HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

March 02, 2020

Ufaransa yatumia Euro milioni 760 kuchangia maendeleo Tanzania

Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania Fr'ed'eric Clavier(wa tatu kulia) akiwa na maseneta sita kutoka nchini Ufaransa ambao wamekuja nchini kwa ziara ya kutembelea miradi mbalimbali ya maendeleo.
 

Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania, Frederic Clavier, akifafanua jambo wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika leo Machi 2, 2020. Kushoto ni Rais wa Kamati ya Bunge ya Mipango Miji na Maendeleo Endelevu nchini Ufaransa Seneta Herv'e Maurey.
 Balozi Frederic Clavier (wa kwanza kulia) akiteta jambo na Seneta Maurey wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika leo jijini Dar es Salaam.
Seneta Maurey akizungumza wakati wa mkutano wa waandishi wa habari na Balozi Clavier.


Na Irene Mark

SHIRIKA la Maendeleo la Ufaransa (AFD), limetumia zaidi ya Euro milioni 760 kusaidia maendeleo endelevu kwenye sekta ya Maji, Nishati na Afya nchini Tanzania.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Dar es Salaam leo Machi 2,2020 mbele ya maseneta sita kutoka wilaya mbalimbali za Ufaransa, Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania, Frederic Clavier alisema fedha hizo zilitolewa kwa awamu kuanzia mwaka 2009 hadi 2019.


Balozi Clavier alisema hayo mbele ya maseneta hao waliofika nchini na kuanza ziara za kikazi visiwani Zanzibar kisha kwenda mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro, Dodoma na Arusha kuona shughuli za maendeleo zinazofanywa na wadau wanaonufaika na misaada ya AFD.


"Ziara hii ni matokeo ya ziara iliyofanywa hapa nchini Septemba 2018 na Seneta wa kundi marafiki wa Ufaransa na Tanzania na kuazimia kufanya mdahalo utakaowahusisha wadau wa maendeleo ngazi ya jamii na wawakilishi wa nchi mbalimbali.


"...Mdahalo huo mkubwa unaitwa 'Africa-France Summit 2020' utafanyika Juni 4 hadi 6 mwaka huu kwenye jiji la Bordeaux huko Ufaransa, utakuwa fursa nzuri kwa wadau na serikali zao kusikia na kupata uzoefu wa nchi nyingine," alisema Balozi Clavier.


Maseneta hao na wilaya wanazotoka kwenye mabano ni kiongozi wa msafara huo, Rais wa Kamati ya Bunge ya Mipango Miji na Maendeleo Endelevu, Herve Maurey (Eure) na Marta de Cidrac (Yvelines).


Wengine ni Franciise Ramond (Eure-et-Loir), Joel Bogot (Maine-et-Loire), Jerome Bignon (Somme) na Guillaume Gontard (Isere).


Akizungumzia ziara hiyo ya siku saba, Seneta Maurey alisema watatembelea na kuzungumza na wakuu na watumishi wa taasisi zinazonufaika na misaada ya AFD ili kuona namna sahihi ya kuendelea kufadhili miradi husika na changamoto wanazokabiliana nazo kwenye utendaji wao.


"Tukiwa Morogoro tutatembelea Shirika la Kilimo Endeleo Tanzania (SAT), hawa wanahirikiana na ubalozi wetu kufanya mradi wa kilimo ikolojia wakiwa na Mamlaka ya Maji  safi na Maji taka Mji wa Morogoro (MORUWASA)," alisema seneta huyo.


Wakiwa Arusha watatembelea Mamlaka ya Eneo la Wanyamapori (WMA) zilizopo ukanda wa Mbuga ya Taifa ya Tarangire na jijini Dodoma watazungumza na Meya Davis Mwamfupe wakimkaribisha kwenye mkutano wa June huku wakizingatia kuwa ni mji unaokua hivyo kuhitaji mpango bora wa makazi ya kisasa.


Kwa mujibu wa Seneta Maurey, watazungumza pia na Waziri wa Maliasili na Utalii, Hamis Kigwangwala kuona namna bora ya kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi na maendeleo  ya wanyamapori na utalii endelevu.

 
Ziara ya maseneta hao ilianzia visiwani Zanzibar Machi Mosi na itahitimishwa kwenye uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Kilimanjaro Machi 8 mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

Pages