HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

October 28, 2015

CUF WATOA TAMKO ZITO

WAKATI ZEC ikitangaza kufuta  uchaguzi huo na matokeo yake, Chama cha Wananchi (CUF) kimeeleza kutotambua uamuzi huo na kuitaka serikali iiache tume hiyo iendelee na kazi yake ya  kuhesabu, kuhakiki na kutoa matokeo ya uchaguzi huo.

Akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi  baada ya ZEC kutoa tamko hilo, mgombea urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, alisema ameshtushwa na hatua hiyo inayokwenda kinyume na Katiba na Sheria ya Uchaguzi  ya Zanzibar  na kwamba anaichukulia kauli ya mwenyekiti huyo kuwa ni yake binafsi.

“…hiyo ni kauli binafsi ya mwenyekiti huyo hasa baada ya kujiridhisha kuwa hakukuwa na kikao chochote cha tume kilichofikia maamuzi hayo. Mwenyekiti kwa nafasi yake hana mamlaka ya kufuta uchaguzi huo.

“Inaonekana kuna njama za makusudi kutaka kuvuruga demokrasia Zanzibar na kuingiza nchi katika machafuko jambo ambalo sisi kama CUF hatutavumilia,’’alisema Maalim Seif.

Maalim Seif ambaye pia ni Makamu wa kwanza wa rais na Katibu Mkuu wa CUF, alisema Mwenyekiti huyo wa ZEC hakutafakari kwamba kuufuta uchaguzi mkuu Zanzibar kunaathiri pia uchaguzi wa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sababu wapigakura ni walewale waliomo kwenye daftari la wapiga kura la ZEC.

Alieleza kuwa katika kusimamia uchaguzi huo ZEC hufanya kazi ya uwakala wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na hali hiyo inaitia Jamhuri ya Muungano katika taharuki bila sababu yoyote ya msingi kwa sababu rais wa Jamhuri ya Muungano hawezi kupatikana  kwa kupigiwa kura na wananchi wa  Tanzania Bara pekee.

“Sisi tunatambua hatua hii imekuja baada ya majaribio yote ya kutaka  kulazimisha ushindi usiokuwepo wa CCM kushindikana. Uhakiki wa matokeo ya uchaguzi wa majimbo yote 36 ya Unguja  na majimbo manne ya Pemba ulikuwa umekamilika kabla ya zoezi hilo kusitishwa kuthibitisha matokeo ambayo CUF ilikuwa imekusanya.

“Tunatambua kwamba zilikuwepo njama za kutaka kumtangaza mgombea urais wa CCM, Dk. Ali Mohamed Shein, kwa nguvu lakini njama hizo zimeshindikana  kutokana na ukweli uliokuwa ukiibuka kupitia uhakiki wa matokeo ya uchaguzi,” alisema na kuongeza:

“Tunatamka wazi kwamba CUF hatuutambui  uamuzi huo  binafsi wa mwenyekiti wa tume na tunaitaka Serikali ya CCM kuiacha tume iendelee na kazi yake ya uhakiki wa matokeo ya uchaguzi na kisha kumtangaza mshindi,” alisema.

Waliitaka Jumuiya ya Kimataifa na marafiki wa Tanzania kuingilia kati suala hilo hasa kwa sababu waangalizi wa kimataifa wameshuhudia hatua zote pamoja na uhakiki wa matokeo ulivyokuwa unakwenda.

Alisema CUF imeonekana wazi kwamba ni mshindi wa uchaguzi wa rais pamoja na majimbo 18 ya Pemba na mengine 9 ya Unguja, hivyo kuiomba Jumuiya ya Kimataifa isiwaruhusu CCM kukandamiza haki za kidemokrasia za wananchi wa Zanzibar kwa mara nyingine tena.

Maalim alisema hawataishia hapo wanaendelea kufuatilia hilo kwa hatua zaidi kwa kuwasiliana na wahusika mbalimbali ndani na nje ya nchi, ili kupata ufumbuzi wa mgogoro huo unaotengenezwa huku akiwaomba wanachama wao kubaki watulivu na kuitunza amani iliyopo.

“Tunawahakikishia kuwa uvumilivu wao utawapa wanachokitaka na sisi viongozi wao  tutasimamia haki yao kwa njia za amani, lakini za uhakika,” alisema Maalim Seif. CHANZO GAZETI LA TANZANIA DAIMA

No comments:

Post a Comment

Pages