CHAMA cha ACT-Wazalendo kimekuwa na mawasiliano na
Dk. Wilbrod Peter Slaa, mwanasiasa nguli wa upinzani nchini, kuhusu uwezekano
wa yeye kushiriki katika kampeni za Chama chetu kwa lengo la kuendeleza
vita dhidi ya ufisadi nchini.
Tunamshukuru
sana Dk. Slaa kwa imani aliyo nayo juu ya chama chetu na uamuzi wake wa
kuikabidhi rasmi ACT-Wazalendo, mikoba
yake ya vita dhidi ya ufisadi nchini.
Dk. Slaa
anaamini kwamba chama chetu cha ACT-Wazalendo ndicho chama pekee chenye uhalali
na uwezo wa kupambana na ufisadi baada ya chama chake cha zamani kuitelekeza
vita hiyo. Dk. Slaa alikuwa ashiriki kikamilifu katika kampeni za uchaguzi
zinazoendelea kupitia jukwaa la ACT-Wazalendo.
Alikuwa aanze na Mkutano wa hadhara Mjini
Iringa siku ya Jumatano tarehe 7 Oktoba 2015, na baadaye angeendelea na
mikutano mingine katika majimbo mbalimbali na kuhitimisha kampeni hizo katika
Viwanja vya Mwembeyanga Jijini Dar es Salaam, ambao ndio uwanja ambapo vita
dhidi ya ufisadi ilitangazwa rasmi mnamo tarehe 15 Septemba 2007.
Baada ya
tathmini ya kina chama cha ACT-Wazalendo kimejiridhisha kwamba hali ya usalama
wa Dkt Slaa ni ndogo sana kwa sasa kutokana na vitisho mbalimbali anavyovipata.
Kutokana na hali hiyo ya vitisho dhidi ya usalama wake, chama chetu
kimejiridhisha kuwa hakina uwezo wa kumhakikishia Dk. Slaa usalama wake
atakapokuwa majukwaani.
Kwa kuzingatia
maelezo ya hapo juu, chama chetu kimefuta mikutano yote ambayo Dk. Slaa alikuwa
aifanye kupitia jukwaa la ACT-Wazalendo. Chama kitaendelea kutambua mchango
wake katika harakati za kukuza demokrasia na hasa bidii yake ya kujitoa katika
kupambana na ufisadi nchini. Tunamuahidi kwamba chama chetu kitaendeleza vita
hii kwa bidii kubwa na juhudi zake kamwe hazitapotea.
Tunamtakia Dk. Slaa na familia yake maisha
mema.
Samson Mwigamba,
KATIBU MKUU
No comments:
Post a Comment