HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

January 21, 2020

FLOFRESTA kukutanisha dunia kwenye kilimo hai leo

Na Irene Mark, Moshi
 
 WAKULIMA na wadau wa kilimo hai zaidi ya 12,000 kutoka ndani na nje ya Tanzania wanakutana kesho mjini Moshi, Mkoa wa Kilimanjaro kwa ajili ya maonesho ya mazao mbalimbali yatokanayo na kilimo hai na kubadilishana uzoefu.
Maonesho hayo ya kila mwaka yatafanyika kwenye viwanja vya Ushirika mjini hapa ambapo Naibu Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe, atazungumza na wakulima hao ambapo pamoja na mambo mengine watajadili changamoto za kilimo hai na njia za kukabiliana nazo.
Mshauri wa masuala ya Kilimo Hai kutoka Shirika la kuendeleza Kilimo Hai Tanzania (TOAM), Constantine Akitanda, alisema wakulima na wadau hao wa kilimo hai wanatoka nchi mbalimbali za Afrika, Ulaya na Marekani.
Akitanda alizungumza hayo mbele ya waandishi wa habari zaidi ya 25 wanaopata mafunzo ya siku mbili kuhusu kilimo hai kwa vitendo katika Kituo cha Kilimo Hai cha Mtakatifu Joseph, kilichopo eneo la Kwanyange Mwanga mkoani Kilimanjaro kinachosimamiwa na Kanisa Katoliki Jimbo la Same.
Maonesho hayo yameandaliwa na Shirika lisilo la Serikali lenye makao yake makuu Moshi mkoani humo la (Flora & Fauna Restoration System Tanzania) FLOFRESTA Tanzania, chini ya kaulimbiu isemayo ‘Kufikia uchumi endelevu wa viwanda na uhakika wa chakula kupitia ubunifu wa kilimo endelevu’.
Kwa mujibu wa Akitanda, viongozi wa ngazi na sekta tofauti za Serikali watahudhuria maonesho hayo ili kujifunza mbinu sahihi za kilimo hai na kununua mazao yatokanayo na kilimo hicho.
Mkurugenzi wa FLOFRESTA Tanzania, Richard Mhina alisema lengo la  maonyesho hayo ni kubadilishana uzoefu na kujifunza mbinu bora za kilimo ili kukuza kilimo cha kibiashara katika kufikia uchumi wa viwanda na kuongeza kipato cha familia na taifa.
“Katika maonesho haya tumeshirikiana na wadau wa maendeleo wakiwemo Shirika la Chakula Duniani (FAO), Swiss Aid, Ubalozi wa Ufaransa, TOAM, SAT, NEMC, TAHA, Vyama vya kiraia, Sekta binafsi, Taasisi za utafiti, Wasomi, Viongozi wa dini, Wanasiasa, Wafanyabiashara na ninyi waandishi wa habari.
“Maonesho haya yanatarajiwa kutengeneza na kuongeza fursa za masoko ya bidhaa za kilimo hai miongoni mwa wakulima na walaji, ikihuisisha masoko ya ndani na nje ya nchi… hii ni fursa kwa wasindikaji wa mazao ya mboga na matunda kufanya biashara na kujenga miundombinu imara ya uzalishaji wa malighafi zinazohitajika katika viwanda vidogo vya usindikaji,” alisema Mhina.
Alisema maonesho ay aina hiyo yanafanyika kwa miaka sita mfululizo na vikundi 450 vya wakulima vyenye wanachama 11,294 hushiriki maonyesho ya kilimo, biashara na kupata fursa ya kujifunza mbinubora za kilimo na kusindika mazao ya mboga na matunda.
Mhina alisema FLOFRESTA Tanzania inao mpango wa kuotesha miti ambapo chini ya mpango huo huotesha miti 1,500,000 kila mwaka na  wamefanya hivyo kwa miaka 10 mfululizo.
Alisema miti hiyo huoteshwa pembezoni mwa vyanzo vya maji, maeneo ya wazi, kando ya barabara na kwenye mashamba ya watu binafsi.

No comments:

Post a Comment

Pages