Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Ernest Mangu akisalimiana na masheikh wa mikoa na maimamu wa misikiti katika ukumbi wa bwalo la maafisa wa Polisi wakati wa kikao cha muendelezo wa kampeni ya familia yetu haina mhalifu kilichoratibiwa na taasisi ya kiislamu ya Mwinyi Baraka.
Na Tamimu Adam, Jeshi la Polisi
Viongozi wa dini wametakiwa kuendelea kufanya
doria za kimwili na kiroho katika
kuimarisha ulinzi na usalama ndani ya jamii ikiwa ni pamoja na kuwajenga vijana katika maadili mema na kuacha kutenda
dhambi ya kujihusisha na vitendo vya
uhalifu.
Rai hiyo imetolewa leo
na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP) Ernest
Mangu alipokutana na viongozi wa dini ya kiislam katika ukumbi wa Bwalo la
maafisa wa Polisi Oysterbay, jijini Dar es salaam. Kikao hicho kiliratibiwa na
taasisi ya kiislamu ya Mwinyi Baraka inayoongozwa na Sheikh Issa othuman.
Kikao hicho kilihudhuriwa
na Mufti wa Tanzania Shabani Simba, Katibu mkuu wa Bakwata, Kadhi Mkuu wa
Zanzibar, Masheikh wa mikoa ya Tanzania bara pamoja Maimamu wa Miskiti.
IGP Mangu alisema kuwa haijawahi kutokea
kokote duniani kwa Polisi kula njama na viongozi wa dini katika kupambana na wahalifu na watenda dhambi, hivyo aliwaomba
viongozi hao wa dini waongeze mahubiri yenye kuwataka waumini kutenda mema pamoja
na kuongeza nguvu ya kuimarisha kamati za ulinzi na usalama katika nyumba za
kuabudia.
Naye, Mufti na Sheikh
Mkuu wa Tanzania Shaban Simba alisema kuwa dini zote zinahimiza waumini
wake kutenda mema na kujiepusha kushiriki katika vitendo viovu, hivyo ameliomba
Jeshi la Polisi kuendelea kuwakamata wale wote watakaobainika kutenda uhalifu
kwani hivi sasa uhalifu upo hata kwenye taasisi za dini.
Kwa upande wake Sheikh
Mkuu wa mkoa wa Arusha Shabani Juma, wakati akitoa salamu za mkoa huo, alisema
kuwa mkoa wa Arusha kwa sasa hivi upo shwari na wa amani, hivyo ni
wajibu wetu kulinda amani tuliyonayo kwani ndio msingi wa kila kitu.
Kikao hicho ni
muendelezo wa mkakati wa Jeshi la Polisi katika kuwajengea uwezo viongozi wa
dini, ambapo viongozi hao wa dini waliazimia
kwa pamoja kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kampeni ya
kutengeneza familia zisizo na wahalifu kupitia mahubili yao pamoja na kuendelea
kuimarisha kamati za ulinzi na usalama katika nyumba za ibada kwa rahisi ya
mawasiliano katika kuwadhibiti wahalifu.
No comments:
Post a Comment