HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

July 06, 2023

ELIMISHENI WANAWAKE JUU YA FURSA ZA MIKOPO YA HALMASHAURI; MHE. MASANJA

Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mwanza na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary  Masanja amewataka wana Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Mkoani Mwanza kuelimisha wanawake na vijana kuhusu fursa za mikopo ya Halmashauri ili waweze kujiinua kiuchumi.

 Mhe. Masanja ameyasema hayo jana katika Kikao cha Baraza la UWT Wilaya ya Nyamagana kilichofanyika katika Ofisi za CCM jijini Mwanza.

"Niwaombe wakinamama turudi chini tuwaelimishe wanawake wengine kuhusu mikopo hii ya Halmashauri na kuwasimamia kutekeleza miradi yao ili wajiinue kiuchumi" Mhe. Masanja alisisitiza.

Aidha, Mhe. Masanja amewataka wakinamama wa UWT  kuhakikisha wanatoa elimu kwa wananchi juu ya mafanikio ya Serikali kuhusu Utekelezaji wa Miradi mbalimbali ili kuhakikisha Chama kinapata ushindi katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaokuja.

"Sasa tunaenda kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa tusilale wakinamama.
 Sisi ni wenye kura sisi ndio wa kuzitafuta kura usiku na mchana kuhakikisha chama chetu kinaibuka kinara" Mhe. Masanja ameongeza.

Amesema ni lazima kutembea kifua mbele kutokana  na miradi iliyotekelezwa na Rais Samia Suluhu Hassan na kusisitiza kwamba anastahili kupewa maua yake.

Katika kuunga mkono juhudi za Rais Samia za kutangaza utalii,Mhe. Masanja wajumbe wataanza kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii hapa nchini.

Mhe. Masanja anaendelea na ziara yake jijini Mwanza kwa ajili  ya kukutana na makundi mbalimbali ya kijamii yenye uhitaji maalum  ambayo yanajihusisha na biashara mbalimbali.

No comments:

Post a Comment

Pages