HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

December 04, 2016

DKT KALEMANI AMTAKA MKANDARASI UMEME KUFANYA KAZI USIKU NA MCHANA

 Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani (kushoto) akitoa maagizo kwa wakandarasi kutoka Kampuni ya KALPATARU, inayojenga Mfumo wa Usafirishaji Umeme katika Mradi wa Umeme wa Makambako – Songea, kufanya kazi usiku na mchana ili ikamilishe kazi hiyo kwa muda uliopangwa ambao ni miezi minne kutoka sasa. Wa pili kutoka kushoto ni Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Songea Palolet Mgema.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dk. Medard Kalemani (kushoto) akisikiliza maelezo kutoka kwa Kanuti Punguti ambaye ni Meneja wa Kituo cha kufua umeme kilichopo Lizaboni, Songea alipotembelea Kituo hicho jana, akiwa katika ziara ya kazi kukagua utekelezaji wa Miradi ya Umeme katika Mkoa wa Ruvuma. (Picha na Veronica Simba, Songea).

Na Veronica Simba - Songea

Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani ameiagiza Kampuni ya Ukandarasi ya KALPATARU inayojenga Mfumo wa Usafirishaji Umeme katika Mradi wa Umeme wa Makambako – Songea, kufanya kazi usiku na mchana ili ikamilishe kazi hiyo kwa muda uliopangwa ambao ni miezi minne kutoka sasa.

Dkt Medard Kalemani aliyasema hayo jana mkoani Ruvuma akiwa katika ziara kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya umeme na madini.

Akikagua maendeleo ya kazi husika katika maeneo ambayo panajengwa miundombinu ya usafirishaji umeme na vituo vya kusambazia umeme vya Mradi huo mjini Songea, Naibu Waziri aliwataka Maofisa wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) wanaosimamia Mradi huo kuhakikisha wanawasimamia wakandarasi husika ili kuhakikisha wanakamilisha kazi hiyo kwa wakati na kwa kiwango kinachotakiwa.

“Ninawataka mfanye kazi usiku na mchana ili kukamilisha kazi yenu kwa wakati kwani hatutatoa muda wa nyongeza,” alisisitiza.

Akifafanua zaidi, Naibu Waziri alibainisha kuwa, muda uliopangwa kukamilisha kazi ya ujenzi wa mfumo wa usafirishaji umeme ni Machi 2017.

Aliongeza kuwa ni lazima kazi hiyo ikamilike kwa wakati ili kutoa fursa kwa kazi ya ujenzi wa miundombinu mingine ya usafirishaji umeme kukamilishwa kufikia mwezi Desemba mwakani na hivyo kuwezesha shughuli zote kukamilika ifikapo Juni 2018 na wananchi kupata umeme ifikapo mwezi Septemba mwaka huo kama ilivyopangwa.

Kwa upande wa miundombinu ya usambazaji umeme, Dkt Kalemani alisema kuwa, Mkandarasi husika ambaye ni Kampuni ya ISOLUX anatakiwa kuwa amekamilisha ujenzi wake ifikapo mwezi Mei, 2017.

Alisema kuwa, kazi hiyo ni kubwa na itahusisha takribani kilomita 300 ambapo wateja wanaotarajiwa kuunganishwa ni 13,000 na hivyo kutatua matatizo ya umeme kwa Mkoa wa Ruvuma.

Kuhusu utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini wa REA II mkoani Ruvuma, Dkt Kalemani alisema kuwa, mradi huo umekamilika kwa asilimia 100 kwa kazi ya kuweka miundombinu lakini wapo wateja ambao hawajaunganishiwa umeme.

Aliwataka wataalam husika kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Tanesco, kuhakikisha wateja wote ambao wameshalipia umeme waunganishiwe nishati hiyo ndani ya mwezi huu wa Desemba ili kuruhusu REA III kuanza pasipo mabaki ya kazi za REA II.

Mradi wa Makambako – Songea unatekelezwa chini ya Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (Big Results Now-BRN) na unalenga kuunganisha umeme kutoka Makambako hadi Songea na kunufaisha wananchi katika maeneo husika yaani mikoa ya Njombe na Ruvuma.
Mradi huo ni wa umeme wa kilovolti 220 kwa umbali wa kilomita 250 na umelenga kuwanufaisha watu 22,700 katika vijiji 120 vya maeneo husika.

No comments:

Post a Comment

Pages