HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

July 07, 2022

NAPE AIPONGEZA TTCL, ataka taasisi kutumia Tehama


NA TATU MOHAMED 


WAZIRI wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye amezitaka taasisi za Serikali kutumia teknolojia ya TEHAMA ya kuendesha mikutano kwa njia ya mtandao (video conference).

Aidha Waziri Nape amelipongeza Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) kwa hatua madhubuti zinazochukuliwa katika kuhakikisha huduma ya TEHAMA inaunganishwa katika ofisi za Serikali na taasisi zake. 
Nape amebainisha hayo alipotembelea Banda la Shirika la TTCL kwenye Maonesho ya 46 ya Kimataifa ya Biashara yanayoendelea Uwanja wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam. 

Nape amesema matumizi hayo ya TEHAMA yatasaidia kiasi kikubwa kupunguza gharama za Serikali huku hatua hiyo pia ikirahisisha mawasiliano kwa shughuli za Serikali na watumishi wake.

“Serikali ipo tayari kuwawezesha kutekeleza mpango huo wa TEHAMA, endelee kufanya kazi nzuri ya kuwahudumia watanzania,” amesema

Akiwa katika Banda hilo la TTCL amepata fursa ya kuona huduma mbalimbali zinazotolewa na shirika hilo ikiwemo huduma ya Faiba Mlangoni kwako, iliyowavutia zaidi wadau wa mawasiliano nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TTCL, Mhandisi Peter Ulanga amesema shirika hilo limejipanga kuhakikisha linaziunganisha taasisi na ofisi za Serikali katika matumizi ya TEHAMA ili kurahisisha shughuli zote za Serikali ikiwemo mikutano.

Amesema TTCL ndiyo mtoa huduma wa kwanza kutekeleza agizo la Serikali la kutumia ‘video comference’ katika mikutano yake na kwamba lengo la Serikali kutaka kutumia huduma hii ni kupunguza gharama na kuwakutanisha watumishi kwa njia ya haraka zaidi.

Amesema mpaka sasa TTCL imeshawaunganisha wateja zaidi  ya 10 mkoani Dodoma ambao wanaendelea kufurahia huduma baada ya kufungiwa mfumo huo.

Akizungumzia huduma ya Faiba Mlangoni, Mhandisi Ulanga amebainisha kuwa huduma hiyo ina umuhimu mkubwa kwa mteja kwani itamwongezea uwezo wa kutumia intaneti kwa haraka na ubora zaidi hivyo kuwashauri wateja kuitumia ili kufurahia mawasiliano rahisi.

Ameongeza kuwa huduma ya Faiba Mlangoni inaingia Sokoni kwa lengo la kubadili soko zima la matumizi ya TEHAMA kwa kuboresha zaidi.


No comments:

Post a Comment

Pages