HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 04, 2021

KONGAMANO LA ELIMU MKOA WA MARA LATOKA NA MAAZIMIO KUPANDISHA UFAULU

Mkuu wa Wilaya ya Rorya, Simon Odunga ambaye ndiye alikuwa mgeni rasmi na Mwenyekiti wa Kongamano hilo, akizungumza na wadau wa elimu katika Kongamano la Elimu Mkoa wa Mara na uzinduzi mpango wa chakula mashuleni mkoa wa Mara.


Ofisa Elimu Mkoa wa Mara, Bw. Benjamin Oganga akizungumza katika Kongamano la Elimu lililofanyika Wilayani Rorya sambamba na uzinduzi wa mpango wa chakula mashuleni mkoani humo.


Mkuu wa Wilaya ya Rorya, Simon Odunga ambaye ndiye alikuwa mgeni rasmi na Mwenyekiti wa Kongamano hilo, akiendesha mjadala wa wadau wa elimu kwenye kongamano. Kulia ni Mratibu wa Mtandao wa Elimu Tanzania (TEN/MET), Bw. Ochola  Wayoga akifuatilia mjadala huo.

Mratibu wa Mtandao wa Elimu Tanzania (TEN/MET), Bw. Ochola  Wayoga akichangia katika kongamano hilo.


Mkurugenzi wa Shirika la CAMFED, Lydia Wilbard na mjumbe wa bodi ya TEN/MET akichangia katika Kongamano hilo.

Mwenyekiti wa Halmshauri ya Rorya, Gerald Ng'ong'a akichangia maoni yake katika Kongamano hilo.

Mratibu wa Mtandao wa Elimu Tanzania (TEN/MET), Bw. Ochola Wayoga  akisisitiza jambo katika kongamano hilo la wadau wa elimu.

Na Mwandishi Wetu, Rorya

KONGAMANO la elimu Mkoa wa Mara limefanyika sambamba na uzinduzi wa mpango mkakati wa utoaji wa chakula kwa wanafunzi mashuleni ili kusaidia kuinua elimu hasa kiwango cha ufaulu mkoani hapa. Kongamano hilo lililofanyika wilayani Rorya Mkoa wa Mara ni mwendelezo wa Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa yanayoendelea wilayani Rorya katika viwanja vya Obwere-Shirati. 

Akisoma maazimio mara baada ya kongamano hilo lililoshirikisha pia wadau wa elimu toka Mtandao wa Elimu Tanzania (TEN/MET), Ofisa Elimu Mkoa wa Mara, Bw. Benjamin Oganga alisema wameadhimia Mkoa wa Mara kuangali uwezekano wa kutumia walimu wa kujitolea ili kupunguza changamoto za upungufu wa walimu hasa wa sayansi wakati Serikali ikijipanga kuajiri. 

Wameazimia pia kuanzisha mfuko wa elimu wa mkoa utakaosaidia kutoa motisha kwa walimu wanaojitolea, pamoja na kuwekeza zaidi kwenye mbinu za ujifunzaji hasa suala zima la kusoma, kuandika na kuhesabu hasa kwa wanaohitimu darasa la saba wawe wakimudu vizuri kusoma kuandika na kuhesabu.

Alisema azimio lingine ni kuishauri wizara kuangalia uwezekano wa kupandisha kiwango cha ufaulu mitihani kidato cha pili kutoka daraja 'D' kwa kuwa kipimo hiki si sahihi kwa mujibu wa wadau wa elimu, kuhamasisha vijana waliohitimu kidato cha nne na wale wa darasa la saba kujiunga na vyuo vya ufundi ili kuwasaidia na kuongeza vitengo vya elimu jumuishi ili kuwasaidia wanafunzi wenye mahitaji maalum kupata elimu sawa na wenzao. Aliongeza kuwa eneo lingine ambalo wamekubaliana ni kuwajengea uwezo walimu kimafunzo hasa ya ndani kwendana na mabadiliko.

"...Azimio lingine ni pamoja na utoaji wa chakula mashuleni, kuweza kuwasaidia watoto namna nzuri ya kujifunza kwa shule za msingi na sekondari, kuwa na utaratimu na ajenda ya kudumu kwenye shughuli zetu kuwaelimisha wazazi na jamii umuhimu wa kushiriki na kufuatilia taaluma na ujifunzaji na ufundishwaji wa watoto wao na kuwa na takwimu za watoto hasa wanaoacha shule kwa sababu zozote zile kujua wangapi ni Ke na Me,..." aliongeza.

Mkuu wa Wilaya ya Rorya, Simon Odunga ambaye ndiye alikuwa mgeni rasmi na Mwenyekiti wa Kongamano hilo, akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mara alisema maazimio yote yatafanyiwa kazi ili kuleta mabadiliko katika sekta ya elimu kwa umuhimu wake.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mtandao wa Elimu Tanzania (TEN/MET), Bw. Ochola Wayoga akichangia katika kongamano hilo alishauri Mkoa wa Mara kujipanga kutumia walimu wa kujitolea ili kukabiliana na upungufu wa walimu wapatao 6140.

"...upungufu wa walimu unaweza ukapungua kwa kutumia mfumo wa walimu wa kujitolea, cha msingi ni kuangalia ni kwa namna gani kama mkoa tumejipanga kutumia mfumo huu, Tanzania inazalisha karibuni wanafunzi laki nane kila mwaka wa fani ya ualimu na si wote wanaopata ajira moja kwa moja hivyo wanaweza kutumika kupunguza changamoto kama hiyo." Alishauri Bw. Wayoga.

Alisema kuna haja ya kuangalia mfumo wetu wa utoaji elimu kwani ni muda mrefu sasa unatumika bila kufanyiwa tathmini kama bado unahitajika kulingana na changamoto zilizopo. "...Baada ya miaka 60 bado tuna darasa la kwanza, darasa la saba, darasa la sita, kidato cha nne, kidato cha sita, chuo kikuu...tujaribu kujiuliza ni mfumo ambao bado tunauitaji kwa kipidi cha miaka ishirini au kumi ijayo,?

Hata hivyo, aliongeza ya kuwa wadau wa elimu walioshiriki katika Maadhimisho ya Juma la Elimu Wilaya ya Rorya watakuwa ni chachu ya kupunguza changamoto za ufaulu Mkoa wa Mara kwa ujumla, hivyo kuwataka jamii kutumia vizuri fursa hiyo. 

Alitaka kongamano la elimu kutoka na mambo ya msingi, kuyapa kipaumbele katika utekelezaji ili kuhakikisha Mkoa wa Mara unapiga hatua na kusonga mbele kutoka kwenye changamoto ya ufaulu. "Kuweka mipango na mikakati hapa ni sawa lakini kuna haja ya kuangalia mikakati tuliyojiwekea inaingiliana vizuri na ile ya kitaifa, sisikama wadau tunaomba tuendelee kushirikiana ili kuhakikisha kila mtoto anapata elimu iliyo bora na inayokidhi mahitaji," alisema.

Mwenyekiti wa Kongamabo hilo, ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Rorya, Simon Odunga akisisitiza jambo kwa wadau wa elimu.

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Mara, Bw. Samweli Nambatatu akizungumza katika kongamano hilo.


Mdau wa elimu, Richard Mabala a.k.a 'Mwalimu Mabala' ambaye pia ni mwandishi wa vitabu maarufu vya fasihi kidato cha pili kama "Mabala The Farmer" akichangia mada katika mkutano huo wa elimu.


Wadau mbalimbali wa elimu wakifuatilia majadiliano katika kongamano hilo.

No comments:

Post a Comment

Pages