HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

July 16, 2023

Jiji la Dar es Salaam lapewa siku 15 kutoa kibali kwa Kampuni ya Givorah Recycling

Na Khadija Kalili

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Dkt. Selemani Jafo leo Jumamosi Julai 15, 2023 ametoa agizo kwa Jiji la Dar es Salaam kuipa kibali Kampuni ya kuchakata na kudhibiti taka ya Givorah Recycling Limited cha kuchukua takataka katika dampo la Pugu Kinyamwezi ambalo linamilikiwa na halmashauri ya Jiji hilo.



Waziri Jafo ametoa agizo hilo wakati akizindua    kiwanda hiko kilichopo Kata ya Mtoni Wlayani Temeke Jiini Dar es Salaam mara baada ya kupokea changamoto iliyowasilishwa kwake kwamba Kiwanda hiko ufanisi wake unazuiwa na upatikanaji wa malighafi taka ambazo wanapokwenda kuchukua katika sehemu zinapopatikana hususani katika dampo la Pugu Kinyamwezi huombwa kibali ili hali wao wanasaidia katika uhifadhi wa mazingira na udhibiti wa taka.

 Dkt. Jafo amesema kuwa, Givorah Recycling  Limited ni miongoni mwa Kampuni ambazo zimetekeleza sheria za nchi , na kukikidhi vigezo vya mazingira hatua ambayo imewawezesha kupata cheti cha mazingira (Environmental Certificate) kinachotolewa na Ofisi yake.

Waziri Jafo  amesema kuwa  Jiji la Dar es Salaam kwa ujumla wake linazalisha taka kati ya tani 6,000 hadi 7,000 kwa siku hivyo ujio wa  Kampuni ya Givorah ni msaada  mkubwa karika kudhibi uchafuzi wa mazingira  Jijini Dar es Salaam  lakini badala yake ameshangazwa kuambiwa Kampuni hiyo changamoto yake kubwa ni upatikanaji wa  malighafi taka na kuzuiwa kuchukua taka  katika dampo la Pugu  Kinyamwezi.

"Jiji la Dar es Salaam linazalisha taka kati ya tani 6,000 hadi 7,000 kwa siku, na Jiji la Dar es Salaam niseme ukweli hatuna dampo la kisasa lakini cha ajabu kiwanda cha kuchakata na kudhibiti taka cha Givorah changamoto yake kubwa ni kupata taka kama malighafi" amesema  kwa mshangao Waziri Jafo na kuongeza

"Nafahamu lile dampo la Pugu Kinyamwezi lipo katika umiliki wa Jiji la Dar es Salaam, nilichosikia ni kwamba Kampuni ya kuchakata na kudhibiti taka ya Givorah Recycling Limited  inahangaikia kupata vibali vya kuruhusiwa kuchukua taka katika dampo la Pugu Kinyamwezi ni maajabu sana, yaani kuna watu wanataka kutusaidia kuchukua taka lakini kibali cha kuchukua taka hakitoki"amesema Waziri Jafo.

Aidha Waziri Jafo ametoa agizo kwa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ifikapo Julai 30, mwaka huu Kampuni ya Givorah Recycling  Limited  iwe imepata kibali  hiki siyo ombi bali ni amri.

Wakati huohuo Waziri Jafo ametoa rai kwa Kampuni hiyo kuwa na vihifadhi taka (dust bin) katika maeneo mbalimbali ikiwemo kwenye Taasisi za serikali kama mashuleni,   Hospitalini, Sokoni na  kwenye mitaa mbalimbali na kwa kuanzia waanze na Wilaya ya Temeke baadaye wasambaze vifaa  hivyo katika  maeneo  ya Dar es Salaam kwa sababu itawarahisishia   kupata malighafi wanayohitaji  kwa ajili ya uzalishaji.

