HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

February 11, 2022

JOWUTA, MCT wapongeza Serikali kufungulia magazeti


Mwenyekiti wa JOWUTA, Cloud Gwandu.

 

Mwandishi Wetu

 

CHAMA cha Wafanyakazi wa Vyombo vya Habari Tanzania (JOWUTA) na Baraza la Habari Tanzania (MCT), wamepongeza uamuzi wa Serikali kuyafungulia magazeti ya Mwanahalisi, Mawio, Mseto na Tanzania Daima ambayo yalifungiwa kwa miaka mingi.

 

Taarifa ya kuyafunguliwa magazeti hayo pendwa ilitolewa na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye juzi wakati akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari mbalimbali jijini Dar es Salaam.

 

Akizungumzia uamuzi huo Mwenyekiti wa JOWUTA, Cloud Gwandu alisema uamuzi wa Waziri Nape kutoa leseni kwa magazeti hayo kwa mara nyingine ni wa kupongezwa na kuigwa na watendaji wengine.

 

“Sisi tunampongeza Waziri Nape kwani ametekeleza agizo la Rais Samia Suluhu Hassan alilolitoa wakati anazungumza na wahariri mwaka jana, huo ndio uuongozi. Sisi tunaamini kurejeshwa magazeti haya kutasaidia kundi kubwa la waandishi ambalo lipo mtaani bila kazi,” alisema.

 

Gwandu alisema JOWUTA inapongeza wote waliofanikisha kurejea magazeti hayo, ikiamini kuwa Serikali imeamua kusimamia misngi ya uatawala bora na uhuru wa habari.

 

“Watoto wa mjini wana msemo wao kuwa Rais Samia anaupiga mwingi, kusema kweli katika hili ameupigwa kweli kweli, lakini pongezi za pekee ziende kwa Waziri Nape na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dk. Jim Yonazi, Mkurugenzi wa Idara ya Habari MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa,” alisema.

 

Mwenyekiti huyo alisema JOWUTA inaamini uamuzi wa kufungulia magazeti hayo umezingatia misingi ya utu na kuongeza ajira kwa vijana na Watanzania kwa ujumla.

 

Alisema uamuzi huo umefungua ukurasa mpya kwenye tasnia ya habari, hivyo anawaomba wanaadishi na wamiliki wa vyombo vya habari kuhakikisha wanafuata misingi ya habari ili kuepuka adhabu zisizo na sababu.

 

Gwandu alisema JOWUTA inapongeza Serikali kuunda kamati ya pamoja kati ya Serikali na wawakilishi wa wanahabari kupitia vifungu vya Sheria ya Huduma za Habari ya Mwaka 2016 ambayo imekuwa ikilalamikiwa na wanahabari na wadau wengine.

 

Aidha, JOWUTA inaipongeza Serikali kwa kuongeza muda kwa waandishi wa habari kusoma ili kufikia elimu ya Stashahada (Diploma). Uamuzi huu ni muhimu katika kukuza tasnia hii hasa ikizingatiwa hali ambayo imepitia miaka ya hivi karibuni.

 

Pamoja na pongezi hizo JOWUTA inapenda kuchukua nafasi hii kumuomba Rais Samia na Waziri Nape kuwaagiza wamiliki wa vyombo vya habari kuzingatia sheria ya kazi ambayo inaelekeza wafanyakazi kupewa mikataba ambayo itawezesha kuwepo michango kama ya hifadhi ya jamii, bima ya afya na mingine.

 

Naye Katibu Mtendaji wa MCT, Kajubi Mukajanga, alisema pamoja na pongezi, baraza limepokea kwa furaha ahadi  ya Serikali ya kuanza mchakato wa kuzifanyia marekebisho sheria zinazokandamiza uhuru wa habari na wakujieleza.

 

Kajubi alisema MCT pamoja na wanachama wake 209 linaahidi kushirikiana na Serikali katika maboresho hayo na ni imani yao kuwa yataleta mabadiliko chanya katika kukuza uhuru wa habari na wakujieleza.

No comments:

Post a Comment

Pages