HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

January 13, 2013

MANCHESTER UNITED YACHINJA JOGOO OLD TRAFFORD




MANCHESTER, England

VINARA wa Ligi Kuu ya England, Manchester United, leo wamezidi kutanua wigo wa pointi kileleni, baada ya kuichapa Liverpool kwa mabao 2-1 katika pambano kali la ligi hiyo kwenye Uwanja wa Old Trafford jijini hapa.

Mpachika mabao wa Mashetani Wekundu, Robin van Persie, alifungua milango ya ushindi kwa bao safi dakika ya 19 akiwa ndani ya boksi, akiitendea haki krosi ya beki na nahodha Patrice Evra, aliyelishwa mpira uliotokana na ushirikiano wa Danny Welbeck, Tom Cleverley na Shinji Kagawa.

Ni bao lililodumua hadi filimbi ya mapumziko ya mwamuzi Howard Webb.

Kipindi cha pili Man United waliendelea kulishambulia lango la Liverpool, ambapo kunako dakika ya 54, beki wa kati wa Man United, Nemanja Vidic aliifungia timu yake bao la pili na kuipa uongozi wa mabao 2-0.

Liverpool ilikuja juu kujaribu kusawazisha mabao hayo, jitihada zilizokuja kuzaa matunda kwa nyota mpya iliyemnasa akitokea Chelsea, Danny Sturridge kuifungia bao la kufutia machozi dakika ya 57 ya mpambano huo uliojaa upinzani na kushambuliana kwa zamu.

Licha ya mabadiliko na jitihada za hapa na pale, hadi filimbi ya mwisho ya Webb matokeo yalibaki kuwa hivyo, ambapo Man United ilitumia vema dimba la nyumbani kwa kushinda mabao 2-0.

Kwa ushindi huo, Man United ikawa imetanua wigo wa pointi zake kufikia 55, pointi 10, juu ya mabingwa watetezi Manchester City, ambao leo usiku wanaumana na Arsenal kwenye Uwanja wa Emirates jijini London.

Liverpool imeendelea kuganda katika nafasi ya nane ya msimamo wa Ligi Kuu, ambayo tayari timu shiriki zimeshuka dimbani mara 22, mechi 16 kabla ya kumalizika kwa msimu huu.

Vikosi, Manchester United: De Gea, Da Silva, Ferdinand, Vidic, Evra, Carrick, Cleverley, Young, Kagawa, Welbeck, van Persie.

Liverpool: Reina, Wisdom, Skrtel, Agger, Johnson, Lucas, Downing, Gerrard, Allen, Sterling, Suarez.

No comments:

Post a Comment

Pages