi ya kuishi na kudumisha utamaduni wa ‘jicho kwa jicho' pia inapingana na misingi ya haki za binadamu kwa vile ni adhabu ya kikatili inayokatisha haki ya binadamu ya kuishi.

Pia alisema adhabu hiyo ikishatekelezwa haiwezi kubadilishwa, hata kama kuna makosa yametokea na Nchi nyingi duniani zimeendelea kuondoa adhabu ya kifo na kuacha kutekeleza adhabu hiyo.

"Mnamo Oktoba 2, mwaka huu 2019, nchi ya Angola imeridhia mkataba wa nyongeza wa hiari kwenye mkataba wa kimataifa wa haki za kisiasa na kiraia wa 1966 na kufuta adhabu ya kifo katika nchi zao na hivyo kufanya idadi ya nchi zilizoridhia mkataba huo kufikia 88.

" Sababu nyingine ni kwamba waathirika wengi wa adhabu hii ni watu maskini ambao hawana uwezo wa kupata mawakili wabobevu kuwawakilisha katika kesi zao. Pia ni vigumu kuhakikisha kuwa inatekelezwa tu kwa wale watu ambao wametenda na kukutwa na hatia ya kosa hili au wabaya zaidi na adhabu hii haimpi nafasi mtuhumiwa kujirekebisha bali ni ya kulipiza kisasi," alisema.

No comments:

Post a Comment

Pages