HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

April 21, 2020

WANANCHI CHUKUENI TAHADHARI KWA WAGENI- RC MWANGEL

 Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brig. Jen. Nicodemus Mwangela akipokea mchango wa shilingi 280,000 Kutoka kwa Mchungaji John Mwasakilali Mkuu wa KKKT Jimbo la Magharibi (Songwe) kwa ajili ya mapambano dhidi ya Ugonjwa wa Corona kwa Mkoa wa Songwe.
 Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brig. Jen. Nicodemus Mwangela, akizungumza na viongozi wa KKKT wakati akipokea mchango wa shilingi 280,000 kwa ajili ya mapambano ya Corona ambapo amewataka wananchi kuchukua tahadhari kwa  wageni wanao ingia Mkoa wa Songwe.
 Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brig. Jen. Nicodemus Mwangela akikabidhi  mchango wa shilingi 280,000 Kutoka kanisa KKKT Jimbo la Magharibi (Songwe) kwa Mganga Mkuu wa Mkoa wa Songwe Dkt. Hamad Nyembea kwa ajili ya mapambano dhidi ya Ugonjwa wa Corona.


 Na Mwandishi Wetu

Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brig. Jen. Nicodemus Mwangela amewataka wananchi wote wa Mkoa wa Songwe kuchukua tahadhari kwakuwa sasa kumekuwa na wageni wengi wanao ingia Mkoa wa Songwe kutoka katika Mikoa mbalimbali hasa yenye wagonjwa wengi wa Corona.
Brig. Jen. Mwangela ameyasema hayo mapema leo wakati akipokea mchango wa shilingi 280,000 Kutoka Kanisa la Kiinjili la Kiluteri Tanzania Jimbo la Magharibi (Songwe) kwa ajili ya mapambano dhidi ya Ugonjwa wa Corona kwa Mkoa wa Songwe.
“Kwa sasa Mkoa wetu umeanza kupokea wageni wengi kutoka Mikoa ya Dar es Salaam na hata Zanzibar, hatuwezi kuwazuia kwakuwa nchi yetu ni moja lakini tusaidiane kutoa elimu ya Corona kwa wageni hao na tuchukue tahadhari zote muhimu.”, amesema Brig. Jen. Mwangela.
Ameongeza kuwa kila mwananchi akipata mgeni kutoka mikoa hiyo waangalie namna ya kutenga chumba kwa ajili ya mgeni huyo ili asichangamane na watu wengine au kutoa taarifa kwa uongozi wowote endapo watakuwa na mashaka na hali ya afya ya wageni hao ili waweze kujikinga na ugonjwa wa Corona.
Aidha amewapokeza Kanisa la KKKT kwa kuwa taasisi ya dini ya kwanza kwa kuchangia mapambano ya Corona kwa Mkoa wa Songwe pia kwa kuchukua tahadhari zote muhimu za kujikinga na Corona ikiwa ni pamoja na kutoruhusu watoto wahudhurie ibada.
Brig. Jen. Mwangela amesema taasisi za Dini ziendelee kuchukua tahadhari na kutoa elimu ya kujikinga na ugonjwa wa Virusi vya Corona ikiwa ni pamoja na kuwatembelea waumini majumbani mwao kuwapa elimu hiyo.
Naye Mkuu wa KKKT Jimbo la Mgharibi (Songwe) Mchungaji John Mwasakilali amesema wanampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John P. Magufuli kwa kutofunga shughuli za ibada kwa makanisa hayo.
Mch. Mwasakilali ameongeza kuwa wamechukua tahadhari ya kujikinga na Ugonjwa wa Virusi vya Corona kwa kupunguza muda wa ibada hadi kufikia saa moja, kukaa kwa kuachiana nafasi na kunawa kwa maji tiririka na sabuni na kuwa waumini wake wametii maelekezo ya Serikali.
Ameongeza kwa kuipongeza serikali kwa hatua mbalimbali ilizochukua kama tahadhari ya kuwakinga wananchi dhidi ya ugonjwa wa Virusi vya Corona nao wataendelea kuunga mkono jitihada za serikali kwa kufuata maelekezo na kwa michango mbalimbali pale inapobidi.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Songwe Dkt Hamad Nyembea amesema fedha hizo zilizotolewa na kanisa la KKT zitasaidia kununua baadhi ya vifaa vinavyohitajika katika Kituo cha Afya Nanyala ambacho kimeteuliwa kwa ajili ya kutoa huduma kwa ngazi ya Mkoa endapo atapatikana Mgonjwa wa Corona.
Dkt Nyembea ameongeza kwa kuwaomba wadau  waendelee kujitokeza kuchangia mahitaji mbalimbali kwa ajili ya mapambano dhidi ya ugonjwa wa Corona kwakuwa Vita ya Ugonjwa huo inahitaji ushirikiano wa jamii nzima.

No comments:

Post a Comment

Pages