Akiongea kwa niaba ya Mkurugenzi wa Kampuni ya Givorah Recycling Limited , Mwanasheria wa Kampuni hiyo Wakili Shehzada Walli amesema  kuwa, Kampuni hiyo imeweza kukusanya asilimia 30 ya taka zilizozalishwa katika kipindi cha Maonesho ya Biashara (Sabasaba)  mwaka huu na kuongeza kuwa kama siyo wao kukusanya taka hizo zingekweda dampo na hata kuchafua mazingira.

Wakili Walli amesema  kuwa, changamoto yao kuu wanayopata ambayo pia ni ya kushangaza ni kwamba badala ya jamii kuisaidia Kampuni kukusanya taka bure wao wanataka kuuza taka zao jambo linalopelekea Kampuni kupata shida  inapokwenda kukusanya taka na kupunguza ufanisi katika uzalishaji.

Kufuatia hilo Wakili Walli ameiomba serikali kupitia Wizara ya Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira iwasaidie kutoa elimu kwa wananchi kwamba Kampuni yao inatoa mchango katika kulinda na kusafisha mazingira na hivyo wawaunge mkono na kuwapa ushirikiano.

 Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke, Elihuruma Mabelya amesema kwa siku moja taka zinazozalishwa ndani ya manispaa hiyo ni tani 1,400, taka zinazotolewa kwa siku ni tani 964  huku taka ambazo hazipati udhibiti kabisa kwa siku ni tani 379.

Mabelya amesema kuwa, na dampo wanalolitegemea la Pugu Kinyamwezi limezidiwa na hivyo ujio wa kampuni ya Givorah Recycling Limited  imekuwa ni mkombozi katika Halmashauri yetu ya Temeke huku akiahidi   kushirikiana  bega kwa bega na Kampuni hiyo.

Akitoa shukrani kwa  niaba ya wananchi Mstahiki Meya  wa Manispaa  ya Temeke  Abdallah Mtinika amesema kuwa  ujio wa Kampuni ya Givorah Recycling Limited  ni neema na faida kwa wana Temeke huku akitoa ahadi ya   kuwalinda na kushirikiana nao katika utendaji kazi wao wa kila siku na kwamba watakuwa wanawatembelea mara kwa mara ili kuwasikiliza  changamoto zao na kujua mwenendo wao katika uzalishaji.

Mtinika ameongeza kuwa, Miji mingi iliyofanikiwa Duniani na kuonekana inapendeza jambo hilo linatokana na mambo mawili makubwa ambayo ni usimamizi thabiti wa usafi na udhibiti wa taka miongoni  mwa jamii.

Givorah Recycling Limited ni Kampuni inayojishughulisha na ukusanyaji na udhibiti wa taka zote ambazo zinazoweza kutumika tena ikiwa na uwezo wa kuzichakata  (recycle) taka hadi tani 1,000 kwa siku.
Kampuni hiyo ambayo ilianzishwa nchini India ipo pia katika nchi za Marekani, Ulaya, Falme za Kiarabu na mwaka huu imeanzishwa rasmi nchini Tanzania.

Wakati  huohuo  Mheshimiwa Jafo amevipongeza vyombo vya habari kutokana na mchango  wake mkubwa wa kuandika habari mbalimbali  zinazohusu utunzaji  wa mazingira  nchini  na hivi sasa wachuuzi wa miti wametapakaa pembezoni mwa  barabara  wakiuza miti badala ya kuuza machungwa  elimu  mliyoitoa kwa jamii  imezaa matunda na yanaonekana.

Uzinduzi  huo umehudhuriwa na Mkurugenzi  wa Manispaa ya Temeke Elihuruma  Mabelya  ambaye amemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Temeke Mheshimiwa Mobhare Matinyi ambaye ana udhuru.

Wengine waliohudhuria  ni pamoja na Mstahiki Meya  wa Manispaa ya Temeke Abdalah  Mtinika na Mheshimiwa Diwani wa Mtoni Amina Abdullah  Batash.


No comments:

Post a Comment

Pages