HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 30, 2020

ALIYEKUWA RAIS WA SERIKALI YA WANAFUNZI CHUO CHA CDTI RUAHA IRINGA APANDISHWA KIZIMBANI

Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Iringa, Mweri Kilimali, akizungumza na waandishi wa habari.
Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Iringa, Mweri Kilimali (kushoto), akimkabidhi mali yake Tarimo Kakiza baada ya kuchukuliwa na wakopeshaji wanaotoa mikopo Umiza.
 


NA DENIS MLOWE, IRINGA

TAASISI ya Kuzuia na Kupambanana na Rushwa mkoa wa Iringa, kwa kushirikiana na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka imemfikisha Mahakamani aliyekuwa Rais wa Wanafunzi wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii Ruaha (CDTI) Christopher Mollel kwa makosa manne.

Akizungumza na wanahabari mkuu wa Takukuru Mkoa wa Iringa, Mweri Kilimali alisema kuwa makosa ambayo yamemfikisha mahakamani Mollel ni kosa la wizi wa sh. Milioni 1,250,000 kinyume na kifungu cha 258(1) kikisomwa pamoja na kifungu cha 265 vya sheria ya kanuni ya adhabu ya sura ya 16 pitio la mwaka 2002.

Kilimali alisema kuwa kosa jingine linalomkabili Christoher Mollel ni kugushi kinyume na vifungu vya 333,335(d) (1) na 337 vya sheria ya kanuni ya adhabu sura ya 16 pitio la mwaka 2002 na kosa jingine ni kuwasilisha maelezo ya uwongo kinyume na kifungu cha 342 kikisomwa pamoja na kifungu cha 337 vya sheria ya kanuni ya adhabu sura ya 16 pitio la mwaka 2002 pamoja.

Aidha alisema kuwa kosa jingine linalompandisha kizimbani ni kosa la kutoa taarifa ya uwongo kwa mtu aliyeajiriwa katika mamlaka ya Umma kinyume na kifungu cha 122(a) cha sheria ya kanuni ya adhabu sura ya 16 pitio la mwaka 2002.

Alisema kuwa makosa hayo yametokana na Takukuru mkoa wa Iringa kubaini kuwa mnamo Oktoba 25 mwaka 2019 mtuhumiwa akiwa Rais wa serikali ya wanafunzi wa chuo hicho alichana na kuiba hundi namba 000063 kutoka katika kitabu cha hundi ya Ruaha CDTI Student Organization kilichokuwa kimehifadhiwa ofisini kwa mshauri wa wanafunzi wa chuo hicho.

“Baada ya kuiba hundi hiyo alijaza taarifa za uongo za kutakiwa kulipwa fedha kiasi cha sh. 1.250,000 ambapo alisaini akiwa mmoja wa watia saini katika akaunti hiyo na kughushi saini ya mtia saini (Mwalimu) wa Pili katika akaunti hiyo” alisema

Aliongeza kuwa uchunguzi ulibaini kuwa mtuhumiwa  Oktoba 26 mwaka 2019 aliwasilisha hundi hiyo namba 000063 ya akaunti 60510007147 katika benki ya NMB tawi la Mkwawa iliyopo Iringa Mjini akiwa ameambatanisha na nakala ya kuwekea Hundi ambayo ilikuwa na maelezo ya kutoa fedha kiasi hicho kutoka akaunti ya Ruaha Cdti student Organization kwenda kwenye akaunti yake binafsi namba 6051.

Kamanda Kilimali alisema kuwa uchunguzi wa tuhuma hizo umekamilika na mtuhumiwa amepandishwa mahakamani leo katika mahakama ya wilaya ya Iringa.

Alitoa wito kwa wakazi wa mkoa wa Iringa kutofumbia macho wanaojihusisha na vitendo vya rushwa na kuwataka wananchi kutoa taarifa sahihi kwa tukukuru ili hatua stahiki zichukuliwe kwa yoyote anayevunja sheria hasa katika masuala ya rushwa.

No comments:

Post a Comment

Pages