HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

March 31, 2017

MAJALIWA AWAASA WATANZANIA WAISHIO NJE YA NCHI KUTOJIHUSISHA NA DAWA ZA KULEVYA

“Asema wasithubutu kuingia huko mtafungwa"

NA MWANDISHI WETU

DAWA za kulevya ni moja kati ya vitu vyenye madhara makubwa ambavyo vinachangia kuporomosha uchumi wa Taifa kwa sababu yanaathiri vijana wengi ambao ndiyo nguvu kazi.

Hata hivyo dawa za kulevya zimekua zikiigharimu Serikali kwa kutumia fedha nyingi katika kupambana na athari zitokanazo na matumizi dawa hizo, hivyo imewataka wananchi na jamii kiujumla kutojihusisha na biashara hiyo haramu.

Mbali na dawa hizo kulisababishia Taifa madhara ya kiuchumi na kiafya, pia biashara hiyo ya dawa za kulevya inachafua na kushusha hadhi ya Tanzania kimataifa.

Madhara ya kiafya yanayosababishwa na matumizi ya dawa za kulevya ni pamoja na kuathirika kwa mfumo wa fahamu kwa mtumiaji ikiwa ni pamoja na  kuchanganyikiwa, kuwa na ulevi uliopindukia na hatimaye kusababisha kifo kama mtumiaji atazidisha matumizi.

Katika kuhakikisha biashara hiyo inakomeshwa Serikali imeunda Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini ambayo ndiyo inayoongoza mapambano hayo.

Jumatano ya Machi 22, mwaka huu akiwa nchini Mauritius, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alizungumza na Watanzania waishio nchini huko katika mkutano alioutisha kwenye hoteli ya Meridien mjini Port Louis.

Akizungumza na Watanzania hao aliwataka wajiepushe na masuala yahusuyo dawa za kulevya. Aliwataka Watanzania wote wanaoishi nje ya nchi wazingatie sheria za Taifa husika na kamwe wasijihusishe na biashara haramu ya dawa za kulevya.

“Vita ya dawa za kulevya ni kubwa, hata hivyo Serikali tunaendelea kupambana nayo. Nchi ilikuwa inapoteza vijana ambao walikuwa wamejiingiza katika biashara haramu ya dawa za kulevya. Nawaomba msithubutu kuingia huko mtafungwa,” alisema.

Alisema katika kudhibiti biashara hiyo haramu ya dawa za kulevya Serikali iliamua kuunda Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) na inafanya kazi vizuri. “Na tutakamata kila mtu anayejihusisha na biashara hiyo bila kujali cheo, uwezo na mamlaka aliyonayo,”.

Aliongeza kuwa mamlaka hiyo inafanya kazi ya kutafuta wazalishaji, watumiaji na wafanyabiashara, lengo likiwa ni kuokoa vijana ambao wameshindwa kutimiza ndoto zao kutokana na madhara waliyoyapata baada ya kutumia dawa za kulevya.

Waziri Mkuu alisema kuna Watanzania wengi wamefungwa katika magereza mbalimbali duniani na wengine wamehukumiwa kunyongwa baada ya kuthibitika  kuwa wanajihusisha na matumizi, usafirishaji na uuzaji wa dawa za kulevya, hivyo aliwataka wawe mabalozi wazuri wa Tanzania kwa kujiepusha na dawa za kulevya.

Akizungumzia idadi ya watu ambao hadi sasa wamekwishakamatwa katika nchi mbalimbali, Waziri Mkuu alisema takwimu za jumla zinaonyesha kuwa Watanzania 515 wamekamatwa na kufungwa gerezani kwa makosa ya kujihusisha na biashara ya dawa ya kulevya.

“Nchini China Watanzania walioko magerezani ni zaidi ya 200; Brazili kuna Watanzania 12; Iran wako Watanzania 63; Ethiopia Watanzania saba na Afrika Kusini wako Watanzania 296,” alisema.

Waziri Mkuu aliongeza kwamba “Dawa za kulevya ni hatari sana kwa usalama na ustawi wa Taifa letu. Vita hii inayopiganwa sasa dhidi ya uagizaji, uzalishaji, usambazaji na matumizi ya dawa za kulevya ni kubwa. Sote kwa pamoja tunapaswa kuunga mkono jitihada hizo,” alisisitiza.

Kwa mujibu wa taarifa zililizopatikana ndani ya Jeshi la Magereza Tanzania hadi Machi 26, mwaka huu kulikuwa na wafungwa 512 wanaotumikia vifungo vyao katika magereza mbalimbali kutokana na makosa yanayohusiana na dawa za kulevya, ambapo kati yake wanaume ni 491 na wanawake 21.

Mbali na wafungwa pia kuna mahabusu 1,284 wanaoshikiliwa kwa tuhuma za kujihusisha na utumiaji, usafirishaji na uuzaji wa dawa za kulevya, ambapo kati yao wanaume ni1,166 na wanawake ni 118.

Katika hatua nyinngine, Waziri Mkuu aliwataka Watanzania hao walioko nchini Mauritius kujenga mshikamano wa pamoja na wawe na uzalendo na nchi yao. Pia wawe mabalozi wazuri wa kutangaza vivutio vya Taifa.

Alisema ni vema wakatumia fursa walizonazo katika kutafuta wawekezaji na kuwashawishi waje nchini na kuwekeza kwenye sekta mbalimbali zikiwemo za viwanda, uvuvi, nishati na utalii.

Kwa upande wake, Waziri wa Fedha na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Dkt. Khalid Salum Mohammed aliwaomba Watanzania hao wazidishe mshikamano miongoni mwao kwa kuwa umoja wao ndiyo nguzo yao.

“Mko hapa kwa ajili ya kutafuta elimu na wengine mnafanya kazi, shughuli ambazo  zitawasaidia kuboresha maendeleo yenu na Taifa kwa ujumla, hivyo nawaomba mzingatie kilichowaleta,” amesema.

Dkt. Khalid aliwahakikishia Wanzania hao walioko nje ya nchi kuwa Tanzania  iko salama na wanaendelea kudumisha amani na utulivu kama walivyoiacha wakati walipondoka.

Naye Mwenyekiti wa muda wa Umoja wa Watanzania waishio nchini Mauritius, Bw. Donald Kongwa ambaye ni Ofisa wa benki ya Standard Chartered nchini Mauritius alimuhakikishia Waziri Mkuu kwamba kipato wanachokipata watakitumia kwa kuwekeza Tanzania kwa lengo la kukuza uchumi wa Taifa.

Alisema wanaunga mkono na kupongeza jitihada zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano katika  kujenga uchumi wa viwanda, mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi, ujenzi wa miundombinu ya kisasa, ununuzi wa ndege pamoja na kuimarisha uwajibikaji na nidhamu kwa watumishi wa umma.

Bw. Kongwa alisema Tanzania ina nafasi kubwa ya kujifunza mambo mbalimbali nchini Mauritius kama namna bora ya kuendesha kilimo cha miwa kwa sababu nchi hiyo inazalisha zaidi ya tani 600,000 za sukari kwa mwaka na tani 530,000 inauzwa nje ya nchi.”Tutumie fursa hii kujifunza zaidi ili tuweze kukuza uchumi wetu,”.

Aliongeza kuwa mbali na kujifunza kilimo cha miwa pia Tanzania inaweza kutangaza vivutio vyake vya utalii nchini Mauritius ili kuwawezesha watalii wengi wanaoingia nchini humo kuweza kuvifahamu na hatimaye kuwa nchini. Kwa mwaka Mauritius inapata watalii zaidi ya milioni moja.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
S.L.P 980, DODOMA
IJUMAA, MACHI 31, 2017.

No comments:

Post a Comment

Pages